Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa

Hon. Joseph Roman Selasini

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Rombo

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa

MHE. JOSEPH R. SELASINI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Jeshi letu ni zuri na Wizara iko vizuri. Uzuri huo unatokana na uongozi wa Wizara na Jeshi lenyewe. Kwa sababu hiyo nichukue nafasi hii kumpongeza Waziri na kumpongeza Mkuu wa Majeshi. Vile vitengo vingine siwafahamu na sivifahamu vyote, kwa hiyo, wachukue tu kwamba ni pongezi zangu kwa wote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kanali Mabeyo namfahamu, ni mtu mpole na mnyeyekevu sana. Nilifanya naye kazi ya Kanisa, mimi nikiwa Mwenyekiti wa Wazee Walei wa Jimbo Kuu la Dar es Salaam, yeye alikuwa anaongoza kitengo kidogo sana cha ulinzi cha Parokia ya Segerea. Meja Jenerali anajishusha, anafanya kazi na watu wa kawaida hata kufagia Kanisa. Ni mtu mzuri sana, nampongeza sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na pongezi hizi nashauri tu mambo machache. Ushauri wa kwanza, Jeshi letu lina heshima katika Majeshi ya Afrika. Heshima yake inatokana na misingi yake. Hili ni Jeshi la Wananchi, ni jeshi letu. Kwa sababu hiyo, nawaomba wanasiasa na viongozi wa Taifa letu tusilichafue Jeshi hili kama tulivyolichafua Jeshi la Polisi. Leo katika Taifa letu ikitokea ajali inayohusu Polisi, watu wanauliza wamekufa wangapi? Tusilipeleke Jeshi letu huko. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nasema hivi kwa sababu tarehe 3 Februari, 2018, wakati wa kutunuku Kamisheni kwa baadhi ya vijana wetu waliohitimu pale Arusha, shughuli hii ya Jeshi ambayo ni muhimu sana ilihusishwa na tukio la kisiasa la kupokea Madiwani waliojiuzulu kutoka chama fulani cha siasa kwenda kwenye chama kingine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kitendo hiki kilipunguza kwa kiasi kikubwa sana heshima ya siku ile. Kwa sababu tuna matukio mengi sana ambayo tunaweza kufanya siasa, lakini siyo katika tukio muhimu kama hili. Huku ni kulinajisi jeshi letu. Kwa sababu hiyo, naomba wanasiasa wajiepushe kabisa na kuwafanya Watanzania ambao tuko kwenye vyama mbalimbali tukaonekana kwamba sisi hatuhusiki na Jeshi kwa sababu Jeshi lilisimama na wanasiasa wa chama fulani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata katika operation fulani iliyotangazwa na chama cha siasa (Operation UKUTA), Wanajeshi walionekana mtaani wakifanya mazoezi. Jeshi letu ni Jeshi linalolinda mipaka yetu, haya mambo ya ndani yanahusu Jeshi la Polisi. Kwa nini tunalihusisha jeshi letu na mambo ambayo yanaweza yakashughulikiwa na Jeshi la Polisi? Au ndiyo kusema kwamba sasa Jeshi linataka lionyeshe misuli yake kwa wananchi ili wananchi waliogope? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi hatuliogopi Jeshi la Wananchi, kwa sababu ni Jeshi letu. Hawa ni watu wetu. Kwa sababu hiyo, narudia kuomba, heshima ya Jeshi la Wananchi iendelee kubaki, tunawaheshimu viongozi wake, tunawapenda viongozi wake, waendelee kutunza jeshi hili ili liwe Jeshi la Wananchi wa Tanzania na siyo vinginevyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri mwingine ambao nangependa kutoa. Inaonesha kwamba katika nchi yetu kuna viashiria niseme vya kigaidi. Ninaliangalia tukio la Kibiti, matukio ya watu kupotezwa na watu wasiojulikana na matukio ya kupigwa risasi kwa watu mbalimbali hapa nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii ni dalili kwamba kuna udhaifu mkubwa sana wa Kitengo cha Upelelezi katika Jeshi la Polisi. Kwa sababu hiyo, namwomba Mkuu wa Majeshi na Jeshi lenyewe kuangalia uwezekano wa kutumia Military Inteligence kusaidia Jeshi la Polisi ili matukio haya ya aibu katika nchi yetu yaweze kupunguzwa na kuondoshwa kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, iko hofu. Ukisoma mitandao hata leo hii, watu wanasema kwamba kuna maeneo fulani fulani nyeti katika nchi yetu sasa