Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Mifugo na Uvuvi

Hon. Abdallah Haji Ali

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Kiwani

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Mifugo na Uvuvi

MHE. ABDALLAH HAJI ALI: Mheshimiwa Spika, awali ya yote napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu muweza wa mambo yote. Aidha, napenda kumpongeza Spika kwa uongozi wake mahiri Bungeni.

Mheshimiwa Spika, nichangie kuhusu uvuvi wa Bahari Kuu Tanzania. Bahari ni fursa kubwa kwa waliojaliwa kuwa nayo kama sisi hapa Tanzania. Mwenyezi Mungu katujalia mwambao mkubwa wa bahari kuu.

Mheshimiwa Spika, eneo hili kama Serikali ingeweza kulitumia vyema, nchi yetu ingeweza kujiongeza na kutoka katika hatua tulionayo sasa.

Mheshimiwa Spika, bahari ni shamba lililosheheni mazao mengi, yaani samaki na vitu vingine kama gesi na mafuta. Bahari ni shamba ambalo halihitaji madawa, mbolea na wala halihitaji pembejeo ya aina yoyote. Lipo tayari kwa ajili ya kuvunwa tu.

Mheshimiwa Spika, naishauri Serikali iondokane na usingizi mzito ilionao ili iweze kuitumia rasilimali ya bahari ambayo imesheheni neema kubwa na ya maana kabisa.

Mheshimiwa Spika, nchi zote zenye bahari kama yetu wananufaika na neema hii kwa kuweka mikakati madhubuti ya kutumia teknolojia ya kisasa na vyombo vya uvuvi vya kisasa.

Mheshimiwa Spika, nchi za wenzetu wenye mikakati thabiti ya uvuvi katika bahari kuu wanakuja kuvua katika maeneo yetu na wanatuvulia samaki wetu kwa wingi na kupeleka neema hii katika nchi zao. Siyo vyema kwamba neema ipo kwetu na kuwaachia wengine kuwavua samaki wetu na kuwahamishia kwao na baadae kuwasafirisha kuja nchini kwetu tukawa ni wateja wao kwa rasilimali itokayo ndani ya bahari yetu.

Mheshimiwa Spika, imefika wakati sasa kwa Serikali kuifanya bahari kuwa ni chanzo kingine cha mapato ya nchi kwa kuwavua samaki waliomo ili wainufaishe nchi kimapato. Sasa Serikali ije na mpango mkakati wa uwekezaji kama unavyofanywa katika sekta nyingine, kwa mfano, sekta ya madini na utalii.

Mheshimiwa Spika, samaki ni chakula maarufu sana duniani kote. Nchi zote zinahitaji samaki. Ni biashara yenye tija na inayoweza kuipeleka mbele nchi yetu kimaendeleo.

Mheshimiwa Spika, Wabunge wameongelea mambo mengi kuhusu uvuvi kiujumla wake. Pamoja na mambo hayo, ni imani yetu kwamba Serikali imesikia ushauri huu na sasa Serikali itaichukulia sekta ya uvuvi kuwa ni chanzo kingine cha mapato, pia ni sekta inayotoa ajira nyingi kwa wavuvi, wachuuzi na wananchi wengine. Tuitumie bahari ipasavyo ili ituletee maendeleo. Ahsante.