Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadilio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Maliasili na Utalii

Hon. Amina Saleh Athuman Mollel

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadilio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Maliasili na Utalii

MHE. AMINA S. MOLLEL: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi nichangie. Sekta ya utalii ni muhimu sana katika nchi yetu na sekta hii ni miongoni mwa sekta mojawapo ambayo inachangia kiasi kikubwa katika pato la Taifa. Mwenyezi Mungu ametujalia nchi yetu ya Tanzania kuwa na hifadhi pamoja na vivutio vingi ambavyo endapo vivutio hivyo vitatatuliwa changamoto ndogo ndogo zilizopo, Tanzania tutafika mbali katika sekta hii ya utalii.

Mheshimiwa Spika, nianze kwanza kabisa kwa kuipongeza Serikali, natambua jitihada wanazofanya na ninakupongeza sana Mheshimiwa Waziri tangu umeingia katika Wizara hii na tunamatarajio makubwa kwamba kutakuwa na mabadiliko katika sekta hii ya utalii.

Mheshimiwa Spika, mimi natoka Mkoa wa Arusha na kwa bahati nzuri katika Mkoa wetu wa Arusha ni Mkoa namba moja ambao tunapozungumzia hifadhi, Kanda ya Kaskazini ndio inayoongoza.Tunafahamu kwamba Tanzania tuna hifadhi 16. Katika hifadhi hizi hifadhi namba moja inayoongoza kwa mapato makubwa ni KINAPA ambayo ipo chini ya Mlima Kilimanjaro na hifadhi nyingine zote za Kanda ya Kaskazini.

Mheshimiwa Spika, pamoja na hifadhi hizi kufanya vizuri bado hizo hifadhi nyingine 11 hazifanyi vizuri kiasi kwamba haziweze kuongeza Pato la Taifa. Hifadhi hizi hazifanyi vizuri kwa sababu ya miundombinu. Kwa mfano Ruaha National Park. Ruaha National Park mbali ya ukubwa wa eneo hili la Ruaha ambalo tukingalia kwa Afrika, Kruger National Park ya Afrika ya kusini inaoongoza kwa ukubwa na Ruaha inafutia kwa sababu ya eneo kubwa. Hata hivyo hii Ruaha bado haijafikia hifadhi zilizopo kaskazini ambazo kwa kiasi kikubwa zinachangia pato la Taifa hili.

Mheshimiwa Spika, katika ziara yake Mheshimiwa Rais hivi karibuni akiwa Mkoani Iringa amesisitiza umuhimu wa kuboresha uwanja wa ndege wa Nduli ili kuhakikisha kwamba watalii wanafika katika mkoa huu wa Iringa ili waweze kufika Ruaha. Pia si tu kwamba uwanja huu wa ndege wa Nduli, tuone pia ujenzi wa barabara ya kwenda Ruaha National Park, barabara hii pia ijengwe ili watalii waweze kufika kwa wingi katika Hifadhi hii ya Ruaha.

Mheshimiwa Spika, pamoja na jitihada hizo ambazo, Wizara inapaswa kuhakikisha kwamba haya yanafanyiwa kazi, lakini bado hatujatangaza ipasavyo hifadhi zetu, vivutio vyetu, utalii wetu na kwa mfano ukienda Kigoma kuna Gombe na Mahale ambapo hapa Tanzania wanapatikana sokwe (chimpanzee), lakini miundombinu bado inakuwa ni tatizo. Kwa hiyo, Wizara tuone ni kwa kiasi gani tunaharakisha uboreshaji ili watalii wengi waweze kufika mpaka huko.

Mheshimiwa Spika, ukienda Katavi ambako nako pia kuna hifadhi na bahati nzuri sasa hivi asilimia kubwa barabara imefika, lakini je, huku Gombe na Mahale ambako hawa chimpanzee walioko kule ni kivutio tosha kabisa cha kuweza kutangaza utalii na watalii wengi wakafika huko.

Mheshimiwa Spika, si hilo tu, pia kuhakikisha kwamba Wizara inatenga fedha na kuhakikisha kwamba Bodi ya Utalii Tanzania ambayo ndiyo yenye jukumu la kutangaza utalii wetu, fedha wanazopewa ni kidogo, tunawawezeshaje kwa sababu unapotaka kitu kizuri lazima wewe mwenyewe ufanye jitihada, toa pesa upate pesa.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo tukiwawezesha Bodi ya Utalii kwa kuwapa fedha wakaweza kutumia nafasi ya kutangaza, ku-brand utalii wetu nina imani kabisa kwamba, Tanzania tutapanda juu na hifadhi hizi zitaweza kuingizia pato kubwa la Taifa.

