Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadilio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Maliasili na Utalii

Hon. Selemani Moshi Kakoso

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mpanda Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadilio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Maliasili na Utalii

MHE. MOSHI S. KAKOSO: Mheshimiwa Spika, awali ya yote nikupongeze Mheshimiwa Waziri kwa kazi kubwa unayoifanya ya kulinda maliasili ya nchi hii.

Mheshimiwa Spika, nizungumzie juu ya utalii wa Ukanda wa Magharabi, Mikoa ya Rukwa, Katavi na Kigoma. Eneo hili la ukanda huu Serikali haijawekeza kabisa ambao una vivutio vingi vya utalii. Mkoa wa Rukwa kuna maporomoko ya Kalambo na Ziwa Rukwa na misitu mizuri ya kuvutia. Mkoa wa Katavi una mbuga nzuri ya Katavi National Park, mbuga ambayo ina wanyama wakubwa wenye afya njema na ndiyo mbuga pekee yenye twiga mweupe anayepatikana Katavi peke yake.

Mheshimiwa Spika, tunaomba mbuga hii muitangaze sambamba na kuweka miundombinu ya maji ili kunusuru wanyama wanokufa kwa kukosa maji wakati wa kiangazi Mto Katuma unapokauka.

Mheshimiwa Spika, Mkoa wa Kigoma kuna mbuga ya Mahale jirani na Mkoa wa Katavi na Hifadhi ya Gombe. Mheshimiwa Waziri tunaomba ukanda huu utengwe kwa ajili ya utalii. Sambamba na hilo kuna fukwe nzuri ya Ziwa Tanganyika ambako watalii wengi wa kutoka nchi ya Israel wangependa sana kufanya utalii wa boti ndani ya Ziwa Tanganyika. Tatizo kubwa bado miundombinu ya kuvutia watalii haijawekwa. Tunaomba Wizara yako muweke mikakati ya kuwekeza katika kuweka miundombinu zikiwemo ununuzi wa boti ya kisasa na kushawishi wawekezaji wa kujenga hoteli za kisasa.

Mheshimiwa Spika, nitoe shukrani za dhati kwako wewe Mheshimiwa Waziri kwa kuidhinisha Pori la Tongwe Magharibi kumilikiwa na Halmashauri ya Wilaya ya Tanganyika. Mheshimiwa Waziri Wana Tanganyika wanakuombea kwa Mwenyezi Mungu akuongoze vyema katika majukumu yako ya Wizara. Pia nakupongeza na kukushukuru sana kwa kutupatia gari ya doria Wilaya ya Tanganyika. Tunaahidi tutalifanyia kazi na kulitunza kwa ajili ya uhifadhi wa mazingira.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja.