Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Maliasili na Utalii

Hon. Eng. Edwin Amandus Ngonyani

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Namtumbo

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Maliasili na Utalii

MHE. ENG. EDWIN A. NGONYANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Kwanza nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa fursa hii ya kusema mbele ya Bunge lako.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nina mambo manne mahsusi yanayohusu Jimbo la Namtumbo. La kwanza, ni ardhi ya Kijiji cha Likuyu Sekamaganga ambayo imechukuliwa na Chuo cha Wanyamapori cha Likuyu Sekamaganga bila kuwashirikisha wanakijiji wa Likuyu Sekamaganga. Sasa hivi pana ugomvi pale na ugomvi huu unakuzwa na kiongozi wa chuo, ambaye inaonekana ametumia ujanja amepata hati miliki katika eneo ambalo ni la Kijiji cha Likuyu Sekamaganga bila kuwashirikisha wenye ardhi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimwombe Mheshimiwa Waziri aliangalie suala hili na atatue ugomwi ule. Ile ardhi ni kubwa, chuo kinahitaji ardhi lakini ardhi iliyochukuliwa na chuo ni kubwa sana sehemu ambayo hawaitumii wairudishe kwa wanakijiji, wanakijiji wanaihitaji ardhi hiyo. Tuache kugombana, tuache kupelekana mahakamani, tuache nguvu za dola kuwaweka lock-up watu ambao hawana makosa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili ni kuhusu yaliyotokea wakati wa Operesheni Tokomeza. Wananchi wetu wa Wilaya ya Namtumbo kuna baadhi walichukuliwa silaha zao kwa ajili ya kufanyiwa uhakiki. Tunaongelea Operesheni Tokomeza iliyoendeshwa mwaka 2012/2013, leo ni zaidi ya miaka mitano, uhakiki haujakamilika. Wale watu wakidai silaha zao ambazo walizinunua kihalali, wamezisajili kwenye vyombo vya dola kwa mujibu wa sheria na wakaambiwa wazilete wakazipeleka kwa ajili ya kufanyiwa uhakiki sasa ni zaidi ya miaka mitano hawajarudishiwa silaha zao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kila wakiulizia wanasema sijui kiongozi wa ile Operesheni Tokomeza kwa upande ule wa Kusini yuko Mtwara. Ukienda Mtwara wanasema kule kule Songea na Polisi ndiyo wanashughulikia, ukienda Polisi hakuna majibu kamili yanayopatikana. Nimwombe Mheshimiwa Waziri, hii operesheni ilikuwa ni ya kwako utusaidie, wale wananchi warudishiwe silaha zao, wanazihitaji kwa ajili ya kujilinda na wanyama wakali lakini vilevile kujilinda, kwa wale walichukuliwa pistol maana silaha zilizochukuliwa ni magobore, shortgun na pistol. Pistol zilikuwa zinatumiwa na watu waliokuwa na maduka kujilinda wao na mali zao mbalimbali sasa hawana ulinzi huo na wanaibiwa kila wakati. Nimwombe Mheshimiwa Waziri anisaidie silaha hizo zirudi kwa wenyewe ili wawe na utulivu na hasa kujilinda na wanyama ambao wanaharibu mazao yao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja nyingine ni hoja ya mipaka ya WMA (Hifadhi za Jamii). Kule kwetu tuna Hifadhi za Jamii tatu, tuna Hifadhi ya Jamii inaitwa Kimbanda pamoja na Kisungule ambazo ziko katika Tarafa ya Sasawala. Maeneo haya ya WMA yalikusudiwa zaidi kulinda ushoroba. Wananchi waliyatoa maeneo makubwa zaidi kuliko yale yanayohitajika kwa ajili ya shughuli za ushoroba kwa makubaliano kwamba wataendelea kulima lakini hawatajenga. Kwa hiyo, wale wananchi ndani ya maeneo yale wamekuwa wakiendelea kulima miaka hadi miaka na ni wakulima hodari wa mpunga unaitwa mpunga wa Lusewa ambao ni maarufu sana una harufu nzuri sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tokea mwaka 2015 wamezuiwa kulima wakidai kwamba haya maeneo ni ya Hifadhi za Jamii wakati makubaliano ilikuwa ukulima uendelee ila wasijenge makazi. Kwa sababu kilimo na njia za wanyama wale tembo wanaovuka kwenda Nyasa haviingiliani na nyakati ni tofauti. Nyakati ambazo wale tembo wana-cross ni kipindi ambacho wale watu wanakuwa wameshavuna zamani lakini sasa wamezuiwa kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, WMA ni zetu, ni mali ya hifadhi za jamii lakini sasa inaonekana udhibiti mkubwa uko Wizarani na hivi sasa hata viongozi wetu wanakubali kuruhusu ng’ombe wafugiwe mle ndani lakini siyo kilimo cha mpunga ambacho kimekuwa kikifanyika miaka nenda miaka rudi. Wananchi wa Tarafa ya Sasawala na hasa hasa wa maeneo ya Mtanga, Msangesi, Semeni, Msukunya na mengineyo ya Kata ya Lusewa, Kata ya Msisima na Kata ya Magazine hawaelewi nini kinachoendelea. Maisha yao muda wote wamezoea kulima mpunga katika maeneo hayo na wamekuwa wakiyalinda maeneo hayo na wakiwalinda wanyama lakini sasa wanakuwa ni maadui, wanataka kuwageuza sasa wale watu wawe maadui hata kwa wale wanyama kitu ambacho siyo kizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba mtusaidie, hizi WMA zilitolewa kwa muda wa miaka 10 na baada ya miaka 10 tulitakiwa tupitie upya mipaka na muda wa miaka 10 ulishapita zamani. Naomba sana mtusaidie tupitie upya mipaka ile ya WMA ili wale wananchi waweze kutofautisha na waendelee kulima katika maeneo ambayo wamezoea kulima, yale maeneo tembo hawapiti. Maeneo yanayopitiwa na tembo yanajulikana toka enzi hizo za mababu. Wanayajua na wanayaheshimu. Niombe hizo WMA zipitiwe upya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, WMA ya tatu inaitwa Mbarang’andu, hiyo ipo nje ya Nyasa Corridor. Tatizo la eneo hili la WMA la Mbarang’andu ni wananchi kunyanyaswa. Kuna maeneo ambayo wananchi wa Kata ya Mchomoro wamelima mpunga na wamekuwa wakilima mpunga miaka nenda miaka rudi. Miaka ya hivi karibuni imetokea NGO moja kutoka nje ya nchi na uongozi wa Wilaya umeiruhusu kunyunyizia dawa ya kuuwa magugu kwenye mipunga ambayo wananchi wamelima. Nimwombe sana Mheshimiwa Waziri tumeliongea hili na najua ameanza kuchukua hatua naomba azikamilishe hizo hatua alizoanza kuzichukua. Niombe sana viongozi hawa wakuu wa maeneo yetu wazuiwe kuendelea kuwanyanyasa wananchi, wazuiwe kuendelea kuwafanya wananchi waichukie Serikali yao. Serikali hii inayoongozwa na Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli wanaipenda sana lakini chokochoko hii ya kutaka kuwagombanisha wananchi wale na Serikali yao naomba Mheshimiwa Waziri aikomeshe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, maeneo ya WMA ni wananchi na yale maeneo ambayo yanalimwa mpunga mengine yapo nje ya maeneo hayo lakini bado watu wanawafuata huku wanakolima mpunga na kuwamwagia madawa ambayo yanakausha mipunga yao. Mwaka huu tunavyoongea sina uhakika wale watu waliozoea kujipatia kipato chao kupitia mpunga itakuwaje.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.