Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa

Hon. Augustino Manyanda Masele

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbogwe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa

MHE. AUGUSTINO M. MASELE: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hotuba ya Mheshimiwa Waziri. Hoja yangu katika mchango wangu ni kuishauri Serikali kwamba ijikite katika kujenga jeshi lenye nguvu kwa kujenga viwanda vya zana za kivita. Tanzania ya viwanda na ujenzi wa uchumi wa kisasa hauwezekani bila kuwa na nguvu za kijeshi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mataifa mengi ulimwenguni yameundwa baada ya vita kupiganwa na zikawepo nchi mbalimbali na ambazo zimejikuta zikianza kujenga viwanda vyenye kulenga katika kulinda mipaka ya Mataifa husika. Kwa misingi hiyo, ni vyema Taifa letu likawekeza zaidi katika Viwanda vya Ndege za kivita, Viwanda vya Makombora, Viwanda vya Magari ya Kivita na Mitambo vikiwemo vifaru, magari na meli za kivita zikiwemo manowari (submarine).

Mheshimiwa Mwenyekiti, tujifunze kutoka Mataifa machanga ambayo yalitutangulia kupata uhuru kwa kipindi kifupi cha miaka kumi, mfano, Mataifa ya Uchina (1949), India (1948), Israel (1948) na Pakstani (1948). Mataifa haya yamefanikiwa pakubwa kwa kuwekeza katika viwanda vya kuzalisha silaha kwa kushirikiana na Mataifa yaliyowatangulia katika utafiti, sayansi na teknolojia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mataifa yaliyotangulia ni pamoja na Marekani, Urusi, Ufaransa, Italia na hata Uingereza na Mataifa mengine ya Ulaya. Nafahamu jeshi letu linazo taasisi za Nyumbu na Mzinga. Naishauri Serikali kuhakikisha inazitengea taasisi hizi fedha za kutosha ili ziweze kuwekeza zaidi katika utafiti, sayansi na teknolojia, ikibidi kununua watalaam katika Mataifa yaliyoendelea katika nyanja za viwanda vya zana za kijeshi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ipo mifano kuhusu Mataifa mengine namna yalivyofanya. Marekani walimchukua Albert Cinstein Mvumbuzi wa bomu la nyuklia tokea Ujerumani na kulisaidia Taifa la Marekani kujiundia silaha za Kimarekani. Marekani pia wamekuwa wakitumia mbinu mbalimbali kuchukua teknolojia kutoka Taifa la Urusi na kinyume chake pia yaani Urusi kuchukua teknolojia tokea Marekani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Tanzania haiko peke yake, inayo Mataifa rafiki ambayo yanaweza kuisaidia, kwani ni dhahiri haliwezi kusubiri mpaka kugundua silaha zetu wenyewe. Iran imekuwa ikisaidiwa na Urusi kuwa na viwanda vya silaha za kivita. Israel ikisaidiwa na Marekani kujenga viwanda vya silaha za kivita wakati wa Dola la Kisovieti. Wachina walimchukua mtaalam wa vita kutoka Ukraine akasaidia uundaji wa meli za kivita Uchina na ku-copy teknolojia kutoka Urusi. Vile vile Iran imepata teknolojia ya matumizi ya nuclear toka Urusi kwa kuwa tu Iran inao utajiri mkubwa wa mafuta ya Petrol.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mantiki hiyo Tanzania ni tajiri mkubwa wa rasilimali kuanzia madini, gesi, maliasili na kadhalika. Kwa hiyo, kulingana na ukubwa wa nchi yetu na utajiri tulionao, ipo haja kubwa kwa nchi yetu kuwekeza kwa kiwango kikubwa katika viwanda vya zana za kijeshi vya Mzinga na Nyumbu. Hatuna kisingizio hata kidogo. Ni muhimu sana kuwa na Sera ya Taifa ya Ulinzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nchi yetu ikiwekeza katika Sekta ya Ulinzi tukawa na viwanda kwa ajili ya ndege za kivita, meli za kivita, vifaru na ikiwezekana tuwe na matumizi ya amani ya madini ya Urani ambayo yanazalishwa nchini mwetu, maeneo ya Namtumbo na Bahi hapa Dodoma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.