Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwakawa Fedha 2018/2018 – Wizara ya Kilimo

Hon. Willy Qulwi Qambalo

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Karatu

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwakawa Fedha 2018/2018 – Wizara ya Kilimo

MHE. QAMBALO W. QULWI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa nafasi hii adhimu ambayo nimeipata ili na mimi niweze kuchangia Wizara hii muhimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimesoma kitabu cha Mheshimiwa Waziri mwanzo mwisho, mara mbili, mara tatu.

Kama kweli haya yalioandikwa humu yatakwenda kutekelezwa nchi hii itakuwa paradiso nyingine. Hata hivyo, inaonyesha miaka yote mitatu iliyopita Waziri hakuwa na hela hivi atafanya maajabu gani ili yote haya mazuri aliyoandika humu yaende kutekelezwa? Sioni tofauti kubwa kati yake Waziri na Waziri Kivuli ambaye hana mafungu, sana sana Waziri anatembelea gari la Serikali. Kwa sababu miaka yote anapata chini ya asilimia 20, atakwendaje kutekeleza haya yote yameandikwa humu ndani? (Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nchi hii tulikuwa na historia ndefu ya ukulima uliotukuka wa mazao ya kahawa, mkonge, ngano na mazao mengine leo mazao hayo yameangukia pua. Sasa mahindi tunakwenda kuangukia pua, mbaazi tumekwishaangukia pua, ngano tunaangukia pua, hivi mkulima wa nchi hii alime nini ili awe salama? Sioni wapi yupo salama. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niende kwenye masoko ya mazao. Mwaka jana mahindi tuliangukia pua, mbaazi tukaangukia pua, safari hii tunakwenda kuvuna, hivi mnatuambia nini sisi wakulima? Tunakwenda kuangukia pua au sasa tunaangukia mdomo ili meno yaishe? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niwakumbushe Waheshimiwa Wabunge mwaka jana wakati Serikali imekuja kutoa kauli ya zuio la kupeleka mahindi nje, Waziri Mkuu alikuwa amekaa pale alipotoa kauli hii ni sisi wenyewe ambao tulimshangilia na upande huu ndiyo mlimshangilia zaidi, wale wanaojiita the big five ndiyo walishangilia kuliko wengine. Kweli wanasema mzigo mzito mbebeshe Mnyamwezi, leo Tizeba ataubeba mzigo huu kwa sababu haikuwa kauli yako. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi wakulima tunalima ili tuzalishe chakula na tukauze ziada. Nimelima mahindi ya kutosha halafu unaniambia nisiuze, hivi unanizuia nisiuze nimekopa shamba niko mwenyewe, nimelima niko mwenyewe, nimenunua mbegu niko mwenyewe, palilia mwenyewe, navuna mwenyewe, halafu unakuja unasema usiende kuuza kule. Sasa kama hutaki nikauze huko basi nunua wewe, sasa na wewe huna uwezo wa kununua si uniche huru nikauze? (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nadhani wakati mwingine huyu mkulima tumuache huru auze. Tuko kwenye utengamano wa Afrika Mashariki haya mambo ya kuuziana mazao ni ya kawaida. Mimi nikivuka Namanga naona soko zuri unaniambia nisiende, hasa nunua wewe basi unipe hela nzuri huwezi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo tumefika mahali wakulima wa mbaazi wameacha mbaazi shambani wanachungia ng’ombe, mahindi yanaoza kwenye maghala yetu, mnataka tupeleke watoto shule, mnataka tujenge madarasa, mnataka tuchangie hospitali, fedha hizi tunapata wapi? Mimi nadhani kwa kweli hatuwatendei haki wakulima. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, juzi tulikuwa kwenye semina ya kilimo masula ya viwavijeshi vamizi. Wabunge tulipata semina lakini imekuja kwa kuchelewa sana, huko vijijini watu wanavuna halafu ndiyo mnatufanyia semina. Pia ilikuwa semina ya Wabunge na wakulima je? Wakulima wamehangaika mwaka mzima hakuna mtu anayewasaidia si Mkurugenzi na si Waziri ni mateso matupu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tishio la viwavijeshi huyu ni kubwa sana, hili kwa kweli ni janga la nchi. Bahati mbaya sana sijui kama nchi hii haina mfuko wa kuhangaika na majanga, kwa sababu hakukuwa na namna ya kumsaidia mkulima. Hata wale wa Maafisa Ugani hawana uhakika wa dawa ambayo inaweza kupambana na mdudu huyu, wakulima wameachwa tu. Kwa hiyo, tusipoangalia mwaka huu hata mavuno yatakuwa chini sana lakini pia ubora wa mahindi yatakayozalishwa utakuwa chini kwa sababu huyu mdudu ametusumbua sana. Kwa hiyo, nafikiri tuwe na mfuko imara ambapo likitokea janga kama hili wananchi waweze kusaidiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hivi Maafisa Ugani ndiyo wamekuwa Watendaji wa Kata na Vijiji. Nakubaliana kabisa na pendekezo…

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)