Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwakawa Fedha 2018/2018 – Wizara ya Kilimo

Hon. Dr. Mary Michael Nagu

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Hanang'

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwakawa Fedha 2018/2018 – Wizara ya Kilimo

MHE. DKT. MARY M. NAGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kumshukuru na kumpongeza Waziri na Serikali kwa bidii. Naomba leo nianze kwa kuongea suala la masoko ya mazao ya kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakulima ndio wanaopinda migongo yao kulima mashambani na wanabeba gharama zote za kilimo. Hawakubaliani na wasingependa kukutana na pingamizi lolote la kuuza mazao yao ambapo wamepata masoko hata kama ni nje ya nchi, badala yake wanataka wasaidiwe ipasavyo. Jukumu la kuona Taifa lina uhakika na usalama wa chakula siyo la mkulima mmoja mmoja zaidi ya wao kulima kwa tija. Uamuzi wa Serikali wa kuwafungia mipaka wananchi kuuza mazao yao, matokeo yake ni Zambia kunyang’anya masoko ya asili nje ya mipaka (nchi jirani). Wakulima wa Hanang wamepata hasara kubwa na kukosa mitaji ya kulima msimu huu kwa kushindwa kuuza mazao yao. Walishindwa kununua pembejeo zao kutokana na bei ya juu pamoja na bei elekezi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naipongeza Serikali kwa kuamua kujenga maghala makubwa yenye uwezo wa kuhifadhi angalau tani 500,000. Jitihada hizo zikutane na NFRA kuongezwa fedha za kununulia nafaka ya akiba kuhakikisha usalama wa chakula na matumizi bora ya maghala. Napenda kuomba Serikali ipunguze kodi na tozo katika mifuko maalum ya kuhifadhi mazao ili bei ya kununua iwe nafuu. Hatua hii itapunguza upotevu wa mazao ndani ya maghala yaliyopo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuuliza utekelezaji wa commodity exchange umepotelea wapi toka sheria kupitishwa? Utekelezaji wa commodity exchange unategemewa kuwa ufumbuzi wa kudumu wa kuwapatia wakulima soko la mazao lililo muhimu. Tungependa kuona Serikali ikiweka mazingira mazuri katika kushiriki sekta binafsi katika sekta hii kikamilifu. Hii ni kwa sababu sekta binafsi ina uwezo mkubwa wa kuwekeza katika sekta hii ikiwa sekta binafsi itawekewa mazingira mazuri hasa yanayohusiana na sera za kikodi na udhibiti.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la mwisho ninalotaka kuongea ni ukuaji wa sekta ya kilimo kutoka 6% mwaka 2004/2005 hadi 2.1% mwaka 2016/2017. Ukichunguza sababu kubwa ni kupungua kwa bajeti iliyotengwa na kutolewa kila mwaka katika miaka iliyofuata. Naiomba Serikali iwe inaongezea sekta ya kilimo bajeti hadi kufikia 10% ya bajeti yote kwa mujibu wa Azimio la Malaba na Maputo. Ikiwa azimio hili likitekelezwa, litavutia sekta binafsi kuwekeza zaidi katika kilimo. Uwekezaji wa ziada utaongeza uzalishaji wa mazao na tija ambao utanufaisha Taifa kwa usalama na uhakika wa chakula, upatikanaji wa malighafi kwa ajili ya viwanda, ongezeko la mauzo ya nje ya mazao ya kilimo na ongezeko la mapato ya Serikali kupitia kodi na ushuru. Matokeo ya manufaa niliyotaja hapo juu ni kuongeza kasi ya azma ya Taifa kufikia uchumi wa viwanda na mapato ya kati ifikapo mwaka 2025.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ikiwa ni vigumu kufikisha bajeti ya kulima 10% ya bajeti ya Taifa tuondoe tozo zote kwenye pembejeo zote, zana zote za kilimo na uchakataji wa mazao ya kilimo. Hii itasaidia kupunguza gharama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naipongeza Serikali kuongeza bajeti iliyotengwa kutoka shilingi 162,224,814,000 mwaka 2017/2018 mpaka shilingi 214,815,759,000 katika bajeti hii tunayoijadili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, uhakiki wa mawakala ni jambo muhimu, lakini tunataka matokeo ya uhakiki ili wale wanaostahili wapate kulipwa na wasiostahili wachukuliwe hatua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushirika ni muhimu kwa wakulima lakini uliingiliwa na mchwa na kuingiza hofu kubwa kwa wakulima. Tuwauwe mchwa na kuupanga ushirika vizuri kabla ya kupitisha fedha za wakulima katika ushirika.