Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi kwa mwaka wa fedha 2016/2017.

Hon. Ridhiwani Jakaya Kikwete

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Chalinze

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi kwa mwaka wa fedha 2016/2017.

MHE. RIDHIWANI J. KIKWETE: Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kwa kuunga mkono hoja. Pamoja na kuongeza juhudi kubwa ambazo Mheshimiwa Waziri, Naibu wake na Watendaji wa Wizara wamekuwa wanafanya, lakini ni ukweli usio na kificho kuwa changamoto zimeendelea kuandama Wizara hii.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika mchango wangu kwenye Bunge la Kumi, niligusia juu ya mahitaji ya kutatua migogoro ya wakulima na wafugaji ili kuwe na tija ya upatikanaji wa chakula cha kutosha, lakini hadi leo ninapowasilisha andiko hili, bado migogoro imeendelea kushamiri. Mheshimiwa Waziri umeshuhudia athari inayotokana na kutokuwepo kwa Sheria zinazobana, kugeuzwa kwa mashamba kuwa sehemu za machungio. Ni vyema Mheshimiwa Waziri atakapokuja, atueleze juu ya mkakati mzima alionao katika kuhakikisha kabla ya Januari, 2017, migogoro imekwisha kama siyo kupungua kwa asilimia kubwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, bei ya sukari imeendelea kuwa kubwa na speed ya upandaji wake naufananisha na kuongezeka kwa migogoro ya wakulima na wafugaji. Katika Awamu ya Nne, kuna mradi mkubwa wa miwa ulioanzishwa Wilaya ya Bagamoyo. Mradi huu ambao una maslahi makubwa sana na Watanzania hususan ni watu wanaotumia sukari, umepelekea watu kuwa na matumaini ya kufufua upya maisha bora kwa wananchi, lakini pia huenda hili tatizo la sukari likamalizika.
Mheshimiwa Naibu Spika, linaloshangaza, hadi leo fedha za Benki toka ADB na IFAD zilikwishatengwa kwa muda mrefu zikisubiri kauli ya Serikali juu ya mradi huu. Namwomba Waziri au Serikali itakapokuja kufanya majumuisho, itoe kauli juu ya lini kauli hii itatoka na je, hawaoni kuwa kwa kuchelewa kutoa kauli ni kuhujumu Ilani ya Chama cha Mapinduzi ya mwaka 2015?
Mheshimiwa Naibu Spika, hakuna maendeleo pasi kuwa na teknolojia inayoendana na tija kubwa ya kimatokeo. Kilimo cha leo kinategemea matrekta na zana bora za kisasa ili kuleta tija ya kilimo hicho. Nakupongeza wewe Mheshimiwa Waziri na wataalam kwa kuonesha kupitia hotuba utayari wenu wa kuvusha kilimo chetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, ukweli ni kwamba matrekta 2,000 ni machache sana; ili kupata tija ni vyema tukaongeza matrekta ili tija nzuri ya kilimo ipatikane. Kwa asilimia kubwa kilimo kinategemea maji. Viko vipindi mbalimbali katika majira ya mwaka ambapo mvua ziko za kutosha, ila linaloshangaza wengi, ni ujuzi mdogo wa kuhifadhi maji hayo.
Mheshimiwa Naibu Spika, nashauri Wizara itengeneze program za kufundisha watu kufanya uhifadhi kwa ajili ya kilimo cha umwagiliaji na pia kuanzisha utaratibu maalum wa kufundishia Maafisa Ugani ili waweze kuwa wenye msaada mkubwa zaidi.
Katika Jedwali Na. 3, ukurasa wa 29 kitabu cha hotuba ya Mheshimiwa Waziri ameonesha ukuaji mkubwa wa mazao ya mafuta. Linalonishangaza hapa ni kwamba, mazao yote yaliyoainishwa, ni mazao ambayo hayana vyombo vinavyoongoza na hata wakati mwingine kujiuliza hizi takwimu zimetoka wapi? Mheshimiwa Waziri aweke wazi jambo hili.
Mheshimiwa Naibu Spika, mazao hayo yaliyoainishwa yanaweza kuwa siyo sahihi kwa upande wa taarifa. Chalinze na maeneo mbalimbali wanaofanya biashara hizi wamekuwa wanafanya kwa utaratibu wanaojipangia wenyewe na hata kupelekea Serikali kupoteza fedha nyingi.
Mheshimiwa Naibu Spika, nafikiri sasa ni muda muafaka kuwe na vyombo maalum kwa uratibu wa mazao haya ili tija ipatikane. Kama katika hali ya sasa tunapata namna hii, basi utaratibu ukiwekwa, tutapata mara tano ya hapa.