Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwakawa Fedha 2018/2018 – Wizara ya Kilimo

Hon. Jumaa Hamidu Aweso

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Pangani

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwakawa Fedha 2018/2018 – Wizara ya Kilimo

NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote napenda nimshukuru sana Mwenyezi Mungu, lakini nitumie nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Magufuli kwa kazi nzuri anayoifanya katika kuwaletea maendeleo Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa namna ya kipekee nitumie nafasi hii kumpongeza Waziri wa Wizara hii pamoja na Naibu wake kwa kazi nzuri wanayoifanya, wamekuwa wakizunguka maeneo mbalimbali ya nchi yetu katika kuhakikisha wanatatua changamoto mbalimbali zinazohusiana na wakulima. Pongezi za kipekee katika nia yao ya dhati kabisa kuondoa tozo zaidi ya 21 katika kuhakikisha zinawaondolea kero wananchi hawa wakulima.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunatambua kabisa nchi yetu asilimia kubwa ya Watanzania wanaishi vijijini na wanategemea kilimo na kilimo chenyewe ni cha kudra za Mwenyezi Mungu kwa maana ya mvua, lakini Wizara yetu imejipanga vizuri sana katika kuhakikisha na kujua namna ya kuweza kumtoa Mtanzania, lazima tuwekeze katika kilimo cha umwagiliaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumebainisha eneo ambalo linafaa kwa kilimo cha umwagiliaji katika nchi yetu ni hekta milioni 29,000.4, lakini mpango wa Serikali mpaka itakapofika mwaka 2025 tuwe angalau tuna hekta milioni moja, na moja ya mipango ambayo tumeipanga tumeshafanya mapitio ya miradi yote kuona changamoto. Tumeona kuna miradi mingi ya umwagiliaji lakini haijakamilika, lakini bado uzalishaji wake unakuwa wa msimu mmoja. Tumeshajipanga, baadhi ya miradi ya umwagiliaji sasa hivi inafanya vizuri na imekuwa ikilima zaidi ya msimu mmoja, kama Mradi wa Lower Moshi, Madibila – Mbarali pamoja na Dakawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaishukuru Serikali kwa kutenga fedha zaidi ya shilingi bilioni 29 ambayo imewekeza katika suala zima la kilimo cha umwagiliaji. Nataka nilihakikishie Bunge lako Tukufu, sisi kama viongozi wa Wizara tutasimamia fedha hizi katika kuhakikisha tunajenga miundombinu ya maji ili hatimaye miradi hii ya umwagiliaji iweze kuwa na tija. Kwa sababu tunapozungumzia uchumi wa viwanda ni lazima tuwe na kilimo cha umwagiliaji kitakachoweza kutuzalishia mazao ya kutosha na yenye msimu wote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo sisi kama Wizara tumejipanga vizuri, na tunaahidi kushirikiana na wadau mbalimbali wa maendeleo katika kuhakikisha tunawekeza katika kilimo cha umwagiliaji ili mwishowe uchumi wa viwanda uweze kukamilika. Kubwa niwaombe san Waheshimiwa Wabunge tuipe ushirikiano wa dhati kabisa Wizara hii ya Kilimo kwa sababu watendaji wanafanya kazi nzuri sana, na sisi kama Wizara ya Maji tutawapa ushirikiano wa dhati katika kujenga na kuunda miundombinu hii ya umwagiliaji katika kuhakikisha azma ya Mheshimiwa Rais ya uchumi wa viwanda inatimilika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine katika bajeti hii tumeona nia ya dhati kabisa ya Serikali kuhusu ujenzi wa Bwawa la Kidunda. Bwawa hili litatumika katika suala zima la maji, lakini pia tutakuwa na kilimo cha umwagiliaji. Hii ni nia njema kabisa ya Mheshimiwa Rais wetu, Dkt. John Pombe Magufuli, katika uwekezaji wa kilimo cha umwagiliaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja. Ahsante sana.