Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 – Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki

Hon. Juma Othman Hija

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tumbatu

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 – Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki

MHE. JUMA OTHMAN HIJA: Mheshimiwa Naibu Spika, nachukua fursa hii kukushukuru wewe kwa kunipatia nafasi ya kutoa mchango wangu katika hotuba ya Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki. Aidha, napenda kumpongeza Mheshimiwa Waziri na watendaji wake wote kwa kutayarisha na kuwasilisha kwa umakini mkubwa hotuba hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika kuchangia hotuba hii napenda kutoa mchango wangu katika maeneo yafuatayo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Uwakilishi wa Tanzania katika Mabunge ya Nje. Napenda kuchukua nafasi hii kutoa pongezi zangu za dhati kwa Waheshimiwa Wabunge wetu waliopata nafasi ya kuteuliwa katika nafasi kwenye Bunge la Afrika. Wabunge hawa wameonesha uwezo mkubwa katika nyanja za kimataifa na kuonesha kuwa Tanzania tunao watu ambao wanaweza katika maeneo ya kimataifa.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na matokeo hayo ya kihistoria yaliyopatikana bado juhudi za uwakilishi wa nchi yetu katika Mabunge hayaridhishi kidogo. Bado kunakosekana uwakilishi katika Mabunge kadhaa kwenye mikutano ya Mabunge. Najua kuwa hali ya uchumi wa nchi yetu bado haijatengemaa vizuri, lakini naiomba Serikali kulipa umuhimu wa kipekee jambo hili la uwakilishi.

Mheshimiwa Naibu Spika, Utafutaji wa Misaada kwa Ajili ya Miradi ya Maendeleo. Napenda kuipongeza Serikali yetu kupitia Wizara hii kwa namna wanavyochukua juhudi za kutafuta misaada kwa wafadhili kwa ajili ya miradi ya maendeleo. Jambo la kutafuta misaada ni jambo la kawaida kwa nchi nyingi ulimwenguni.

Mheshimiwa Naibu Spika, ushauri wangu katika jambo hili ni kwamba, ni vyema Wizara ikawa na wafanyakazi wenye ujuzi wa aina zote hasa za mikataba ya miradi hiyo pamoja na biashara. Hii itatuepusha na ujanja wa mitego ya kisheria za mikataba ambayo mara nyingi baadhi ya wafadhili huwa wanaitumia.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja.