Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi kwa mwaka wa fedha 2016/2017.

Hon. Juliana Daniel Shonza

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi kwa mwaka wa fedha 2016/2017.

MHE. JULIANA D. SHONZA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuzingatia kuwa kilimo ni uti wa mgongo wa Taifa letu; na kwa kuzingatia pia kuwa asilimia 75 ya Watanzania wanaishi vijijini na wanategemea kilimo ili kuweza kukidhi mahitaji yao ya kila siku. Suala la pembejeo limebaki kuwa changamoto kubwa kwa wakulima wa Tanzania, hususan wakulima wa kahawa na mahindi Mkoani Songwe.
Mheshimiwa Naibu Spika, vocha za mbolea huwafikia wakulima kwa kuchelewa sana na hata hivyo, huwa hazikidhi mahitaji. Hii inatokana na kwamba Mawakala wengi hawana sifa za kuwa Mawakala. Hivyo, hutaka makusudi kuchelewesha vocha za mbolea kwa wakulima ili baadaye baada ya msimu kupita, hupeleka vocha kwa wakulima na kwa kuwa msimu huwa umepita, hulazimika kupokea fedha kidogo toka kwa mawakala ili waweze kusaini kuwa wamepokea vocha kumbe sivyo. Hali hii hurudisha nyuma kilimo nchini na kuwakatisha tamaa wakulima wetu. Nashauri yafuatayo ili kuleta kilimo chenye tija:-
(a) Mfumo wa upatikanaji Mawakala wa Vocha za Mbolea, upitiwe upya ili kuondoa Mawakala ambao hawana sifa, wanaopata nafasi hizo kwa kujuana tu. Hili liende sambamba na kupitia upya mfumo wa ugawaji pembejeo ili ziweze kuwafikia walengwa tofauti na ilivyo sasa ambapo vocha za mbolea huwafikia wasio walengwa na walengwa wenyewe hawanufaiki na mfumo uliopo sasa.
(b) Nashauri Serikali ipitie upya hili suala la bei ya mazao ya wakulima wetu. Ni vyema Serikali ikafungua mipaka ili wakulima waweze kuuza mazao yao nchi jirani. Kutokana na kwamba uzalishaji ni mkubwa lakini soko siyo la kuridhisha, maana Serikali hushindwa kununua mazao yote toka kwa wakulima. Ni vyema Serikali ikafungua mipaka ili soko liamue bei ili kuongeza motisha ya uzalishaji kwa wakulima wetu.
(c) Nashauri Serikali ipunguze tozo katika zao la kahawa, ambapo kuna tozo zaidi ya 36, hivyo wakulima hawanufaiki na kilimo chao. Ni vyema Serikali ikapunguza hizo tozo zisizo za lazima kama walivyofanya kwenye zao la korosho.