Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 – Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki

Hon. Machano Othman Said

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

House of Representatives

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 – Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki

MHE. MACHANO OTHMAN SAID: Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kupata nafasi hii ya kuchangia mchana huu wa leo. Pia nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri na Naibu wake kwa kutekeleza majukumu yao kwa uadilifu na weledi mkubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, niwapongeze pia Mheshimiwa Masele na Mheshimiwa Mboni kwa nafasi ambazo wamezipata katika Bunge la Afrika.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa haraka haraka nizungumzie baadhi ya majukumu ya Wizara hii na umuhimu wake. Wakati wa bajeti ya Wizara ya Maji Mheshimiwa Waziri wa Maji alizungumzia pia kuhusu mradi wa maji ambao tunatarajia kutoka India. Sasa mradi huu karibu ni mwaka wa tatu naomba Wizara hii nayo itusaidie kutupa maelezo ya ziada kuhusu hatima ya mradi huu wa maji ambao pia na Zanzibar ipo katika mpango huu.

Mheshimiwa Naibu Spika, la pili ni kuhusu Wizara ya Mambo ya Nje katika ofisi za Zanzibar. Baadhi ya Waheshimiwa Wabunge na Kamati naipongeza sana wamezungumzia umuhimu wa kufanywa matengenezo ya jengo la Zanzibar au kujenga jengo jipya. Kwanza nikiri kwamba lile eneo ni nzuri na liko katika sehemu nzuri na niiombe Wizara ijenge au ifanye matengenezo makubwa kwa jengo lile lakini pia na vitendea kazi kwa ofisi ya Zanzibar. Pamoja na watenda kazi wenyewe bado ni tatizo kwa upande wa Zanzibar. Kwa hiyo, natarajia Mheshimiwa Waziri hili nalo atalitilia mkazo na kutuletea majibu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nipongeze uamuzi wa Wizara wa Serikali wa kufungua ofisi ndogo au Council katika Mji wa Guangzhuo na Lubumbashi. Vile vile pia niipongeze sana Serikali kwa kuamua kufungua ubalozi mjini Havana, Cuba kwa masilahi ya Tanzania. Cuba ndio nchi ya kwanza kutambua Mapinduzi ya Zanzibar mwaka 64, kwa hivyo kwa Cuba, Tanzania ni rafiki wao wa kudumu kwa hivyo nimefurahi nawashukuru na kuwapongeza Wizara kwamba mwaka huu pengine tunaweza tukafungua Ubalozi nchini Cuba.

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine suala la Mahujaji, Mheshimiwa Masoud alizungumza lakini mimi kidogo na tofautiana naye. Ni kweli tunazo fursa na uhuru wa makundi kupeleka mahujaji Makka, lakini mwaka jana kupitia makundi haya haya mahujaji wa Tanzania walipata tabu sana nchini Saudi Arabia. Wengine walitapeliwa na imefikia hatua Serikali ya Saudia kuagiza mahujaji wa Tanzania mwaka huu walipiwe mwanzo kabla ya wakati wa Hija ili kuepusha tatizo hili.

Mheshimiwa Naibu Spika, tatizo ambalo limewasababisha baadhi ya mahujaji kuwa katika wakati mgumu kwa sababu kwa utaratibu Mahujaji wanachanga fedha kidogo kidogo ili wawahi nao kutekeleza ibada. Sasa kwa uamuzi huu imekuwa kazi kubwa sana na ngumu. Nimwombe Waziri pia kwa sababu masuala haya ya dini pamoja na kwamba ni Tanzania lakini yanashughulikiwa sehemu mbalimbali, kulikuwa na wazo kwa mahujaji wa Zanzibar kufunguliwa akaunti yao peke yao na mahujaji kutoka Bara wawe na akaunti yao. Sasa sijui Serikali ya Jamhuri ya Muungano imefikia wapi katika suala hili la kuweka sawa ili kupunguza hili suala la utapeli kwa mahujaji wetu na kuweza kupata huduma nzuri katika mji wa Maka. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine ni kuhusu Ubalozi wetu Msumbiji. Msumbiji ukiacha lile jengo kubwa ambalo tumejenga la ghorofa tisa liko kwenye sehemu nzuri lakini pia tunayo majengo mengine yasiyopungua mawili mpaka matatu. Maeneo ambayo tumepewa Msumbiji ni mazuri na wenyewe Msumbiji wanaona wametuheshimu sana kutupa maeneo yale, lakini kwa bahati mbaya tumeshindwa kuyaendeleza.

Mheshimiwa Naibu Spika, nashauri Wizara kama ingewezekana wangebadilisha matumizi ya lile jengo jipya badala ya kulitumia kwa Ofisi ya Ubalozi, tungelitumia kwa kituo cha biashara na yale majengo mengine tukayajenga na tukatumia kwa shughuli za kibalozi ambayo yanatosha sana. Yaani pale fedha nyingi tumetumia lakini tuna maeneo mazuri tunaweza tukawa vizuri zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini hata wao Msumbiji Tanzania yapo maeneo bado wanadai kwamba walipewa na wamenyang’anywa katika utaratibu ambao hauko wazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja.