Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwakawa Fedha 2018/2018 – Wizara ya Kilimo

Hon. Margaret Simwanza Sitta

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Urambo

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwakawa Fedha 2018/2018 – Wizara ya Kilimo

MHE. MARGARET S. SITTA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi hii ili na mimi nichangie hoja iliyopo mezani. Nichukue nafasi hii pia kuwashukuru wapiga kura wa Urambo na wakati huo nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa nafasi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara ya Kilimo hii ni ngumu, kwa kweli nichukue nafasi hii kuwapa pole Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri, Makatibu Wakuu wawili pamoja na watendaji wote kwa kazi ngumu wanayoifaya, lakini wasikate tamaa, waendelee kufuatilia ili hatimaye wafanye kazi nzuri kwa manufaa ya Taifa letu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi hii kumshukuru Mheshimiwa Waziri Mkuu kipekee kwa kazi nzuri aliyoifanya Mkoani Tabora alipokwenda kushughulikia changamoto za tumbaku, ahsante sana Mheshimiwa Waziri Mkuu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mambo aliyafanya Mheshimiwa Waziri Mkuu pia ni kuteua Bodi mpya ya Tumbaku ambayo imeanza vizuri, nawatakia kila la kheri na hasa kwa vile wameongeza ndani yake wajumbe wenye uwezo na uzoefu wa zao hili la tumbaku, nawatakia kila la kheri. Pia nichukue nafasi hii kuiomba Serikali ikamilishe uteuzi wa Mwenyekiti ili bodi iweze kufanya kazi vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nachukua nafasi hii kumuuliza Mheshimiwa Waziri na Wizara nzima kwa ujumla, hivi kweli ina kalenda ya kilimo kwa mikoa yote ya Tanzania? Kama ina kalenda ya lini mvua zinaanza mkoa gani, wakati gani pembejeo zinatakiwa; iweje wakulima waanze kulima baadae washtukie hawana mbolea, inakuwaje? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu kitu ambacho kinawasaidia wakulima wapate mazao mazuri ni kuwa na pembejeo hususan mbolea kwa wakati, lakini inasikitisha pale ambapo wakulima wamelima lakini hakuna mbolea unaambiwa zitakuja wiki ijayo na mazao yanaharibika pale ambapo hayapati pembejeo kwa wakati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, mimi naomba Mheshimiwa Waziri atakapokuja kuhitimisha atuambie hivi kweli wanafanya kazi kwa kufuatana na kalenda ya misimu mbalimbali ya mvua katika mikoa kwa sababu mikoa inatofautiana ili tuache usumbufu wa wakulima kulima bila kuwa na matumaini ya kuwa na pembejeo yoyote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi hii pia kukumbusha Wizara kwamba katika mazao ambayo yamekuwa na matatizo hapa Tanzania moja wapo ni tumbaku; wakisahau kwamba tumbaku inaiingizia nchi hii fedha za kigeni zaidi ya asilimia 40. Sasa kama zao linaingiza zaidi ya asilimia 40 ya fedha za kigeni, iweje lisipewe kipaumbele ili nchi yetu iendelee kupata fedha za kigeni?

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii ni kwa sababu ukiangalia sana changamoto hizi si kwamba tunazizungumzia leo kwa mara ya kwanza, tumezungumzia kila wakata hasa hata mimi mwenye kama Mbunge wa Jimbo la Urambo nimekuwa nikilizungumzia suala la tumbaku na pembejeo kila ninapopata nafasi ya kuongea humu Bungeni. Sasa iweje zile changamoto bado ziendelee pamoja na jitihada kubwa ya Mheshimiwa Waziri Mkuu na Serikali kwa ujumla?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano tumbaku tofauti na mazao mengine, tumbaku inatakiwa mbolea iwe imefika kabla ya mwezi wa saba. Je, Serikali inatuhakikishia kwamba mbolea inayotumika na tumbaku hasa NPK itakuwa imefika nchini hapa na kupatikana kwa wingi kabla ya mwezi wa saba? Kwa sababu ndipo ambapo wanaanza kuandaa mabedi (seed beds) kwa ajili ya kupanda mbegu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, mimi ningeomba hili suala Mheshimiwa Waziri husika alizungumzie pia anapo- wind-up, kweli wakulima wa tumbaku wanahakikishiwa kwamba kuna mbolea ya NPK tayari nchini mwezi wa saba karibu unafika?

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tumekuwa na tatizo kubwa sana la pembejeo hasa NPK ambayo inategemewa sana na wakulima wa tumbaku. Kwa sasa hivi bei ya tumbaku inatofautiana kwa sababu ya utaratibu wa uingizaji wa mbolea nchini. Je, Mheshimiwa Waziri anaweza kutuhakikishia kwamba kama wamefanya utaratibu wa bulk procurement kwa ajili ya mbolea za mahindi, hawawezi kufanya utaratibu huo huo pia kwa ajili ya zao la tumbaku ili wakulima wapate tumbaku nyingi kwa wakati mmoja lakini pia iondoe tofauti ya mbolea inayojitokeza kutokana na manunuzi ya mbolea kutoka nje. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala ambalo tumekuwa tukiliongelea sana Mheshimiwa Waziri anajua, msimu uliopita sasa hivi wa zao la tumbaku tumepata shida sana wakulima wa tumbaku kutokana na tumbaku nyingi kushindwa kuuzwa, na hii imetokana na uhaba wa masoko. Je, Mheshimiwa Waziri anaweza kutuhakikishia sisi wakulima wa tumbaku kwamba ameweka utaratibu mpaka sasa wa kupata wanunuzi wangapi ili waingie nchini wasaidie kuinua bei ya tumbaku? Kwa sababu panapokuwa na wanunuzi wengi kunakuwa na ushindani.

Je, Mheshimiwa Waziri utakuja utuambie hatua ambazo tayari Serikali imeshachukua, hata kwa kutumia Waheshimiwa Mabalozi waliopo nchi za mbali ili kupata wanunuzi ili kuwe na ushindani katika kuuza tumbaku yetu nchini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la masoko ni la muhimu sana ukiangalia adhabu waliyopata wakulima wa tumbaku mwaka huu. Kwa vyovyote mkulima anapolima kitu cha kwanza anachoangalia ni soko, sasa anapokuwa na uhakika wa soko ndipo analima vizuri ili aweze kujiendeleza yeye mwenyewe kibinafsi lakini pia kusaidia nchi yetu kuingiza fedha za kigeni kutoka nje. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ni suala muhimu sana la Bodi ya Tumbaku, kweli Bodi ya Tumbaku ipo lakini nasikitika kusema kwamba bado haijawezeshwa kufanya kazi vizuri, maana yake ni kwamba kupata fedha za kutosha… (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)