Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Kilimo

Hon. Katani Ahmadi Katani

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tandahimba

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Kilimo

MHE. KATANI A. KATANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nikushukuru lakini kabla sijaendelea kuchangia niseme tu kwamba siungi mkono hotuba hii ya Wizara ya Kilimo. Kama mimi ningekuwa Waziri mwenye dhamana kwa namna mambo yalivyo ningejiuzulu kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Sheria Na. 18 ya mwaka 2009 ukiisoma pamoja na Sheria ya Fedha Na.15 ya mwaka 2010, kifungu cha17A(2) kinaeleza wazi kuwa asilimia 65 ya export levy inakwenda kwenye tasnia ya korosho. Msimu wa korosho 2016/2017, asilimia 65 ya export levy ambayo ni shilingi bilioni 77, ukijumlisha na maduhuli ya nyuma jumla ya shilingi bilioni 91 haijaenda kwenye tasnia ya korosho. Msimu huu tuliomaliza wa 2017/2018, asilimia 65 ya export levy ni shilingi bilioni 115 haijaenda kwenye tasnia ya korosho. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Waziri atuambie kama fedha hii ya korosho shilingi bilioni 206 imekwenda kulipia Bombardier wakulima wa korosho wajue. Leo hakuna pembejeo wakati fedha hizi asilimia 65 ndizo zinatumika kwenye pembejeo. Wapo watu wamezalisha miche inayokuja mpaka Dodoma mpaka leo hawajalipwa, wapo watu mwaka jana wamegawa pembejeo mpaka leo hawajalipwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tarehe 30 Mei, 2017, TRA ilitoa taarifa na walimuandikia Katibu Mkuu Fedha kwamba export levy shilingi bilioni 75 imekusanywa, inatakiwa iende Bodi ya Korosho, haikwenda. Tarehe 15 Desemba, Katibu Mkuu wa Kilimo kaandika barua kumpelekea Katibu Mkuu wa Fedha, fedha haijaenda. Juzi amekuja Waziri wa Fedha anatupa blabla, anasema kuna shilingi bilioni 10, hakuna shilingi bilioni 10, ni sanaa tu, hii Serikali imekuwa ni Serikali ya kubeti. Kwenye kilimo tunabeti? Ndugu zangu kilimo si suala la kubeti mnalolifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo ukisoma kitabu cha Mheshimiwa Waziri, ukurasa 30, ili ujue kwamba hii fedha haipo, Waziri anasema:-

“Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa 2018/2019 kiatilifu aina ya sulphur pamoja na vifungashio vya korosho (magunia) havitatolewa kwa njia ya ruzuku kama ilivyokuwa msimu wa kilimo 2017/2018. Wakulima watauziwa kwa bei ambayo itatangazwa na Bodi ya Korosho.”

Mheshimiwa Mwenyekiti, maana yake mpaka leo bei haijatangazwa. Hata hivyo, ukienda kwa wakulima wa korosho sulphur inauzwa Sh.32,000. Ukiendelea kusoma ukurasa huu, utaona mchakato unaendelea unawahusisha na watu wa benki kwenye kukopa huko. Kwa hiyo, inaonyesha wazi kabisa kwamba fedha za korosho zile za export levy ambavo zipo kisheria hazipo, ndiyo maana Mheshimiwa Waziri ameandika haya. Atakapokuja ku-wind up atuambie kama fedha zimelipa Bombardier, shilingi bilioni 206 miaka miwili mfululizo, tunakwenda mwaka wa tatu hazionekani mtuambie. Mnacheza kwenye kilimo mnawadanganya Watanzania, mnawadanganya wakulima wa korosho. (Makofi)

Mhesimiwa Mwenyekiti, mbaya zaidi ukienda Mtwara, Tandahimba na Newala kuna Chama Kikuu cha Ushirika kinaitwa TANECU. Hiki Chama wenyewe hawa wanadanganywa, Chama hakifanyi vizuri, kinaendeshwa na Serikali. Nami nakuwa na mashaka, inawezekana TANECU Waziri ana hisa nacho. Moja, mwaka jana TANECU imekopa fedha TIB imeshindwa kulipa Waziri ameindikia Bodi ya Korosho wameikopesha TANECU shilingi bilioni 2 za Bodi ya Korosho, huyu huyu Waziri Tizeba, shilingi bilioni 2. Leo Waziri amekuwa mtu wa benki, wameshindwa kuilipa benki halafu anakaa anakuja anakwambia TANECU wanafanya vizuri kwa kuwapa fedha Serikali? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 2006 Waziri Kikwete ameinusuru TANECU ikiwa inadaiwa. Mwaka 2008, 2009, 2010 wameshtakiwa na River Valley wamechukua fedha za wakulima zaidi ya shilingi bilioni moja na kitu wamemlipa River Valley, nimekwambia na kwenye takwimu za korosho zenyewe nimemuonyesha tofauti Mheshimiwa Waziri. Msimu wa korosho wa 2016/2017 ukienda kwenye Bodi ya Korosho Tandahimba wamekusanya tani zaidi ya 70,000 lakini maelezo ya TANECU aliowakopesha fedha wametupa maelezo kwamba tumekusanya tani 68,000, kuna tani zaidi ya 2,500 zimepigwa, ziadi ya shilingi milioni 600 za wana-Tandahimba, anajua, nimempa na takwimu wanaendelea kuibeba TANECU. Kumbe nilikuwa sijajua kwamba wanaibeba TANECU kwa sababu kuna maslahi, wameikopesha shilingi bilioni 2 wanatafuta namna ya kurejesha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sehemu ambazo zina matatizo makubwa ni kwenye tasnia ya korosho. Leo Waziri huyu hawezi akatuambia sababu ya msingi ya kumuondoa Mkurugenzi wa Bodi ya Korosho. Kama fedha hawapeleki, kama yeye ndiye amemuandikia Mkurugenzi wa Bodi ya Korosho akopeshe shilingi bilioni 2 lakini juzi wamemtoa kafara Mkurugenzi wa Bodi ya Korosho. Kama tatizo lilikuwa Bodi ya Korosho kwa nini wasingeondolewa watumishi wote wa Bodi ya Korosho? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mambo haya si ya leo, Mkurugenzi wa kwanza ameondolewa hakuna maelezo yanayojitosheleza, Mkurugenzi huyu ameondolewa hakuna maelezo yanayojitosheleza, kumbe maelezo ndiyo yale wanatuma vikaratasi wenyewe maana nina barua yake ya kumuagiza Mkurugenzi kuwakopesha shilingi bilioni 2 TANECU ambapo mpaka leo wamekusanya shilingi bilioni 3 kwa wakulima wamerejesha shilingi bilioni mbili CBT. Kwa hiyo, wana maslahi yao na inawezekana kuna biashara ndani yake wanafanya, mwisho wa siku wanakaa wanatuambia unajua, TANECU ile, kumbe wenyewe wana mipango yao kule. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hawa wakulima wa korosho tuwaonee huruma sana. Mnasema mna nia njema kwenye mazao haya, juzi mtu mmoja sijui ni Waziri sijui ni nani anauliza suala la mbaazi hapa anasema mbaazi ni chakula. Sisi Lindi na Mtwara mbaazi ni chakula na ni zao la biashara na siyo chakula tu. Mnawavunja moyo wakulima, mwishowe mtawaambia watu wa Rukwa kwamba mahindi ni zao la chakula tu na si zao la biashara. Ni Serikali ya namna gani hii? Serikali ya kubetibeti, inakuwaje? Inakuwaje tunabeti kwenye masalhi ya wakulima? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo tunapozungumza kumekuwa na danadana kwenye sulphur, kumekuwa na danadana kwenye mambo haya, wanakaa Bodi ya Korosho na...

KUHUSU UTARATIBU . . .

MHE. KATANI A. KATANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakubaliana kwa tafsiri yako, maana ungenitaka tafsiri yangu ningeifafanua, nakubaliana na tafsiri yako, niendelee kuchangia. Mheshimiwa Mwenyekiti, nafuta ili niweze kuendelea kuchangia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunayazungumza maneno haya, mfano mzuri kwa nini tunasema tunabahatisha bahatisha. Mheshimiwa Pascal Haonga akiwa anatoa rekodi ya bajeti tunayoipanga humu na namna ya fedha inavyopelekwa kama si kubahatisha ni kitu gani?