Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadilio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Maliasili na Utalii

Hon. Dr. Stephen Lemomo Kiruswa Mamasita

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Longido

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadilio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Maliasili na Utalii

MHE. DKT. STEVEN L. KIRUSWA: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi ili nami niweze kutoa mchango wangu katika hoja hii iliyoko mezani ya hotuba ya bajeti ya Wizara ya Maliasili na Utalii. Ninapenda kutanguliza shukurani zangu za dhati kwa kazi nzuri inayofanywa na Serikali hii ya Awamu ya Tano na hususan katika mambo mazuri pia yanayofanywa na hii Wizara ya Maliasili na Utalii.

Mheshimiwa Spika, kuna mambo mengi mazuri yanayofanywa na pale mambo mazuri yanapofanywa hatuna budi kutambua na kuunga mkono na kupongeza.

Pia kuna madudu sehemu kadhaa, na hayo pia hayana budi kutolewa maelekezo ndani ya Bunge hili, sisi kutoa ushauri na tutegemee kwamba kuna marekebisho na mabadiliko yatakayofanywa.

Mheshimiwa Spika, awali ya yote niruhusu pia nitoe shukurani kwa niaba ya watu wa Longido kwa Wizara ya Maliasili na Utalii kwa sababu kwa miaka mingi tumekuwa na changamoto ya kutokuwa na gari la kusimamia uhifadhi wa wanyapori na maliasili katika Wilaya yetu. Idara yetu ya Maliasili ya Halmashauri ya Wilaya ya Longido ilikuwa na kilio cha muda mrefu cha kupewa gari la kusaidia doria. Hivi majuzi hata wiki mbili hazijaisha, ndipo gari hilo limepatikana na kwa niaba ya wananchi wa Longido naomba nifikishe shukrani zangu hapa kwa Wizara na kwa Serikali yetu sikivu.

Mheshimiwa Spika, nimepitia hotuba ya Waziri na pia nasimama kuunga mkono maoni yaliyopo katika taarifa ya Kamati kwa sababu nami ni mmojawapo wa wajumbe walioandaa, na maoni yetu tuliyoyatoa ninayasimamia, ninayaunga mkono mia kwa mia na ninaomba yafanyiwe utekelezaji. Bila kusahau lile suala la vigingi vilivyowekwa na TANAPA katika maeneo mbalimbali ya hifadhi za TANAPA ndani ya nchi yetu na yale yaliyogusa maeneo ambayo jamii imekuwa ikiishi kwa miaka mingi bila kuwashirikisha na bila kuwaandaa na kuwafanya watoe ridhaa. Hilo zoezi la kusitisha naomba litekelezwe.

Mheshimiwa Spika, pia nimeona katika hotuba ya Waziri kwamba anafanya overhaul ya vitu mbalimbali, sheria, kanuni na kuna rasimu zimeshaandaliwa. Kwa mfano katika mapitio ya Sera za Taifa kuna rasimu ya Sera ya Misitu na Utalii, anasema imeshaandaliwa.

Mheshimiwa Spika, ningeomba atakapokuja kujumuisha hotuba yake atuambie ni lini itaonekana kwa sababu kuna mapitio mengi ambayo anayafanya na bila sisi kuona na kuridhia inaweza ikawa bado yale mambo ambayo tungependa yabadilishwe yakawa hayatafanyiwa kazi. Kwa mfano, amesema pia kwamba kuna mapitio ya Sheria ya Misitu, kuna utunzi wa Sheria mpya ya Mali Kale, kuna sheria mpya ya uhifadhi wa wanyamapori zinazosimamiwa na TANAPA, Ngorongoro na taasisi mpya ya TAWA, kuna kanuni mpya za usimamizi wa shoroba na maeneo ya wazi yale ambayo wanyamapori wanatawanyikia ambayo kwa asili yake ni maeneo wanamoishi watu.

