Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadilio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Maliasili na Utalii

Hon. Nape Moses Nnauye

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mtama

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadilio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Maliasili na Utalii

MHE. NAPE M. NNAUYE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi na mimi nichangie. Kama Mwenyekiti wa Kamati ya Ardhi, Maliasili na Utalii nichukue nafasi hii kwa niaba ya Kamati kuwashukuru Waziri na Naibu Waziri na Katibu Mkuu wake pamoja na watendaji wa taasisi zilizo chini ya Wizara hii kwa ushirikiano mkubwa ambao walitupa wakati wa kutekeleza kazi zetu kama Kamati. Kwa kweli wametupa ushirikiano mkubwa, kwa hiyo, nimshukuru sana Waziri, Naibu wake, Katibu Mkuu na watendaji chini ya Wizara hii kwa ushirikiano wao.

Mheshimiwa Spika, nilisema nichangie jambo moja hapa kubwa. Wakati tunakamilisha Taarifa ya Kamati, tarehe 25 Aprili, 2018 Tanzania Forest Services walitangaza tender ya kukata miti kwenye Pori la Akiba la Hifadhi la Selous. Tender hii inahusisha ukataji wa miti zaidi ya cubic meter 3,495,362, na point fulani. Maelezo, ukisikiliza tafsiri ya idadi ya miti itakayokatwa wanasema ni karibia ukubwa wa Mkoa mzima wa Dar es Salaam na zaidi yake na wapo wengine wanasema ni ukubwa wa Unguja nzima. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa eneo hili ni kubwa sana kukatwa ndani ya Hifadhi ya Taifa ambayo inaliletea heshima nchi yetu hifadhi hii, ni kubwa sana kiasi kwamba imenishtua sana.

Mheshimiwa Spika, lakini itakumbukwa Bunge hili lilitunga sheria mwaka 2004, Sheria Na. 20 ya mwaka 2004 ya Usimamizi wa Mazingira. Katika sheria ile sehemu ya saba ya sheria ile inazungumza tathmini ya mazingira kimkakati. Naomba niinukuu, inasema hivi:-

“Iwapo rasilimali ya madini au mafuta itagundulika kabla ya mpango wowote au kabla ya kuwa na mpango wa kujenga kituo cha nishati ya umeme wa maji haujafanyika Waziri mwenye dhamana ya masuala ya madini, nishati au maji atafanya tathmini ya mazingira ya kimkakati.” (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunavyoongea, tathmini hii haijakamilika, tathmini hii bado inaendelea, TFS wametangaza tender ya kukata miti hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sehemu ya pili ya sheria hii inasema hivi:-

“Tathmini ya mazingira kimkakati iliyotajwa chini ya kifungu cha kwanza itatathmini eneo lililotengwa kwa ajili ya shughuli husika pamoja na mambo yafuatayo; la kwanza; hali halisi ya mazingira na ya maliasili, utambuzi wa maeneo nyeti kiikolojia yanayolindwa, utambuzi na maelezo kuhusu jamii zinazolizunguka eneo husika, hali halisi ya kiuchumi, ya jamii iliyopo, shughuli za kiuchumi na miundombinu…”

Mheshimiwa Spika, na yako mengine muda hautoshi kusoma. (Makofi)

Sasa nataka nimuombe AG aisaidie Serikali kujenga utamaduni wa kuheshimu sheria zilizopitishwa na Bunge. Kwa unyenyekevu sana, Serikali naiomba isitishe zoezi hili, isubiri tathmini ya kimkakati ya mazingira ikamilike. Hifadhi hii ya Selous inahusisha mikoa mitano, Morogoro, Pwani, Lindi, Mtwara na Ruvuma. Haiwezekani tukapuuza maisha ya watu, wanyama, mimea na viumbe mbalimbali katika mikoa mitano ya nchi, tunaamua kwenda kukata miti yote hii; napata taabu, inaingiaje akilini? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi nilidhani tungesubiri tathmini hii ikafanyika, ikija hata kama tunataka kuendelea na mradi, tathmini itatuambia wapi tukanyage, wapi tusikanyage, tutaokoa maisha ya watu hawa. Maisha ya kwetu sisi kule baada ya gesi kuyumba ni korosho, ufuta, mbaazi na mazao mengine.