Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadilio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Maliasili na Utalii

Hon. Constantine John Kanyasu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Geita Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadilio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Maliasili na Utalii

MHE. CONSTANTINE J. KANYASU: Mheshimiwa Spika, kuhusu matumizi ya nishati ya mkaa na kuni kwa taasisi, nimesoma ushauri wa Waziri kwa taasisi kutumia nishati mbadala. Ushauri huu hauonekani kuwa ni msisitizo wa kuokoa misitu. Naishauri Serikali kuleta sheria ambayo itazilazimisha taasisi kuweka mkakati wa matumizi ya gesi badala ya kuni au mkaa. Pamoja na sheria hiyo Serikali itoe punguzo la kodi maalum kwa vifaa vya gesi yenyewe kwa taasisi zilizo tayari ambazo zitatambuliwa. Jambo hili iwapo litafanyika litasaidia kupunguza matumizi ya kuni na mkaa kwa sehemu kubwa.

Mheshimiwa Spika, suala la mipaka mipya ya hifadhi, naunga mkono maoni ya Kamati juu ya kuondoa kabisa mipaka mipya ya mbuga na hifadhi kwenye vijiji na nchi nzima kwa ujumla. Mipaka hii imeleta tafrani kubwa na imekiuka kabisa mipaka ya asili iliyowekwa kwa mujibu wa GN na sheria za nchi hii. Mipaka mipya isimame mpaka ushirikishwaji utakapofanyika.

Mheshimiwa Spika, kuhusu kesi za mifugo inayokamatwa, baadhi ya mifugo imekuwa ikikamatwa ndani ya hifadhi au mbuga za wanyama na Serikali kuzishikilia kwa muda mrefu. Kwa kuwa askari wa wanyamapori hawana utaalam wa mifugo, mifugo mingi huwa inakufa na Serikali na wananchi kupata hasara kubwa. Kwa mfano mwaka 2014/2015 huko Ngara Tanzania mifugo (ng’ombe) 887 ilikamatwa ndani ya hifadhi, mifugo 700 ilikufa kabla ya maamuzi ya Mahakama na hata waliobaki walikosa bei ya soko kwani walikuwa wamekonda sana.

Naishauri Serikali kubadilisha utaratibu wa kushikilia mifugo, badala yake iachwe kwa mtuhumiwa kwa uangalizi maalum mpaka kesi ya msingi itakapoamuliwa.