Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Mifugo na Uvuvi

Hon. Saed Ahmed Kubenea

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Ubungo

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Mifugo na Uvuvi

MHE. SAED A. KUBENEA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia.

Mheshimiwa Spika, kwanza niseme wazi baada ya mjadala kufungwa jioni, nitatoa taarifa kwa Kiti chako kwamba kwa kutumia Kanuni zetu nitaleta Hoja ya Kuundwa Kamati Teule ya Bunge kuchunguza Operation Sangara yote ilivyofanyika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nchi yetu ina square meter zaidi ya 800 eneo la bahari, kutoka Mtwara mpaka Tanga, kutoka Pemba mpaka Mafia lakini eneo la uvuvi linachangia sehemu ndogo sana ya pato la Taifa letu kwa sababu hatujawekeza kabisa katika uvuvi. Wananchi wa Dar es Salaam sisi tunaishi kwa nyama, kuku na samaki lakini nchi yetu haiangalii kabisa katika eneo zima la nyama, hivi Tanzania inaagiza kuku, nyama na samaki kutoka nje? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Tanzania ambayo tuna bahari ya kutosha, meli za nje zinakamatwa ndani, tunazitaifisha, tunapelekwa mahakamani, tunadaiwa fidia ya mabilioni, lakini sisi tunaagiza samaki kutoka nje, hii ni aibu! Ni aibu miaka 50 baada ya uhuru Tanzania yenye bahari, maziwa na mito inaagiza samaki kutoka nje. Halafu Wabunge wa CCM wanasimama hapa wanasema tutazuia bajeti, hakuna Mbunge wa CCM mwenye uwezo wa kuthubutu kuzuia bajeti, hayupo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kama akiwepo na bajeti hii ikazuiwa, mshahara wangu wa mwezi huu nisilipwe, wapeleke kwenye majimbo ya hao Wabunge. Mheshimiwa Spika, nisilipwe. Hakuna Mbunge wa CCM anaweza kusimama katika maneno yake mpaka mwisho.

Mheshimiwa Spika, hiki kilichoandaliwa na Mheshimiwa Mpina, mimi namfahamu sana Mheshimiwa Mpina. Mwaka 2012 akiwa Mbunge alizuia bajeti hapa, alikataa bajeti ya Serikali, leo Mheshimiwa Mpina anakaa kwenye Wizara, anachukua hela za wafugaji, anachukua hela za uvuvi, halafu harejeshi fedha kwa wananchi. Nashangaa nikimuona Mheshimiwa Mpina wa leo nikimuangalia na Mheshimiwa Mpina wa miaka saba iliyopita, siyo huyu, siyo kabisa. Ni rafiki yangu, ni kaka yangu, tunaheshimiana lakini nikimuangalia yule Mheshimiwa Mpina wa miaka ile siyo huyu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, suala la uvuvi ni tatizo kubwa sana katika nchi yetu. Kuna Sheria ya Hifadhi ya Bahari ya mwaka 1999, zaidi ya miaka 30 leo haijafanyiwa marekebisho. Wavuvi wetu katika maeneo ya pwani na visiwani, ukienda kule Mafia na Rufiji, utakuta eneo limetengwa kwa ajili ya hifadhi ya bahari lakini hifadhi ya bahari inaweka boya mita 100 inazuia wavuvi wasifanye kazi zao za uvuvi.

Mheshimiwa Spika, leo uvuvi katika visiwa kama vya Mafia, Kware na Koma kwa Mheshimiwa Ulega, asilimia 99 ya wananchi wanategemea uvuvi. Pale Kware na Koma kwa Mheshimiwa Ulega wananchi hawalimi, wanategemea bahari lakini hifadhi ya bahari imeenda kuchukua maeneo ya bahari, imezuia wananchi wasivue, imeleta matatizo makubwa.

Mheshimiwa Spika, katika baadhi ya maeneo Jeshi la Wanchi linatumika na hifadhi ya bahari kukimbiza wavuvi na kuzamisha boti za watu na kunyang’anya nyavu za watu, Jeshi la Wananchi. Nchi gani hii mnaongoza? Nchi hii tuliomba uhuru ili wananchi wawe huru, wafanye mambo yao huru kwa mujibu wa sheria. Hata hivyo, baada ya kuwa huru Watanzania wamekuwa watumwa katika nchi yao. Wanazungumza Wabunge wa CCM hapa unaona uchungu, mnaenda kwenye uchaguzi kesho mtasemaje? Mtawaambia nini wananchi au ndiyo mtatumia dola na polisi kushinda? Hoja hizi za Mheshimiwa Bulembo hazijibiki. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jana kuna mtu ameniambia, sijui kama kweli, kwamba Waziri wa Mifugo anatoka Kanda ya Ziwa, hafahamu kabisa mambo ya Pwani. Mheshimiwa Ulega anatoka Mkuranga, lakini anatoka Kimanzichana, hata bwawa kwake hakuna. Mkurugenzi wa Uvuvi anatoka Kanda ya Ziwa. Sasa hiki kilio cha wananchi wa Pwani ambacho kilianza toka enzi za akina Mheshimiwa Mudhihir Mudhihir, Mheshimiwa Bakari Mbonde, Mheshimiwa Ayoub Kimbau…

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)