Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2017 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019; na Mapendekezo ya Serikali Kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

Hon. Dr. Harrison George Mwakyembe

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kyela

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2017 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019; na Mapendekezo ya Serikali Kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA
MICHEZO: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi hii. Nianze kwa kuunga mkono hoja na vile vile kumpongeza Waziri wa Fedha na Naibu wake kwa kazi nzuri na yenye viwango. Katika dakika tano pengine nigusie suala moja tu, muda ukibaki nitaongelea suala la pili na pengine la tatu.

Mheshimiwa Spika, jana lilijitokeza suala la ukabila hapa, ambalo haliwezi likabaki kwenye Hansard bila ya ufafanuzi. Kwa bahati mbaya sana liliibuliwa na Mbunge ambaye namheshimu sana na ambaye mimi mwenyewe najivunia kwa kumwita mdogo wangu Mheshimiwa James Mbatia.

Mheshimiwa Spika, pamoja na Wabunge wenzangu hapa, pamoja na maudhi yote ambayo tunaweza kuyapata, maana sisi wote ni binaadam, tuna upungufu mwingi sana; sisi viongozi tusikubali kwa njia yoyote ile kuwa abiria kwenye basi la ukabila na basi la udini. Tukifanya hivyo, tutafuta kabisa mafanikio makubwa ambayo Taifa hili limepata kupita Taifa lolote lile katika Bara la Afrika hasa katika kujenga umoja wa kitaifa na sisi kujisikia ni Watanzania na si ni wakabila.

Mheshimiwa Spika, ndugu yetu Mheshimiwa Selasini ni Mheshimiwa mmoja Mbunge na ambaye vile vile namheshimiwa sana; jana aliweza kutoa sababu kwa nini imekuwa hivyo, akagusia magazeti mawili, kwamba kuna magazeti mawili hapa, Tanzanite na Jamvi kwamba ndiyo sababu hasa nafikiri kwamba kuna ubaguzi wa Wachaga.

Mheshimiwa Spika, lakini haya magazeti yanaweza kushtakiwa tu na Sheria ya Huduma ya Habari kifungu cha 41, mtu akileta upuuzi upuuzi mpeleke Mahakamani. Sisi kama Wizara ya Habari tutakuwa mashahidi wenu tutafungiaje, kesho tutafungia mtasema tunaminya uhuru wa habari.

Mheshimiwa Spika, Wizara hatuwezi kufungia kitu ambacho hakiko direct katika kuvunja usalama wa nchi hii. Kama umetukanwa wewe nenda Mahakamani, kifungu cha 41 kinakuruhusu, lakini ukileta hapa kwa sababu umesema wewe ukaleta Wachaga wote wanabaguliwa ni maneno ambayo kwa kweli yanaturudisha nyuma sana Watanzania.

Mheshimiwa Spika, naomba niseme neno moja, hivi leo Mchaga ni nani katika Taifa leo la Watanzania? Yupi hapa anaweza akashika jiwe akamtupia, akatupa jiwe kwenye kabila lingine asimguse mkwewe au mjomba wake kule? Hili Taifa limebadilika sana; mimi niko kwenye hali ngumu hapa, mimi natoka Mbeya huko lakini siwezi kutupa jiwe kwa Mchaga, watoto wangu wenyewe ni Wachaga wana damu hiyo na ndiyo Tanzania nzima iko hivi.

Mheshimiwa Spika, mwaka 1961pengine tukumbushane kwa vijana wadogo wadogo hapa; tulipopata Uhuru, ulikuwa ni uhuru wa makabila haya zaidi ya 120 ambayo hawakuwahi kukaa na kukubaliana kwamba sisi ni Taifa. Kwa hiyo kazi kubwa aliyokuwa nayo Baba wa Taifa ni kuunda a Nation State; ataiundaje?

Mheshimiwa Spika, ndiyo maana Baba wa Taifa ilibidi afanye kazi kubwa ambayo viongozi wengine wote Afrika walidharau na ndiyo maana kwao bado ukabila ni mkubwa. Sisi hatuna ukabila hapa, yeyote yule anayepanda basi la ukabila hana safari ndefu huyo, atapotea, ndiyo maana kitu cha kwanza Mwalimu ikabidi tusitishe mamlaka ya Machifu katika Serikali, ilikuwa nzuri tu, ili tuunde national state.

Mheshimiwa Spika, pili lugha ya Kiswahili kuwa ndiyo lugha yetu ya Taifa; lakini tatu education system yetu. Unakumbuka na viongozi wengine hapa, unamaliza darasa la saba wewe unatoka Kyela sekondari utakwenda Bukoba, wa Bukoba atakwenda Nachingwea, wa Nachingwea ataenda Tanga, wa Tanga ataenda Kigoma.

Mheshimiwa Spika, tumejichanganya na tuna tafiti za kisosholojia hapa, watu wote waliopitia mfumo huo, asilimia zaidi ya 85 hawajaoa maeneo yao, wameoa maneo mengine; na ndilo Taifa alilokuwa anataka kuliunda Mwalimu Nyerere.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, naomba sana, nimeanza ndani ya Bunge hili tumeanza kupanda mabasi ya ukabila, mabasi ya udini. Kuna sentensi za udini na za ukabila, tuache kabisa sisi ni viongozi, hawa watoto, bahati mbaya nimepewa dakika tano, lakini ujumbe wangu ulikuwa ni kwamba jana nilishtushwa, nikasema haya yasiongelewe hapa, tusiongee kabisa, tumefika mbali, tumefanikiwa sana kama Watanzania.

Mheshimiwa Spika, nakuhakikishia hili ni Taifa jipya, hapawezi kabisa kuwa na mtu akisema watu fulani tunabaguliwa, haiwezekani utambagua nani? Maana wote ni wale wale. Ahsante sana.