Mheshimiwa Spika, kwa sababu ya uhaba wa muda naomba basi nijikite zaidi katika maeneo matatu katika mchango wangu. Eneo la kwanza niongelee hili suala la WMA’s, eneo la pili nigusie mambo yanayoendelea ya uhifadhi kupitia TANAPA na nipitie pia maeneo yanayosimamiwa na NCAA maana yake ni Ngorongoro Conservation Area Authority, pamoja na taasisi yetu hii ya TAWA.

Mheshimiwa Spika, kuhusu hili la WMA’s, WMA’s ni sera nzuri ya Serikali iliyokuja kubaini kwamba uhifadhi wa wanyamapori nje ya maeneo yaliyohifadhiwa rasmi ni kitu cha muhimu na kisichoweza kuepukwa kwa sababu hatujaweka fence katika hifadhi zetu. Wanyama wanatoka, wanaingia katika maeneo ya jamii na wanapoingia humo maisha yao yanaweza yakawa hatarini, lakini pia wanaleta hatari katika maisha ya watu.

Mheshimiwa Spika, Sera ililenga kuwafanya wananchi wawajibike, kuwatunza hao wanyama na kuwafaidi pia hao wanyama na ndiyo maana WMA’s zilianzishwa. Kwa wale ambao WMA’s zinawaletea kero na hazijawa baraka mimi nawapa pole kwa sababu inategemea mchakato wao waliufanyaje kwa sababu ni mpango shirikishi wa jamii kutunga, kutenga, kupitisha na kuweka utaratibu wa kusimamia rasilimali ya maliasili iliyoko katika maeneo ya jamii.

Mheshimiwa Spika, sisi kule Longido tuna WMA moja ya mfano, WMA ya Enduimet na WMA hii ilitungwa na jamii kwa kushirikiana na Wizara na wadau wa maendeleo ya uhifadhi (African Wildlife Foundation) mimi nilipokuwa Mkurugenzi kule na tuliweka kwamba ni matumizi jumuishi
ambayo yanaruhusu ufugaji na uhifadhi wa wanyamapori ndani ya eneo lile bila vikwazo kwa utaratibu wa mipango ya kanda ambayo imeshawekwa, inafanya kazi na haijafeli hata siku moja.

Mheshimiwa Spika, Ngorongoro iko hivyo hivyo, ule uhifadhi jumuishi ambao unawaruhusu wananchi na wanyama wabaki ndani ya lile eneo la hifadhi halijashindwa, limebaki na limekuwa sahihi na limekuwa salama kabisa kitu ambacho kinakera leo na labda hatujui kama dhana ni nini nafahamu kwamba kuna sensa ambayo imefanyika ya kuhesabu idadi ya watu halali na mifugo iliyoko ndani ya Ngorongoro na inawezekana pia hiyo ikawa ni chanzo cha kutafuta namna ya kuwasogeza watu ndani ya eneo lile.

Mheshimiwa Spika, ninaomba niishauri Serikali kwamba ile dhana ya uhifadhi jumuishi kwa sababu wananchi walitolewa Serengeti wakaambiwa kwamba Ngorongoro wataishi pamoja na wanyamapiri na jamii yetu ya Wamasai kwa asili yao ni wahifadhi wakuu haijashindwa, kinachotakiwa ni mikakati thabiti ya jinsi ya kuendeleza uhifadhi shirikishi bila kuwabughudhi wananchi katika maeneo ambayo wanaishi kihalali na wanaishi sambamba na maliasili ya wanyamapori iliyoko kule. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hali kadhalika nikitumia mfano wa WMA ya Makame ambayo pia ilianzishwa mimi nilipokuwa Mkurugenzi wa taasisi ya African Wildlife Foundation ilianzishwa na ikachukua yale maeneo ya muhimu ya wanyamapori ambayo wamekuweko tangu enzi za kale wananchi wale wakiishi katika vile vijiji. Nikisikia leo kwamba kijiji cha Lekuishoibor wako hatarini kupoteza vitongoji vyao viwili, kitongoji cha Lombenek na Enjulah kwa sababu Mkungunero Game Reserve inapanuliwa ije imege yale maeneo ninasikitishwa sana.

