Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Mifugo na Uvuvi

Hon. Dr. Stephen Lemomo Kiruswa Mamasita

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Longido

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Mifugo na Uvuvi

MHE. DKT. STEVEN L. KIRUSWA: Mheshimiwa Spika, kwanza naipongeza Serikali yetu ya Awamu ya Tano kwa kazi nzuri ya kupeleka mbele maendeleo ya nchi yetu. Nampongeza Rais wetu Dkt. John Pombe Magufuli, Makamu wa Rais Mama Samia Suluhu, Waziri Mkuu Mheshimiwa Kassim Majaliwa pamoja na Baraza lote la Mawaziri.

Mheshimiwa Spika, napenda kumpongeza Waziri wa Mifugo na Uvuvi kwa hotuba hii ya bajeti na kazi kubwa anayofanya yeye na Naibu wake kuendeleza sekta ya mifugo na uvuvi.

Mheshimiwa Spika, baada ya pongezi hizi, naomba nichangie hoja ya bajeti ya Wizara ya Mifugo na Uvuvi kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Wizara izingatie umuhimu wa kuongeza bajeti ya kutekeleza vipaumbele vya sekta ya mifugo kama vile upatikanaji wa maji, majosho, dawa, tiba na masoko.

Mheshimiwa Spika, kutokana na bei ya mifugo kuyumba kila wakati kutokana na mabadiliko ya hali ya hewa hususani katika Wilaya za Kaskazini Mashariki kwa nchi yetu ikiwemo Longido, Monduli, Simanjiro na Ngorongoro, naiomba Serikali kupanga bei elekezi ya kuuza mifugo kwenye masoko yetu kama mazao mengine mfano zao la pamba na korosho ambazo hupangiwa bei kwa kilo. Ng’ombe nao wapangiwe bei kwa kilo kwa ng’ombe hai na nyama ili wafugaji wapate tija zaidi.

Mheshimiwa Spika, kuhusu masoko/minada inayoanzishwa mipakani na Halmashauri za Wilaya kama soko la Halmashauri ya Wilaya ya Longido lililopo Eorendeka. Soko hili lilibuniwa na Halmashauri kwa makusudi ya kuinua mapato ya ndani ya Halmashauri na kuwapatia wananchi mnada wa uhakika na kuuza mifugo kwa faida ili kuinua kipato chao. Kwa kuwa Wizara imejitokeza na kuja kunyakua mnada wa Eorendeke na ninatambua kuwa pia Serikali Kuu inahitaji kodi, nashauri Serikali ichukue tu asilimia ndogo ya kodi na kuwaachia Halmashauri ndio wenye jukumu kubwa la kuendelea kuimarisha na kusimamia wafanyabiashara ili mnada/soko la mifugo la ndani liimarike.

Mheshimiwa Spika, kuhusu viwanda vya kuchakata bidhaa za mifugo, napenda kuishauri Serikali iwakopeshe wananchi ili waweze kuanzisha viwanda vidogo vya usindikaji maziwa, nyama na ngozi na pia Serikali ifufue viwanda vilivyokuwepo kwa mfano Kiwanda cha Maziwa kilichotelekezwa na mwekezaji Longido. Kwa kufanya hivyo wananchi watanufaika na mazao ya mifugo.

Mheshimiwa Spika, napenda pia kuishauri Serikali ianzishe kiwanda kikubwa cha ngozi pamoja na mazao yote ya mifugo na kuwa na viwanda vidogo katika mikoa yote ya wafugaji. Ngozi ni bidhaa ya thamani sana kwa mfano Ethiopia ngozi zina bei kubwa ndani na nje ya nchi hiyo.

Mheshimiwa Spika, kuna tatizo kubwa linalowakabili wafugaji la kupoteza mifugo kutokana na kula mifuko ya plastiki. Licha ya mifuko hii ambayo imetapakaa kila mahali katika nchi yetu kuchafua na kuharibu mazingira, mifugo wengi wanaangamia wakati wa kiangazi na kula karatasi hizo za plastiki. Naomba kuishauri Serikali ipige marufuku matumizi ya mifuko ya plastiki katika nchi yetu. Rwanda na Kenya majirani zetu wao wamepiga marufuku na wamefanikiwa, sisi pia tuige mfano wao.

