Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwakawa Fedha 2018/2018 – Wizara ya Kilimo

Hon. Jitu Vrajlal Soni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Babati Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwakawa Fedha 2018/2018 – Wizara ya Kilimo

MHE. JITU V. SONI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Naomba nichukue fursa hii kwanza kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa siku ya leo. Mimi naomba nitoe ushauri kwa Serikali, kuna maeneo mengi tu lakini naomba nianze kwa kusema Mheshimiwa Spika kama alivyounda Kamati mbalimbali za kuangalia kwa mfano Tanzanite, makinikia na masuala ya uvuvi wa baharini, angeunda Kamati ya kukaa pamoja Wabunge ili tuweze kuona maoni mbalimbali na tuweze kuishauri Serikali nini cha kufanya kwenye sekta hii ya kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini la pili ningeomba Serikali kwa kupitia Waziri wa Kilimo waangalie Hansard za miaka ya nyuma ushauri mbalimbali ambao ulikuwa unatolewa miaka nenda rudi, je, upi umefanyiwa kazi? Kwa sababu haya mambo Wabunge tunayasema kila mwaka lakini kwa sehemu kubwa unakuta ushauri huo hautiliwi maanani. Haya mawili yakifanyika, nina uhakika kuna mengi tutakuja kufaidi huko mbele ya safari.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nianze kwanza kwa kusikitika kwamba bajeti ya sekta hii ya kilimo kila mwaka huwa inaendelea kushuka lakini bajeti kuu inaendelea kupanda na lengo lilikuwa bajeti iongezeke. Wizara ya Kilimo inafanya kazi yake vizuri sana ikiongozwa na Waziri, Naibu Waziri na wataalam wao, lakini hakuna uratibu au coordination baina ya Wizara ya Kilimo na Wizara zingine zote na ndiyo maana tunakwama. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni muhimu tuangalie tunataka kuelekea wapi. Moja, naomba tuwe na mkakati kwamba bidhaa zile kuu ambazo tunaagiza kutoka nje kwa mfano mchele, sukari, mafuta, mbegu hata hizi juice zote za matunda hakuna tone la juice ambayo tunakunywa inazalishwa hapa nchini, yote ni concentrates zinazotoka nje ya nchi wakati bidhaa zote hizi tunaweza kuzalisha hapa nchini.

Ni vizuri tuje na mkakati kwamba ndani ya hii miaka miatatu au minne mchele, sukari, mafuta, mbegu na vitu hivi tutazalisha ndani ya nchi, uwezo tunao na namna ya kufanikiwa hivyo ni kuwekeza kwenye utafiti.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hatuweki fedha kwenye utafiti na hata hii leo tukisema tunataka kujitosheleza kwa mafuta hatuna mbegu. Hatuna mbegu nzuri ambayo tunaweza kujitosheleza lakini hivyohivyo kwenye maeneo yote inatakiwa tuwekeze zaidi kwenye utafiti. Tuna vituo 17 vizuri na bajeti yake sijaona kwamba kila kituo kitapatiwa shilingi bilioni ngapi ili vituo hivyo viweze kuboreshwa kwa kuwekewa vifaa vya kutosha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mbali na hiyo narudia kusema kwamba hakuna coordination ndani ya Serikali. Leo hii vituo vya utafiti vinaomba msaada kutoka nje, vifaa vikija vinatozwa kodi, vifaa vinasaidia Mikocheni, Makutupora hapa kwenye umwagiliaji, vifaa vya umwagiliaji ambavyo havina kodi lakini wametozwa zaidi ya shilingi milioni 42. Sasa kama Serikali kwa Serikali inatozwa kodi, je, mwananchi na mkulima wa kawaida itakuwaje?

