Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi kwa mwaka wa fedha 2016/2017.

Hon. Dr. Shukuru Jumanne Kawambwa

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Bagamoyo

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi kwa mwaka wa fedha 2016/2017.

MHE. DKT. SHUKURU J. KAWAMBWA: Mheshimiwa Naibu Spika, nampongeza sana Mheshimiwa Waziri kwa hotuba nzuri ambayo imesheheni mipango na mikakati mizuri, kwa ukombozi wa Watanzania. Nawapongeza pia Naibu Waziri, Katibu Mkuu na Watumishi wote wa Wizara kwa maandalizi mazuri ya Bajeti. Ni mategemeo yetu kuwa utekelezaji wa Bajeti utakuwa wa ufanisi mkubwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, Mipango mizuri ya Wizara inatutia moyo. Katika Jimbo langu la Bagamoyo, Kilimo Ufugaji na Uvuvi, ndizo sekta zinazoishikilia Bagamoyo, isipokuwa tuna changamoto kadhaa ambazo tunategemea kupitia bajeti hii tutapata ufumbuzi.
Mheshimiwa Naibu Spika, mradi wa ECO-energy Bagamoyo ni changamoto. Sasa ni miaka 10 tangu mradi umeasisiwa, hadi leo hakuna mashamba, hakuna miwa, hakuna sukari, hakuna ethanol, hakuna umeme. Wawekezaji hawaoneshi dalili ya kuanza na jambo hili limeleta mzozo kwa wananchi. Wapo wananchi wa Gama ambao wanadai eneo lao kuporwa na ECO-energy, lakini miaka 10 sasa ufumbuzi haujapatikana. Waziri akifanya majumuisho, atueleze nini mpango wa Serikali kumaliza mgogoro huo wa wananchi wa Kitongoji cha Gama na lini Mradi utaanza kwa uhakika?
Mheshimiwa Naibu Spika, mpango wa Wizara wa kukazia kilimo cha umwagiliaji ni mpango sahihi sana. Bagamoyo tuna maeneo makubwa ambayo yanafaa kwa kilimo cha umwagiliaji. Tuna changamoto ya mafungu madogo kwa ajili ya uendelezaji wa kilimo cha umwagiliaji; Mradi wa umwagiliaji wa BIDP wenye eneo zaidi ya hekta 3,000, lakini ni sehemu ndogo sana ndiyo ina miundombinu ya umwagiliaji. Serikali itenge mafungu ya kutosha, kujenga miundombinu ya umwagiliaji ili kuwezesha zana za kilimo na pembejeo. Kilimo kina fursa ya kutoa ajira nyingi kwa vijana.
Mheshimiwa Naibu Spika, tatizo la wakulima na wafugaji bado halijapata ufumbuzi katika Jimbo la Bagamoyo. Wakulima wanapata tabu sana, kwa kuharibikiwa mazao yao na wafugaji, wakulima wamejaribu kila njia lakini mafanikio hayapo. Waziri atueleze, ana mikakati gani ya kumaliza matatizo haya ya wakulima wa Bagamoyo?
Mheshimiwa Naibu Spika, tunatiwa moyo na mikakati ya Wizara kuhusu kuendeleza uvuvi nchini, ila nimjulishe Waziri kuwa uvuvi wa Bagamoyo hauna mabadiliko yanayoonekana, kwa miaka 54 ya uhuru wetu, bado mvuvi wa Bagamoyo anatumia ngalawa yenye tanga na nyenzo hafifu sana.
Mheshimiwa Waziri afahamu kuwa uvuvi una fursa ya kutengeneza ajira nyingi za vijana, wanawake na wajasiriamali. Wizara ijikite katika kuongeza elimu ya uvuvi, ujasiriamali na uwezeshaji katika Sekta ya Uvuvi katika Jimbo la Bagamoyo, Wilaya ya Bagamoyo na maeneo yote ya uvuvi nchini.
Mheshimia Naibu Spika, naunga mkono hoja.