Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi kwa mwaka wa fedha 2016/2017.

Hon. Oran Manase Njeza

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbeya Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi kwa mwaka wa fedha 2016/2017.

MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kumpongeza Waziri na Naibu Waziri kwa hotuba nzuri na kazi kubwa wanayoifanya. Sekta ya Kilimo inatoa mchango mkubwa kwa sekta nyingine hasa viwanda, fedha, usafirishaji na biashara.
Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na umuhimu wa kilimo, hakijapewa kipaumbele inavyostahili. Uzalishaji kwa eneo ni mdogo na tija ni ndogo; miundombinu ya barabara vijijini ni mibovu, mfumo wa masoko ni duni na uwezo wa kupata fedha toka vyombo vya fedha ni mdogo; vile vile Sekta ya Kilimo hupewa chini sana asilimia 0.9 badala ya asilimia 10 kama ilivyo kwenye Azimio la Maputo na changamoto za upatikanaji wa pembejeo bora.
Mheshimiwa Spika, uzalishaji wa pareto unaporomoka sana na hata kwa huo uzalishaji mdogo, bei kwa wakulima ni ndogo sana ukilinganisha na msimu wa mwaka 2013/2014. Sababu kubwa za kuporomoka uzalishaji na bei:-
(1) Mnunuzi ambaye ndiye mwekezaji ni mmoja na wanunuzi wadogo wazalendo wamefungiwa kununua kwa kuwekewa masharti magumu sana;
2) Ukosefu wa wataalam kusimamia zao hili hupelekea ubora wa pareto yetu koporomoka sana;
(3) Kutokana na monopoly ya mnunuzi, bei imeporomoka kutoka sh. 2,400/= kwa kilo mwaka 2014 mpaka sh. 1,400/= kwa kilo mwaka 2015;
(4) Mwaka 2010 Tanzania na nchi nyingine za Afrika Mashariki zilikuwa zinazalisha asilimia zaidi ya 70 ya mahitaji ya dunia. Leo hii Kisiwa kidogo cha Tasmania (Australia) ndiyo kinaongoza kwa kuzalisha asilimia zaidi ya 65 wakati bei ya pareto kwa mkulima Tanzania ni sh. 1,500/= kwa kilo. Wakulima wa nchi nyingine ni zaidi ya sh. 4,000/= kwa kilo. Naomba Waziri uagize Bodi ya Pareto iwakutanishe wanunuzi wadogo, wawakilishi wa wakulima na bodi ili kupanga utaratibu mzuri wa ununuzi wa pareto; na
(5) Pia Serikali iweke mazingira ya kujenga Kiwanda cha Pareto Mbeya.
Mheshimiwa Naibu Spika, changamoto kubwa ya zao la kahawa ni uzalishaji duni na usimamizi mbovu wa Soko la Kahawa. Ni lini Commodity Exchange Market itaanza kufanya kazi?
Mheshimiwa Naibu Spika, bei ya kahawa (Arabica) kwa wenzetu Kenya wenye Nairobi Coffee Exchange ni zaidi ya sh. 8,000/= kwa kilo wakati kwenye soko la TCB Moshi ni chini ya sh. 4,000/= kwa kilo. Kwa nini mkulima wa Tanzania anaibiwa kiasi hicho? Wanunuzi ni wale wale!
Mheshimiwa Naibu Spika, Benki ya TADB ina umuhimu mkubwa sana kwenye Sekta hii muhimu. Mtaji wa shilingi milioni 60 ni mdogo sana. Serikali kama ilivyoahidi, iongeze mtaji wa Benki hii ili iweze kukidhi mahitaji makubwa ya wakulima na wajasiriamali wa kilimo.
Mheshimiwa Naibu Spika, napongeza sana mpango wa Serikali wa shilingi milioni 50 kwa kijiji. Kiasi hiki cha pesa zikisimamiwa vizuri zinaweza kubadilisha kwa kiasi kikubwa tija na uzalishaji wa kilimo. Napendekeza hizi shilingi milioni 50 zilizotengwa kwa kila kijiji zisimamiwe kwa ukaribu na TADB.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu mafunzo ya wakulima na Maafisa Ugani:-
Serikali iongeze idadi ya Maafisa Ugani vijijini;
Vijana wapewe elimu ya ujasiriamali wa kilimo; na
Vyuo vyetu na hasa Vyuo vya Utafiti vitumike kupima udongo ili tuweze kutumia pembejeo sahihi.