Mheshimiwa Mwenyekiti, mkulima kitu anachohitaji ni uwezeshaji na mazingira mzuri ya kufanya kazi. Moja, Benki ya Kilimo ingepewa mtaji wa kutosha ile itoe mikopo wakulima waweze kununua vifaa vya kisasa kufanyia kazi na Mfuko wa Pembejeo uwezeshwe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mbali na hilo tufanye utafiti, ndiyo maana nasema hiyo tume au Kamati ya Bunge ikikaa iangalie masuala haya. Leo hii kodi na tozo tulizoainishiwa hapa nyingi tumeshangilia, lakini ipi yenye athari hata moja ambayo imemsaidia mkulima moja kwa moja, hakuna. Ukiangalia ushuru wa mazao iko palepale, ni ile tu kwamba waliokuwa wanakusanya 3% tumeshusha kwenye maandishi tu kutoka 5% kuja 3%, lakini mkulima wa kawaida hakuna mahali amefaidika na hilo. Zile kodi kumi na zaidi hakuna mahali mkulima zimemnufaisha moja kwa moja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, bila kuwekeza zaidi kwenye ushirika na kutoa elimu vizuri hatutafika popote. Tumeanzisha commodity exchange leo mwaka wa tano hakuna maendeleo yoyote yanayofanyika pale. Stakabadhi ghalani pamoja na commodity exchange inaweza kuwa mkombozi
wa mkulima. Kwa hiyo, kwenye suala hilo pia, tuweke nguvu zadi, elimu itolewe, lakini Serikali iwe na nia njema, iwe na mkakati wa kuhakikisha kwamba haya yote tunaweza kufikia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii Wabunge wengi wamechangia masuala ya mbolea. Kwenye mbolea kuna upotoshaji mkubwa unatokea kwa sababu hatuelewi. Ni vizuri tukajua kwamba sawa na binadamu huendi hospitali ukapewa tu dawa, ukimueleza unaumwa kichwa, basi daktari anakupa dawa; hivyohivyo kwenye udongo unatakiwa ukapimwe. Pima udongo kujua mbolea inayotakiwa wataalam watakwambia tumia mbolea A, B, C, ndiyo utumie mbolea hiyo badala ya hii ya kwa ujumla tu. Watu wanapiga kelele kwamba Minjingu haifai, nini haifai, mkakati wa Minjingu ni kuzalisha mbolea ifikapo mwaka 2021 kiwanda kile kinachojengwa kule…

T A A R I F A . . .

MHE. JITU V. SONI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Wangekuwa kwanza wanaelewa kinachosemwa badala ya kurukia tu. Nimesema fanya utafiti kwenye udongo wako, ukifanya utafiti upate ushauri. Je, nyanda hizo zilifanya utafiti wa udongo wao wakaambiwa watumie aina gani ya mbolea? Kama utafiti huo upo ulete mimi niko tayari hapa kukulipa fidia wewe. Mimi niko tayari kulipa fidia kama ana utafiti wa udongo uliofanywa, nina uhakika hamjafanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye masuala yote lazima twende kwa utafiti na ndiyo maana nasema tuwekeze kwenye utafiti badala ya kila siku hapa kupiga tu kelele kwamba tufanye A, B, C. Twende kisayansi, kilimo ni sayansi, kilimo ni biashara, kilimo tukiwekeza vizuri ndiyo kitakomboa watu wote. Watanzania 100% wanategemea kilimo cha humu ndani kwa sababu tunategemea chakula kinachozalishwa humu nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna jambo lingine muhimu sana inabidi Serikali ijipange kuhusu hili suala la regulatory bodies. Uzalishaji wa ndani ya nchi gharama inakuwa kubwa na ndiyo maana bidhaa hizi zinatoka nje ya nchi kutokana na hizi tozo, ushuru, ada na leseni mbalimbali ambazo tunatozwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, haya yote tungekuwa tumeyafanya vizuri nina uhakika kwamba gharama za uzalishaji zitapungua na viwanda vingi huku ndani vitapata malighafi kutokana na sekta hii ya kilimo, mifugo na uvuvi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kwenye yale mazao ambayo Wabunge wengi wameyazungumzia, leo hii Dodoma inaweza kuzalisha zabibu, lakini bado tunaagiza zabibu kutoka nje ya nchi wakati mvinyo na zabibu zingeweza kuzalishwa kwa wingi tukapata fedha hapa ndani lakini pia tukawa tuna-export. Tukiangalia upande wa migomba, Serikali ilikuwa na mpango mzuri wa kuzalisha miche ya tissue culture ipelekwe Kanda ya Ziwa. Suala lile lingefanyiwa kazi ungekuta ugonjwa ule ungepungua sana na wananchi wa kule wangekuwa wamepata chakula cha uhakika na ndizi za uhakika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia nishukuru kwamba mpango wa kuanzisha LAPCOT mmeusema. Naendelea kushauri kwamba mpango huu uanzishwe mapema ili kanda ile pia ambayo inaweza kuzalisha mambo mengi sana katika hii sekta ya kilimo kwa ujumla wake na wenyewe waweze wapate mafanikio kama SAGCOT …

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)