Mheshimiwa Spika, ninasikitishwa na kufanya nione kama inawezekana Watanzania tunapotea katika kuhifadhi maeneo yetu kwa kuanza kuhifadhi mpaka maeneo ambayo yalishahifadhiwa tayari na jamii kwa kufikiri kwa kuondoa jamii ndiyo hifadi itafanikiwa. Tunaweza tukashindwa vibaya kwa sababu ya kuwafukuza wananchi katika maeneo waliyohifadhi kwa sababu wao wenyewe ni wahifadhi tayari na tunapowafukuza watapoteza urafiki na wale wanyama, na inawezekana wakawa maadui wa hifadhi badala ya kuwa marafiki wa hifadhi.

Mheshimiwa Spika, nchi yetu haina haja ya kufukuza fukuza watu wanaoishi karibu na maeneo yaliyohifadhiwa, ina haja kubwa ya kutoa elimu, kuwashirikisha, kuwapa manufaa ya uhifadhi ili waweze kuwa wahifadhi sambamba na wale wa taasisi zinazohusika, hatuna uhaba wa maeneo. Naomba ninukuu kwamba kulingana na taarifa zilizopo za Wizara ya Maliasili na Utalii, Tanzania inasemekana imehifadhi asilimia 30 ya ardhi yake. Hata hivyo ukienda katika uhakiki wa kina zaidi, ni zaidi, almost asilimia 40.

Mheshimiwa Spika, kwa mfano, TANAPA wana hifadhi 40 zinazochukua asilimia nne za ardhi ya Tanzania. Ardhi mseto kama ile ya NCAA inachukua asilimia moja. Mapori ya akiba ambayo ziko 28 zinachukua asilimia 13, akiba ya misitu ambayo iko 570 inachukua asilimia 12, mapori tengefu ambayo yapo 44 yanachukua asilimia nane na hifadhi za bahari ambazo ziko nane zinachukua asilimia mbili.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, tuna iddadi ya maeneo yaliyohifadhiwa 657 ambayo ni sawa na asilimia 40 ya eneo lote la ardhi ya nchi ya Tanzania. Sasa kama tuna hifadhi zote hizi ambazo nchi nyingi za Afrika hazina, kuna haja gani ya kujenga uadui na wananchi wanaoishi karibu na maeneo yaliyohifadhiwa kwa kuwafukuza fukuza na kuwabughudhi? Hakuna haja! (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini pia kuna suala lingine ambalo naomba nishauri Serikali. Kuna hili suala la jinsi tunavyoweka enforcement ya kuzuia mifugo isiingie katika maeneo yaliyohifadhiwa. Ni kweli yanahitaji kuhifadhiwa na mifugo inaweza ikaharibu ile ardhi lakini hiyo modality ya kuwapiga fine na kuwakamatia ng’ombe ina kasoro kubwa sana na itazidisha uaduzi miongoni mwa jamii ambayo siku zote wameishi kwa urafiki na wanyapori. Ninaomba na ninaishauri Serikali, wale ng’ombe wote ambao walishashikwa, kesi zikaendeshwa na zikamalizika, ng’ombe waachiwe mara moja. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pili ninaomba Serikali ifikirie kuondoa hili suala la kupiga watu fine ya pesa kwa sababu kwanza imeleta mazingira mabaya sana ya ufisadi. Wale watekelezaji wa hizi sheria kule chini wengine wamekuwa mamilionea kwa sababu ya hili zoezi. Ninaomba ule utaratibu sasa utumike kwamba hawaruhusiwi kupokea pesa, hawaruhusiwi kutoza faini, ikiwezekana ng’ombe wanapokamatwa kwa sababu wameingia pale, utaratibu tu ufanyike wa kuwa-identify kwamba ni wa nani na wakaandikishwe na mwenye ng’ombe awajibishwe kulingana na sheria zilizopo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, naomba kuunga mkono hoja na ninaomba baadaye nipate maelezo kwamba ni kwanini WMA ya Lake Natron haijasajiliwa mpaka leo na wakati mchakato wote ulishamalizika, niko tayari kushika shilingi kama Waziri hataniambia kwa nini WMA ya Lake Natron haijapatikana.