Mheshimiwa Spika, ukienda katika uwanja wetu wa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, hebu nenda pale, kwa mfano unapoingia katika barabara hii kubwa ya Mwalimu Nyerere, barabara hii mgeni anapoingia ni vivutio gani, matangazo yamewekwa ili kumuwezesha, mbali ya kile ambacho yeye ametoka huko anataka kwenda kukitembelea, lakini je, kuna kitu gani kingine cha ziada ambacho kitamfanya yeye aweze kutoka na kwenda kutembelea? Tuone umuhimu wa ku-brand hifadhi zetu, tuone umuhimu wa ku-brand utalii wetu pamoja na vivutio mbalimbali.

Mheshimiwa Spuka, tunazo mali kale nyingi, kwa mfano tu hapa katika Mkoa huu wa Dodoma ukienda hapo Kondoa kuna utalii upo, lakini haujatangazwa ipasavyo kuhakikisha kwamba watalii wanafika. Hivi sasa Dodoma ni Jiji, sasa kama Dodoma ni Jiji tunai-brand vipi Dodoma ili kuhakikisha kwamba vivutio vingi vinakuwepo?

Mheshimiwa Spika, katika matukio mengi nimeshuhudia, kwa mfano tu shughuli mbalimbali, ngoma zinazochezwa na wagogo, hizi ngoma zikitumika ipasavyo ni utalii tosha ambao utawawezesha watalii mbali ya kuona vivutio vingine hata hizi ngoma tu na kwa sasa kwa sababu Dodoma ni Jiji, tuone umuhimu wa kuwekeza katika mila, desturi na tamaduni zetu ili watalii wanapokuja wawe na vitu vingine vya ziada. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika hoteli zetu, kwa bahati nzuri sijatembea sana lakini nimefika nchi ya Nepal. Katika nchi ya Nepal unapokwenda katika sehemu yoyote ile na hasa wakati wa jioni katika hoteli zote wa kitalii kuna utaratibu wa ngoma, mila na tamaduni zao, ambapo wanashuhudia pale, na ni kivutio. Kwanza inawawezesha wale wananchi wanapata kipato, lakini pia Serikali inapata kipato. Kwa hiyo wakazi wanaoishi maeneo ya karibu na pale wanafaidika kwa kiasi kikubwa.

Mheshimiwa Spika, kule kwetu kwa mfano jamii ya Wamasai, Mmasai tu yeye mwenyewe ni kivutio, lakini je, tunawatumiaje hawa ndugu zetu Wamasai kuhakikisha kwamba ule utamaduni, mila na desturi zao zinawafaidisha hawa Wamasai lakini pia inakuwa ni njia mojawapo ya kuiongezea Serikali pato la Taifa?

Mheshimiwa Spika, nizungumzie pia katika mapori tengefu. Tunayo mapori mengi ninaiomba sasa Serikali kwa kupitia Sheria ya mwaka 2009/2010 ambayo inampa dhamana Waziri mwenye dhamana kuhakikisha kwamba anatenga maeneo kwa ajili ya wafugaji na wakulima ili kuepusha hii migogoro ambayo imekuwa ni shida. Ukisikia hawa wote wanaolalamika juu ya mifugo, mimi wakati na kwenda form one mama yangu aliuza ng’ombe Kwa hiyo ninajua thamani ya ng’ombe.

Mheshimiwa Spika, leo hii mnavyowafilisi hawa na hasa kwa watendaji ambao si waaminifu inakuwa ni pigo na tunawaingiza kwenye umaskini hawa wafugaji. Tunahitaji wafugaji, tunahitaji hifadhi zetu kwa sababu tunaelewa umuhimu wa hifadhi zetu, tunaelewa umuhimu wa mifugo, lakini pia hata wakulima.

Mheshimiwa Spika, mimi nina imani kubwa na Waziri, tuone ni kwa jinsi gani hawa wafugaji hawaumii, wanakuwa ni sababu ya wao kuweza kulinda hizo hifadhi na wanyama lakini pia wakulima nao wanafaidika na haya maeneo yaliyopo. Tuone kwamba haya ni maeneo gani ambayo tutayatenga kwa ajili ya wafugaji na kwa ajili ya wakulima. Vile vile tuangalie jinsi ya kuisuluhisha migogoro hii yote kwa amani na utulivu ili kuepuka haya malalamiko ambayo yanawaumiza wananchi, na hasa wafugaji.

Mheshimiwa Spika, niipongeze pia Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro hasa kwa ujenzi wa maktaba mpya ya kisasa kabisa ambayo itasaidia na inasaidia kwa kiasi kikubwa kuhifadhi mali kale.

Mheshimiwa Spika, hivi karibuni…

SPIKA: Makumbusho, sio maktaba.

MHE. AMINA S. MOLLEL: Makumbusho ambayo inasaidia kuhifadhi hizi mali kale. Kwa mfano hivi sasa tayari imegundulika kwamba mtu wa kwanza duniani aliishi Afrika; na kwa bahati nzuri huyo mtu wa kwanza imegundulika aliishi Tanzania…

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)

Mheshimiwa Spika, nikushukuru, naunga mkono hoja ahsante