Mheshimiwa Spika, hoja kuhusu mnada wa mifugo wa Halmashauri ya Wilaya ya Longido iliyo Kijiji cha Eor Endeke Longido, mnada huu umejengwa kwa juhudi za Halmashauri bila msaada kutoka Wizarani. Lengo la mnada huu ulio karibu na mpaka wa Kenya na Tanzania katika eneo la Namanga lilijengwa kwa kusudi la Halmashauri kujiongezea mapato ya ndani na wananchi kupata soko la mifugo yao.

Mheshimiwa Spika, leo hii kuna kero kubwa imejitokeza baada ya Wizara kuja kuingilia mnada huo na kupanga kodi kubwa ya ushuru wa Serikali wa shilingi 20,000 kwa ng’ombe na shilingi 5,000 kwa mbuzi na kondoo. Kodi hii si rafiki kwa wananchi na hali hii imewakatisha tamaa na kupelekea kuanza kurudi tena kupitishia mifugo maporini kuvusha Kenya ili kuendeleza biashara zao. Hivyo kupelekea Serikali Kuu na Halmashauri kupoteza mapato.

Mheshimiwa Spika, kutokana na hali hii, naomba kuishauri Wizara na Serikali izingatie kufanya yafuatayo:-

Mheshimiwa Spika, kwanza ipunguze kodi kwa kushauriana na wananchi, itoe huduma za export permit palepale mnadani badala ya kwenda hadi Arusha au Wizarani. Wizara ya Mifugo wakae na Halmashauri waafikiane jinsi ya kuendesha mnada huu ili uweze kuleta tija kwa wananchi, Halmashauri na Serikali Kuu.

Mheshimiwa Spika, mwisho wajasiriamali wa mifugo (wachuuzi) na wananchi wa Longido wanaiomba Serikali yetu sikivu iwatafutie soko la ndani la uhakika kwani wasingetamani kupeleka mifugo kwenye minada na masoko ya nchi jirani kama siyo ni kutokana na kutokuwepo mnada wenye bei nzuri nchini ukilinganisha na nchi ya jirani.

Mheshimiwa Spika, changamoto ya wafugaji waliopoteza ardhi kwa ajili ya uwekezaji na uhifadhi; mfano wa mashamba yaliyoko Kanda ya West Kilimanjaro, wafugaji walikuwepo West Kilimanjaro kabla ya Bara la Afrika kugawanywa na wakoloni mwaka 1884. Wajerumani ndio
wakoloni wa kwanza kuitawala Tanganyika na ndio waliowatoa wafugaji kutoka katika nyanda za juu zenye rutuba, mvua za uhakika, malisho na maji kwenda katika maeneo ya mbugani ambayo ni makavu na yasiyo na maji wanapoishi hadi leo.

Mheshimiwa Spika, baada ya Vita Kuu ya Pili ya Dunia mwaka 1945 Serikali ya Uingereza baada ya kukabidhiwa koloni la Tanganyika na Umoja wa Mataifa wakati huo ukiitwa The League of Nations, waliwazawadia wanajeshi waliopigana Vita ya Pili ya Dunia yale maeneo. Wafugaji wakaendelea kubaki bila ardhi yenye maji na malisho ya mifugo yao nyakati za kiangazi.

Mheshimiwa Spika, mwaka 1968 baada ya Serikali kutangaza Azimio la Arusha na kutaifisha yale mashamba, Rais wa Tanzania Hayati Mwalimu Julius Kambarage Nyerere (Mungu ampe heri ya milele) alipotembelea Wilaya ya Maasai kama ilivyojulikana wakati huo alisikitika alipobaini kuwa wafugaji hawana ardhi inayofaa kwa malisho na maji ya mfugo yao nyakati za kiangazi. Akaagiza wapewe ekari 5,500 kwa ajili ya malisho ya mifugo yao. Tarehe 13/3/1973 Bunge liliridhia wafugaji kurudishiwa hizo ekari 5,500 na tarehe 16/3/1973 Serikali ilitenga rasmi ekari 5,500 za malisho kupitia GN No. 59.

Mheshimiwa Spika, TANAPA ilipopitisha operation ya kubaini na kuweka alama mipaka ya Hifadhi ya Mlima Kilimanjaro miaka ya karibuni eneo hilo lilijumuishwa katika Hifadhi ya KINAPA (Kilimanjaro National Park).

Mheshimiwa Spika, naomba kuishauri na kuiomba Serikali iwape wafugaji hawa ardhi mbadala katika mashamba pori ya NDC, NARCO na NAFCO yaliyoko katika ukanda huo wa West Kilimanjaro.

