Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 – Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki

Hon. Dr. Augustine Philip Mahiga

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nominated

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 – Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki

WAZIRI WA MAMBO YA NJE NA USHIRIKIANO WA AFRIKA MASHARIKI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nitumie muda uliobakia kujibu baadhi ya maswali ambayo nimeyasikia kutoka kwa Waheshimiwa Wabunge.

Mheshimiwa Naibu Spika, la kwanza, ni lile linalohusu haki za Wapalestina na watu wa Western Sahara. Katika hotuba yangu nimesema misingi ya Tanzania katika Jumuiya ya Kimatifa ni kuheshimika, kuthamini utu na kulinda uhuru. Kama hilo ndio letu inafuata kwamba wale ambao wamenyimwa uhuru, wamenyimwa utu, lazima washughulikiwe na wapate haki zao. Sasa sisi kama Tanzania lazima tufanye mambo matatu; la kwanza, tutambue kutokuwepo kwa haki hizo kwa watu huku duniani maana yake kama tunalitaka sisi na tunataka wenzetu wapate na hilo hatuwezi kuliacha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini sisi wenyewe Tanzania tumesema ili hilo lipatikane lazima iwe ni diplomasia ya siasa na diplomasia ya siasa kusaidia nchi moja au nyingine inapatikana kwenye majukwaa ya kimataifa. Utazungumzia uhuru na haki na heshima ya Wapalestina au ya Western Sahara kwenye majukwaa muda umepita. Wakati ambapo kutetea haki za Afrika Kusini au Msumbiji au Namibia tulisema tutatumia silaha hatutumii silaha tena, tunasema tutaongea na moja ya silaha zetu ni kwamba tutashiriki kikamilifu katika mijadala ya kimataifa katika majukwaa mbalimbali kuhusu suala la Palestina na suala la POLISARIO. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini wakati huo huo tuna diplomasia ya uchumi; wagomvi wa Palestina ni wa Israeli. Sasa hawa wa Israeli katika diplomasia ya uchumi kuna vitu pale tunaweza kuvipata na sisi tumesema hayo yanayozungumza kuhusu haki za wa Palestina tuyapeleke kwenye vikao, majukwaa ya kimataifa, Tanzania ni peke yake ilikuwa nchi ya kwanza kuipa Palestina diplomatic status hakuna nchi nyingine. Hiyo baada ya Mwalimu Arafati ondoa majeshi yako Uganda alipoondoa majeshi Uganda wakati wa vita akasema tutawapa diplomatic status. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sisi ni watu wa kwanza na nilifanya makusudi kwamba Trump anapokwenda kufungua Jerusalem mimi nafungua Tel Aviv kwa sababu hilo ni kutambua kwamba Jerusalem ni mji wa utata. Nilipokwenda kule kwa makusudi nilisema nipelekeni Gaza Strip pale kwenye kivuko nikaona pale na nimewaambia Waisrael kimacho macho nikasema this is a time bomb lazima muishughulikie suala hili tulizungumze. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika resolutions 12 za Umoja wa Mataifa kuhusu Palestina na kuhusu Israeli nimewaambia pande zote mbili na umoja wa Mataifa wanakubali kwamba tukae tutazame kwamba kuna resolution nyingine zimepitwa na wakati na tufanye zoezi hilo tutazame lakini hatutaweza kuacha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Kabwe leo katika hotuba yangu nimeanza na aya inayosema POLISARIO na imeishia maneno ya POLISARIO sijawasahau. Ni kweli kwamba suala hili linazungumzwa mbele ya Umoja wa Mataifa, lakini maadam tumewaambia Morocco warudi ndani ya Afrika suala hili litaongezewa tija zaidi kama pia Afrika itachangia. Nadhani suala hili sio rahisi kihivyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo, wakati huo huo Morocco ni nchi yenye uchumi mkubwa ya tano ndani ya Afrika, sio uwanja tu wa ndege au uwanja wa mpira au stadium, lakini kuna maeneo hasa katika diplomasia ya kutengeneza mbolea na utalaam na mafunzo ambavyo tunaweza kupata. Hiyo haitatuzuia katika majukwaa yote Afrika and non-aligned countries au Umoja wa Mataifa kuwaambia jamani hili suala tulishughulikie kwa pamoja. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la diplomasia ya uchumi uliojikita kwenye viwanda ili uwe na viwanda na vinavyofanya kazi kuna mambo manne muhimu. La kwanza, ni mtaji lazima kupata investors tupate pesa, kama zinatoka hapa au zinatoka nje. La pili, huwezi kuwa na viwanda kama huna energy, nishati ya kutosha, huwezi kuwa na viwanda kama huna miundombinu mizuri na huwezi kuwa na viwanda kama huna wataalam wanaoshika ule umeme na kufunga na kufungua wale watalii wataalam na hatimaye lazima uwe na soko. Sisi katika kuandaa vijana wetu tumesema hayo unapokwenda kule, hayo ndio uyafuate matano utafute pesa, mtafute wawekezaji, kwenye miundombinu, mtafute watakaoshiriki katika nishati, watakaoweza kutoa mafunzo na masoko ambayo lazima tuwe nayo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa hili linaingia katika kutayarisha vijana wetu wanaokwenda nje kwa miaka miwili tumekuwa tunarudisha watu kuna wengine walikuwa wanakaa miezi na miezi, miaka na miaka hawarudi, tumehakikisha kwamba Balozi zote zinatazamwa na tunarudisha watu. Kurudisha watu ni fedha nyingi sana, tumerudisha 109 katika miaka miwili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa tunaandaa kupeleka vijana ambao wanafanana na haya matano niliyoyasema. Tayari tumeshawatambua na sasa hivi tuko katika ngazi ya upekuzi, lazima wapekuliwe na vyombo vinavyohusika kabla hatujawapeleka. Natumaini hela nitakayopata kutoka bajeti hii ndio itakayotumika kuwapeleka vijana katika vituo vyote. Wote majina yao tumeshayaandaa na tunasubiri wapate kibali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Umoja wa Mataifa ulizaliwa mwaka 1945, leo una wanachama 193. Katika 193 chombo chenye nguvu kupita vyote ni Baraza la Usalama na Baraza la Usalama lina watu wa kudumu Mataifa matano Marekani, Uingereza, Ufaransa, Urusi na China. China isingeingia Security Council bila Tanzania, kabla ya mwaka 70 China ilikuwa inawakilishwa na Taiwan au Formosa au Sheing Tang Sheing lakini sisi Mwalimu akasema haiwezi kuwa Umoja wa Mataifa bila China. Hivyo ikarudi na ndio tuliiweka kule kwenye Security Council.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya mageuzi ya mwisho yalifanyika mwaka 1963 kuongeza Baraza la Usalama kutoka tisa kufika 15, tangu mwaka 1963 hakujawa na mabadiliko. Sasa kuna aina nyingine ya mabadilko, kuna wale wanaosema tuingie na tupewe turufu na hao ni wakubwa Japan, Brazil, German. Ni kwamba hayo mageuzi Afrika nayo inadai ipewe haki kama hizo.

Mheshimiwa Naibu Spika, nawashukuru sana Waheshimiwa Wabunge kwa mchango wao. Maswali mengi nimeyapata na mengi tutayajibu kwa maandishi na haya yataleta tija sana katika kuboresha, kuna mengine ambayo lazima niseme wazi hatuwezi kuyafanya bila nyinyi kutusaidia kupitisha bajeti hii ili tuweze kuendeleza vizuri zaidi kwa pamoja. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi hii. Baada ya kusema hayo, naomba kutoa hoja.