Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Maliasili na Utalii

Hon. Leah Jeremiah Komanya

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Meatu

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Maliasili na Utalii

MHE. LEAH J. KOMANYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kunipatia nafasi jioni ya leo nami niweze kutoa mchango wangu. Awali ya yote, napenda kuwapongeza na kuwashukuru Mheshimiwa Waziri pamoja na Naibu wake kwa kazi nzuri wanazozifanya, wamekuwa wakinipa ushirikiano ninapowafuata. Moja ya ushirikiano walionipa ni tarehe 16 Mei, katika swali langu waliponijibu kwamba sasa Wizara itaanza kutoa takwimu kwa kila halmashauri ili ziweze kujua ni kiasi gani cha fedha za uwindaji ama upigaji picha wa kitalii kimepatikana katika eneo husika la uhifadhi ili halmashauri ziweze kufuatilia fedha yao ambayo ni asilimia 25. Halmashauri zimekuwa zikipewa asilimia 25 ya uwindaji wa kitalii bila ya kujua msingi wa tozo ya hiyo asilimia 25. Naamini kuanzia tarehe 1 Julai, walivyoahidi tutaanza kuziona takwimu hizo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niendelee kusema bado pale pana changamoto, fedha hizi tumekuwa tukifuatilia Wizarani unaambiwa hazipo kisheria kwa maana hiyo tunapewa kama hisani. Kama ni hisani basi ni muda muafaka sasa sheria hiyo iletwe ili sisi tuweze kuipitisha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto nyingine ni ya huo mgawanyo wa asilimia 25, sababu asilimia 60 inatakiwa iende katika vijiji, asilimia 40 ibaki katika Idara ya Wanyamapori ili iendeleze mambo ya uhifadhi. Changamoto iliyopo zile asilimia 60 hazipelekwi na halmashauri kwa sababu zinaingia katika mfuko wa amana na kufanya matumizi mengine. Nashauri sasa kwa kuwa vijiji vina akaunti, fedha hiyo ipelekwe moja kwa moja katika vijiji ili na wenyewe wawe na ule mwamko wa kuhifadhi maliasili na kupambana na ujangili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naamini wananchi walioko kandokando ya hifadhi wanafanya kazi hiyo kwa sababu nikiangalia katika Halmashauri ya Wilaya ya Meatu ambapo mchango wangu wa leo utajikita huko katika hifadhi ya wanyamapori, kumekuwa na uvamizi mkubwa wa wanyamapori wakubwa na wakali ambao wanavamia makazi ya wananchi na kuleta taharuki katika maisha ya wananchi na wakati mwingine kusababisha vifo. Kumekuwa pia na uharibifu wa mali, mashamba na mazao ya wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi wa Halmashauri ya Wilaya ya Meatu wamekuwa na juhudi mbalimbali za kukabialiana na wanyama hao. Makundi makubwa ya tembo yamekuwa yakiingia hasa nyakati za usiku, tembo wanne mpaka sitini, hali hii inakuwa ni ngumu mpaka wanapeana zamu za usiku kwenda kulinda. Wametumia mbinu mbalimbali ikiwemo kutumia mavuvuzela. Waheshimiwa Wabunge tumenunua mavuvuzela, mwanzo yalikuwa yanafanya kazi lakini baadaye hayafanyi kazi ikawa kama vile tembo wale tunawapigia muziki. (Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mwaka 2016/2017, heka 135 ziliharibiwa katika Halmashauri ya Wilaya ya Meatu, katika miezi hii mitano ya mwaka huu hekari 200 zimefanyiwa uharibifu. Kwa hiyo, wananchi wameingia katika tatizo la njaa. Naheshimu maamuzi ya Mheshimiwa Rais kwamba hakutakuwepo na chakula cha bure kwamba wananchi wafanye kazi. Hilo nalikubali na naliunga mkono na naona wanachi wamelima, mazao ni mengi lakini changamoto iliyopo wananchi wa vijiji vile mazao yao yaliliwa na tembo. Kwa hiyo, Serikali inapofanya uamuzi sasa iangalie maeneo mengine mahsusi ambapo wananchi hawakujitakia wenyewe isipokuwa ni tembo ndiyo walisababisha. Viongozi wamekuwa waoga kufanya maamuzi ili kuyaleta juu kuelezea hali halisi ilivyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nasema mbele yako leo hali si nzuri katika maeneo yale. Naomba vijiji vile viangaliwe kwa upande mwingine siyo kuogopa tamko la Mheshimiwa Rais. Viongozi wengine wanaogopa matamko ya Rais na kuyatasfiri visivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, uwezo wa halmashauri wa kukabiliana na changamoto dhidi ya wanyamapori waharibifu ni kubwa sana. Kwanza eneo la hifadhi ni kubwa. Ukiangalia Halmashauri ya Wilaya ina kilomita za mraba 8,835, eneo la hifadhi ni karibia nusu kwa sababu lina kilomita za mraba 3,900 sawa na asilimia 44.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo hili kubwa la hifadhi kuna mwingiliano mkubwa wa matumizi ya rasilimali zilizopo kati ya wanyamapori na wananchi. Rasilimali hizo ikiwa ni matumizi ya maji pamoja na malisho. Nakubaliana na hotuba ya Kamati kwamba katika vijiji vinavyopakana na hifadhi pachimbwe visima au mabwawa ili wananchi hao wapate maji, wasiende kuchangia na wanyamapori katika mito iliyopo kandokando. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto iliyopo nyingine ni malisho. Pamoja na agizo lililopo nashauri kwa upande wa pili basi katika buffer zone tuangalie hata mita 500 tuwape hawa wananchi. Naamini ndiyo watakuwa walinzi wa ujangili na wako tayari kuweka mipaka. Tukiangalia Tanzanite ukuta umejengwa ili kuhifadhi Tanzanite yetu, hata sisi tuko tayari kuhifadhi wanyamapori, tunaweza tukaweka hata mipaka ambayo haina gharama kubwa ili mradi wananchi waweze kujipatia malisho kwa ajili ya mifugo yao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika eneo hili la uhifadhi la kilomita hizo za mraba, asilimia 70 linajulikana kwamba ni eneo la wanyama wanaohama yaani migratory belt. Asilimia 70 ya hawa wanyamapori wanakaa nje ya maeneo yale maalumu ya hifadhi. Hii ni changamoto kubwa sana kwa halmashauri yetu, ukiangalia asilimia 70 ya hao wanyama tena wanakaa nje ya yale maeneo yao, maana yake wanakaa vijijini. Changamoto iliyopo ni uhaba wa watumishi, tuna watumishi watatu tu, naomba idara iongezewe watumishi. Pia tuna changamoto za vitendea kazi kama silaha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi hii kumshukuru Mwiba Holding Company kwa kununua silaha tatu, Mzinga Corporation. Naomba sasa mchakato wa kumilikishwa zile silaha uharakishwe kwa kuanzia na kwa OCD wa Wilaya ya Meatu maana toka apelekewe mwezi wa pili hajaanzisha mchakato huo na mchakato ni mrefu. Kupitia Bunge hili naomba mchakato huo upelekwe haraka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, zoezi la Operesheni Tokomeza silaha saba zilichukuliwa mpaka leo hazijarudishwa. Naomba Wizara warudishieni sasa hao watumishi hizo silaha. Mmeyaona hayo makundi makubwa ya tembo pamoja na wanyamapori wakali wakiwemo na viboko ili wale watumishi waweze kupambanana nao. Ainza za silaha zile nina orodha pamoja na namba zake. Naomba sasa zile silaha zilizochukuliwa wakati wa zoezi la Tokomeza ziweze kurejeshwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nashauri…

Mheshimiwa Mwenyekiti, nauga mkono hoja.