Mheshimiwa Spika, aidha kuna mashamba mawili ambayo matumizi yake yamekuwa yasiyo na tija, hususani West Kilimanjaro Ranch yenye jumla ya ekari 95,000 na ng’ombe wa NARCO wasiofika 200 na Endarakwai Ranch yenye ekari 11,000 ambayo mwekezaji mmoja wa kiingereza, Peter Jones, analitumia kufugia wanyamapori na mifugo hawaruhusiwi kuingia.

Mheshimiwa Spika, mwaka 1982 Rais wa Awamu ya Kwanza, Hayati Mwalimu Nyerere alimwagiza aliyekuwa Waziri Mkuu wakati huo, Hayati Edward Moringe Sokoine (apumzike kwa amani) kuanzisha Ranchi ya Jamii ya Larkarian. Ardhi husika iliainishwa, Mbunge na Waziri Mkuu wa wakati huo, Hayati Sokoine aliwahamasisha wafugaji wakachanga mitamba 1,500. Lakini baada ya kifo chake, mradi wa Ranchi ya Jamii nao ukafa. Baada ya Hayati Sokoine na Mradi wa Ranchi ya Jamii kufa, wawekezaji wakapewa ardhi hiyo ambayo inajumuisha mashamba nane yafuatayo; Ndarakwai Ranch, Roselyn Farm, Tilonga Farm, Simba Farm, Mountain Side Farm; Engushai Farm, Mawenzi Farm na Leghumushira Farm.

Mheshimiwa Spika, kwa sasa baadhi ya mashamba haya yamekuwa mashamba pori. Kwa hiyo, naomba kuishauri na kuiomba Serikali iwarejeshee wafugaji wa Kanda ya West Kilimanjaro ardhi hiyo au wepewe mbadala kwa ajili ya shughuli zao za ufugaji na hasa kufufua Mradi wa Ranchi ya Jamii.

Mheshimiwa Spika, Ndarakwai Ranch yenye ukubwa wa ekari 11,000 ilikuwa ni mojawapo ya maeneo muhimu ya jamii ya Kimasai ya kulisha mifugo yao hadi wakoloni walipojimilikisha. Ni baada ya Azimio la Arusha mwaka 1967 ndio Serikali ilitaifisha shamba hili na kuikabidhi TBL.

Mheshimiwa Spika, mwaka 1992 TBL ilibinafsisha shamba la Endarakwai kwa Kampuni ya Tanganyika Film and Safari Outfitters inayomilikiwa na Bwana Peter Jones, raia wa Uingereza. Mwekezaji huyu aligeuza shamba hili kuwa pori la kufugia wanyamapori na amekuwa na ugomvi mkubwa na wafugaji wanapojaribu kwenda kulisha katika eneo hilo.

Mheshimiwa Spika, wafugaji wa West Kilimanjaro wanaiomba Serikali iwarejeshee ardhi hii.

Mheshimiwa Spika, naomba kuhitimisha kwa kutoa kilio cha wafugaji, wafugaji wana matatizo mengi lakini kubwa zaidi ni la kunyang’anywa ardhi yao ya asili katika sehemu mbalimbali za nchi yetu ikiwemo eneo hili la West Kilimanjaro nililojadili, Serengeti, Tarangire, Mkungunero na maeneo mengine mengi ndani ya nchi yetu. Maeneo haya yalibadilishwa kuwa ya matumizi mengine yenye maslahi mapana kwa Taifa lakini tatizo ni kuwaacha wenyeji bila ardhi inayofaa ya mbadala kwa malisho na maji ya mifugo yao na watu.

Mheshimiwa Spika, naiomba Wizara ya Mifugo na Uvuvi ichukue hatua za kizalendo na watatue migogoro ya ardhi ya wazawa iliyotwaliwa kwa jina la uwekezaji na kugeuzwa kuwa mashamba pori yasiyo na faida kwa Serikali wala wananchi na badala yake, yamekuwa chanzo cha ufilisi kwa wafugaji maskini ambao kila wanapokanyaga mashamba pori hayo wakitafuta malisho na maji wakati wa kiangazi wanakamatwa, wanapigwa na kutozwa faini kubwa zinazozidi kuwakandamiza kiuchumi na kuwaacha katika umaskini mkubwa zaidi.

Mheshimiwa Spika, naomba kuwasilisha na ninaunga mkono hoja.