Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadilio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Maliasili na Utalii

Hon. Oran Manase Njeza

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbeya Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadilio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Maliasili na Utalii

MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Spika, napenda kuchukua nafasi hii kumpongeza Waziri, Naibu Waziri na timu nzima ya wataalam wa Wizara ya Maliasili na Utalii kwa hotuba nzuri ya bajeti.

Mheshimiwa Spika, pamoja na jitihada za Serikali kuwekeza katika maliasili zetu bado kuna changamoto nyingi za migogoro ya mipaka kati ya hifadhi za wananchi.

Mheshimiwa Spika, wananchi wa Wilaya ya Mbeya wamekuwa wadau wakubwa wa hifadhi zetu ikiwemo Hifadhi ya Kitulo na Hifadhi ya Misitu ya Kata ya Inyala. Kuna mgogoro wa muda mrefu kati ya TANAPA (Hifadhi ya Kitulo) na wananchi wa Kata za Ilungu, Igoma na Ulenje. Pamoja na juhudi za Serikali za kutatua mgogoro huu, pia Mheshimiwa John Pombe Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania aliahidi kumaliza mgogoro huu kwa kuwafidia wananchi zaidi ya 600 waliopisha maeneo yao kwa ajili hifadhi.

Mheshimiwa Spika, inaelekea TANAPA kwa kushirikiana na Serikali ya Mkoa wa Mbeya badala ya kumaliza mgogoro wameanza kuchochea chuki na wananchi pasipo kushirikisha uongozi wa chini ikiwemo vijiji na Halmashauri. Wameanza kuchukua hatua za kutaka kuhamisha wananchi wa Kijiji cha Kikondo na kukipeleka kwenye Hifadhi ya Msitu wa Kijiji cha Ilungu ambacho ni chanzo kikubwa cha maji na kimekuwepo kisheria kabla ya uhuru. Bila kushirikisha Serikali Kijiji cna Baraza la Madiwani TANAPA wameenda kupima hekta 800 kwa ajili ya kuhamisha wananchi wa Kijiji cha Kikondo ambacho kipo kisheria.

Mheshimiwa Spika, wananchi wanajiuliza ni kwa nini kuhamishia wananchi kwenye hifadhi ambayo ni chanzo muhimu cha maji? Hata hivyo, wadai ni zaidi ya 600 ambao walihakikiwa tangu awali, miaka zaidi ya mitano iliyopita na si 20 wanaokusudiwa kupata fidia.

Mheshimiwa Spika, hatua zinazoshawishiwa na TANAPA zinachochea migogoro isiyokuwa ya lazima, ukichukulia hawa wananchi ndio wanaotegemewa na Serikali katika kulinda hifadhi hizi. Hifadhi ya kituo na misitu ya Kata ya Ilungu ni muhimu sana kwa ajili ya vyanzo vya maji ikiwemo Mto Ruaha. Pamoja na mgogoro wa hifadhi ya Kitulo, wananchi wa vijiji vya Kata ya Inyala wameporwa maeneo yao na TFS. Naomba Serikali kuchukua hatua za kutatua mgogoro huu ambao eneo lililochukuliwa kinyemela ni dogo sana ukilinganisha na athari za mgogoro.

Mheshimiwa Spika, wananchi wa Kijiji cha Mjele, Kitongoji cha Mtakuja, wanapata usumbufu mkubwa kutoka TFS na mara kwa mara wamekuwa wanapata usumbufu wa kuchomewa nyumba zao na kuharibu mazao yao kwa mazingira ya uonevu. Serikali irekebishe hii mipaka ambayo wananchi wapo hapo kabla ya mwaka 1940.