Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Mifugo na Uvuvi

Hon. Nuru Awadh Bafadhili

Sex

Female

Party

CUF

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Mifugo na Uvuvi

MHE. NURU A. BAFADHILI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kabla sijachangia chochote nimshukuru Mwenyezi Mungu kuniwezesha kusimama hapa kwa siku ya leo. Kwanza napenda kutoa pongezi kwa Serikali kudhibiti uvuvi haramu. Kwa sababu uvuvi haramu sina maana ya nyavu tu, uvuvi haramu ni wale pia wanaotumia mabomu. Vijana wetu wanaathirika kwa kutumia mabomu, kuna wengine wamekuwa ni vipofu, kuna wengine wamekuwa ni viwete hawana miguu, wengine hawana mikono na wengine wanapoteza maisha kutokana na mabomu.

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile mabomu haya yanaharibu matumbawe ambayo ndiyo nyumba za kuzalia samaki. Kwa hiyo, tunaishukuru sana Serikali kudhibiti hali hiyo na tunaiomba Serikali iendelee na hili zoezi kwa sababu tunao vijana na ushahidi upo wapo tayari wamepoteza hali yao ya kuona kutokana na mabomu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka kuzungumzia kuhusu hizi nyavu; kwa kweli wavuvi siyo wanaotengeneza nyavu, wavuvi wananunua. Sasa ilitakiwa wale wanaouza nyavu wazuiliwe kuuza zile nyavu ambazo hazistahili kwa ajili ya kuvulia samaki, badala ya kumwadhibu mvuvi ambaye yeye anakwenda kununua kwa ajili ya kufanya kazi yake.

Mheshimiwa Naibu Spika, Waswahili wana maneno wanasema unapofagia unaanzia kufagia pale miguuni kwako kwenda mbele. Sasa ninachosema sisi Mwenyezi Mungu ametupa bahari, Mungu ametupa maziwa na Mwenyezi Mungu ameweza kutupa mito. Kwa hiyo, tuna samaki wengi sana, sasa kabla hatujanunua samaki kutoka nje kwenye makopo, kwenye super markets ni lazima sisi tutumie samaki wetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, samaki wetu ni wazuri sana, kwanza unapokula samaki unakuwa una akili, mtu yoyote anayetumia samaki anakuwa na akili nzuri sana. Vilevile samaki ni chakula kizuri hata kama huna chakula chochote cha kula lakini unaweza ku-survive kwa kula samaki. Kwa hiyo, tujitahidi kula tuweze kula samaki wetu ambao wanavuliwa hapahapa, tuone fahari kutumia samaki wetu kuliko kununua samaki ambao wanatoka nje. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile wenzangu nadhani walikwishasema kuhusu leseni hizi ambapo mvuvi anakata leseni, mwenye chombo anakata leseni, msaidizi anakata leseni. Sasa hizo leseni zimekuwa nyingi kabisa kiasi ambacho wanalalamika hawapati faida. Matokeo yake wanapokwenda kwenye bahari kuu kule samaki wanauzwa hukohuko.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano, kama Tanga sisi tumepakana na Kenya. Kwa hiyo, samaki wanapopatikana pale wanauzwa mvuvi anarudi hivihivi anakwambia sikupata chochote. Kwa hiyo, tunapoteza mapato kwa ajili ya nchi yetu, hivyo, tuhakikishe hizi leseni zinapungua ili kuwapungizia wavuvi adha ya kupata kiasi kidogo katika hela zao wanazozipata. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tuna viwanda vya samaki kwenye Mikoa ya Kanda ya Ziwa lakini sisi watu wa Pwani hatuna viwanda vya kuchakata samaki. Sasa Mheshimiwa Waziri atuambie ni lini Serikali itafanya mpango wa kutujengea viwanda ambavyo tunaweza tukachakata samaki, kwa sababu tuna samaki wengi sana, tuna jodari, changu, kolekole, ngisi, pweza na wengineo. Pia tunajua pweza anawasaidia sana akinamama wazazi wakati wanapokuwa wamejifungua wanapata maziwa na akinababa pia wanasaidiwa na hao pweza, wenyewe wanajua jinsi gani wanavyowasaidia hao pweza. (Makofi/ Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa niongelee kuhusu ufugaji. Nadhani hapa ufugaji una matatizo kwa watu wanaoishi katika maeneo ya Miji. Kwa mfano, katika Jiji la Tanga watu wanajitahidi wanafuga ng’ombe katika nyumba zao, lakini inakuja amri kutoka Halmashauri ya Jiji kwamba atakayeonekana anafuga ng’ombe ndani ya nyumba yake atachukuliwa hatua. Sasa hiyo inamvunja moyo mtu ambaye anataka kufanya ujasiriamali wa ufugaji. Kwa hiyo, Serikali ihakikishe inaandaa utaratibu vilevile wale wafugaji wafuge kwa amani badala kwa kunyanyasika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile kuna mifugo inayotembea tembea barabani sasa mifugo hii hatujui ina wenyewe au haina wenyewe ile ndiyo mifugo ambayo inayotakiwa idhibitiwe ili isiweze kuzunguka barabarani wakati mwingine inagongwa na gari, wakati mwingine inasababisha ajali kwa watu, kwa hiyo mifugo ile inatakiwa iangaliwe.