Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadilio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Maliasili na Utalii

Hon. Silafu Jumbe Maufi

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadilio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Maliasili na Utalii

MHE. SILAFU J. MAUFI: Mheshimiwa Spika, napenda kuwapongeza kwa kazi nzito waifanyao Waziri, Naibu Waziri, Katibu Mkuu na baadhi ya wataalam wafanyao kazi kwa weledi na kwa maslahi kwa nchi yetu. Wizara hii inatoa pato au inachangia kwa asilimia ya kutosha kwenye pato la Taifa. Kama miundombinu yake ikiboreshewa ipasavyo na kwa kukubali maoni, ushauri wa Wabunge na Kamati husika ni dhahiri pato la Taifa litaongezeka hadi asilimia 10 -15.

Mheshimiwa Spika, Wizara hii imekuwa na upungufu wa watumishi wenye mafundisho sahihi kwa kada mbalimbali za kutoa huduma kwa watalii na wabunifu wa shughuli kadhaa za kuwavutia watalii kwenye maeneo yetu kuzingatia mazingira yetu. Vyuo vya Utalii kuongezeka kwa idadi ya usaili na miundombinu ya kuikabili hali na mahitaji ya wataalam. Mitaala iendane na mahitaji ya kuwa na utalii endelevu uendao na wakati wa maendeleo ya utalii ulimwenguni.

Mheshimiwa Spika, kutokana na kwamba eneo kubwa la utalii linahitajika ulinzi na usalama kwa wageni na nchi kwa ujumla wake, ni vyema usaili wa watumishi wa Wizara hii watokane na vijana wa JKT pia.

Mheshimiwa Spika, bado Serikali haijasambaza nishati mbadala kwa matumizi ya wananchi wetu kwa huduma mbadala ya nishati ya kuni na mkaa. Ni vema Wizara ikajikita katika kuhakikisha tunapata umeme wa kutosha na gesi na kupelekea gharama yake kuwa rafiki kwetu na wananchi kuelimika na kuikubali hali ya matumizi hayo kutapunguza uharibifu wa misitu yetu.

Mheshimiwa Spika, wakati huu tunalazimika pia kuangalia tozo zitolewazo kwa wajasiriamali wa uuzaji wa mkaa mpaka afikishapo mjini kutoka vijijini ni kubwa ukichanganya na changamoto azipatazo katika kuupata mkaa na kuusafirisha.

Mheshimiwa Spika, baadhi ya watumshi wakusanyao maduhuli ya misitu vijijini si waaminifu, ni bora uwepo utaratibu wa kutumia mashine za kieletroniki, kudhibiti makusanyo hayo kwa kuwapa malengo.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa tumekubaliana kuendeleza utalii Nyanda za Juu Kusini, tunaomba Wizara kuwa na utaratibu wa awali kabisa kuimarisha miundombinu (barabara) inayoelekea kwenye maeneo ya vivutio vilivyobainishwa kwenye maeneo yetu, naomba ushauri kuzingatiwa. Kwa mfano barabara inayoelekea Kalambo Falls – Rukwa.

Mheshimiwa Spika, naomba kuunga mkono hoja.