Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadilio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Maliasili na Utalii

Hon. Zuberi Mohamedi Kuchauka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Liwale

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadilio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Maliasili na Utalii

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Spika, leo naomba mchango kwenye Wizara hii kwa kujadili namna ya migogoro ya mipaka kati ya hifadhi na vijiji vinavyozunguka hifadhi zetu kwani migogoro hii imedumu kwa muda mrefu na kurudisha nyuma hali ya mahusiano ya wahifadhi na wananchi pia hata na Serikali kwa ujumla. Kwa mfano katika Wilaya ya Liwale kuna mgogoro mkubwa na wa muda mrefu kati ya Hifadhi ya Selous na Kijiji cha Kikulyungu. Hadi sasa mgogoro huu umegharimu maisha ya watu wake katika kijiji hicho. Ni muda mrefu sasa mgogoro huu haujapewa kipaumbele licha ya kugharimu maisha ya watu.

Mheshimiwa Spika, unapozungumza juu ya malikale utakuwa unafanya dhambi kama ukiacha kumbukumbu zilizoachwa wakati wa Vita ya Maji Maji na utawala wa Wajerumani hapa nchini. Wizara bado ina kazi ngumu na muhimu sana ya kutambua majengo na alama mbalimbali za malikale kwa faida ya utalii na urithi wa nchi yetu kwa majengo mengi nchini yamesahauliwa hivyo kupoteza historia ya nchi yetu. Kwa mfano katika Wilaya ya Liwale kuna Boma la Mjerumani, boma hili lina kumbukumbu nzuri na nyingi sana hasa ya Vita ya Maji Maji. Mawe ya kujengea jengo hili yametoka Wilayani Kilwa, zaidi ya kilometa 250 kutoka Liwale, mawe hayo yalibebwa na watumwa.

Mheshimiwa Spika, kuna mabaki na picha za mashujaa na watawala wa Kijerumani waliotawala Ukanda wa Kusini. Kama haitoshi vilevile kuna kumbukumbu ya Mfaransa inayojulikana kama Mikukuyumbu, hapa ndipo mzungu wa kwanza kuingia Liwale aliuawa na mtu ajulikanaye kama Mchimae. Huyu ni mzungu ajulikanaye kama (Mfaransa). Kumbukumbu zote hizo zimesahauliwa sana.

Mheshimiwa Spika, Pori la Akiba la Selous kwa upande wa Ukanda wa Kusini hauna lango la utalii wa picha kwani kuna utalii wa uwindaji tu, jambo hili linakosesha mapato katika ukanda huo na watu wa ukanda huo kukosa kuona faida ya kuwepo kwa Selous Ukanda wa Liwale. Tunahitaji lango la utalii wa picha ili kuongeza ajira na mapato ya Halmashauri yetu ya Liwale.

Mheshimiwa Spika, hadi leo Liwale zaidi ya kushambuliwa na tembo na wanyama wakali hakuna faida ya moja kwa moja kwa wananchi kwa kukosa lango la utalii wa picha. Hivyo, kukosa wawekezaji wa mahoteli na miundombinu mingine ya kiutalii.

Mheshimiwa Spika, Halmshauri zinazopakana na hifadhi zinatakiwa kupata asilimia 25 ya mapato ya hifadhi husika. Naomba Wizara kupitia upya sheria hii kwani kiasi hiki ni kidogo sana kwa sasa, ni bora kiasi hiki kikaongezwa kufikia asilimia 30. Vilevile fedha hizi zinachelewa sana kufika kwenye Halmashauri zetu.

Mheshimiwa Spika, kuhusu malipo ya kifuta machozi na fidia ya uharibifu wa wanyama pori, fedha hizi licha ya kuwa ni kiasi kidogo lakini hata utaratibu wa upatikanaji wake bado hauko wazi, haueleweki kwa watu wetu jambo linalofanya watu wetu kutopata fidia yoyote licha ya wengine kupata vilema na mashamba yao kuliwa na wanyama kama tembo, nyati na kadhalika. Malipo ya kifuta machozi ni kama danganya toto kwani walio wengi hawapati. Kwa mfano Halmashauri ya Liwale ina muda mrefu sasa watu hawajawahi kupata malipo haya licha ya kuwa na madai ya muda mrefu zaidi ya miaka mitano.

Mheshimiwa Spika, naomba Serikali ipitie upya sheria ya TFS kwani wakala huyu anavuna mazao ya misitu ya vijiji hata ile ya open area kiasi kinachokibaki kwenye Halmashauri ni kidogo sana. Misitu inakwisha lakini Halmashauri inakosa mapato ya moja kwa moja kutoka TFS jambo linaloleta mahusiano ya mabaya kati ya TFS na wananchi wa kawaida kwani hakuna faida ya moja kwa moja kutokana na uvunaji huu wa TFS. Kwa mfano katika Wilaya ya Liwale mahusiano ya TFS na wananchi si mazuri kutokana na watu wetu kutoona manufaa ya moja kwa moja kutoka kwenye taasisi hii.