yanalindwa na Askari kutoka nje, hususan Rwanda. Sasa katika hofu hiyo, inawezekana ikahusishwa pia na watu wasiojulikana. Kwa hiyo, naomba sana Kitengo cha Military Inteligence cha jeshi kiimarishwe ili kuweza kuangalia haya maeneo ambayo watu wana hofu nayo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaliamini jeshi letu pamoja na weledi wake. Hatuna sababu yoyote ya kufikiria kwamba kuna mahali popote katika nchi yetu tunaweza tukaazima watu kuja kutusaidia ulinzi. Wanajeshi wetu ni weledi na wanaweza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo ningependa kulizungumza ni ajira. Kuna utaratibu mzuri wa ajira ambao vijana wetu kutoka JKT wanachukuliwa na kuingizwa katika mfumo wa Jeshi. Sasa kuna manung’uniko ya vijana kwamba wale vijana waliomaliza JKT awamu ya nne, hawajaajiriwa na hawanufaiki na utaratibu huo. Sasa hawa vijana wamefunzwa silaha, wakiachwa hivi hivi na manung’uniko mitaani, tunaweza tukaja kutengeneza kitu kingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii hata inanipa hofu kwamba kama tunafikiria hatuwezi kuwaajiri vijana wote, ni vizuri hawa vijana wa JKT pengine tukaangalia wale ambao wanafaa kuwapa mafunzo ya kijeshi na wale ambao pengine tunafikiria wataenda uraiani wapewe mafunzo ya aina nyingine. Vinginevyo kuwafundisha kijeshi na kuwaacha tu mtaani italeta athari kubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hawa tunaowachukua Jeshini ningeomba wafanyiwe psychometric test ili tuweze kupata Wanajeshi kweli ambao wanafaa. Kwa sababu zipo tetesi za baadhi ya Wanajeshi kufanya vitendo vya uhalifu mitaani. Kwa mfano, siku za karibuni Meya wa Ubungo alivamiwa na vijana waliovaa nguo za Jeshi. Sasa hatujui kwamba ni Wanajeshi, hatujui kwamba ni vijana waliomaliza JKT wako mtaani wakapata hizo nguo, hatujui kwamba ni Polisi walipata hizo nguo? Kwa hiyo, hili ni jambo la kuangalia sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kitu kingine ambacho napenda kukichangia ni kuhusu Kitengo cha Utafiti Ndani ya Jeshi. Ukiangalia sasa hivi, Maprofesa wetu wameamua kufanya siasa, wameamua kuingia kwenye utawala. Ukiangalia majeshi makubwa duniani hata Jeshi la Marekani, limeingia katika utafiti wa masuala mbalimbali ya kijamii kwa mafanikio makubwa kabisa. Kwa hiyo, naomba ajira za jeshi zihusishe pia vijana wataalam katika fani mbalimbali waingizwe katika tafiti za Jeshi lenyewe, lakini tafiti nyingine za kiraia ambazo zinaweza zikasaidia nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama tulivyosema, leo hapa tunajadili nchi, Jeshi letu ni nchi. Kwa hiyo, Jeshi letu lijipanue, lijihusishe katika mambo mengine ya kitafiti ambayo yanaweza yakaja yakawa na manufaa katika Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la tano ambalo ningependa kulisemea ni kuhusu madeni ya Jeshi. Jeshi kudai ni jambo la fedheha. Jeshi kudai kwa ajili ya kukarabati vifaa vyake ni fedheha. Jeshi kuomba omba kwa sababu ya vifaa, ni fedheha. Nadhani mahali ambapo tungekuwa na jeuri kabisa ya kufanya investment ya uhakika ni hapa. Kwa hiyo, namwomba Waziri wa Fedha, fedha zote zinazolihusu Jeshi letu zitolewe, tena kwa wakati kwa sababu zinahitajika kwa ajili ya ulinzi wetu. Tusiwe na blah blah na maneno maneno kuhusu pesa ambazo zinahusu wanajeshi; ziwe za pension, ziwe za vifaa, ziwe za nini, lazima Jeshi liwe na morali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukiwa na Jeshi lenye wanajeshi wanaonung’unika, hali yetu ni mbaya sana. Sasa hivi tumshukuru Mungu kwamba jeshi letu liko pamoja, hakuna manung’uniko na nini; lakini huku kuwanyima fedha kwa wakati, kunaweza kukaja kutuletea manung’uniko huko baadaye na itakuwa ni mbaya sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la mwisho ambalo napenda kuchangia ni kuhusu SUMAJKT. Mimi nimetoka ziara Kanda ya Ziwa kwa ajili ya kutembelea Sekondari ya Ihungo pamoja na Nyakato, zile zilizokumbwa na madhara ya tetemeko. Sasa Shule ya Ihungo mkandarasi aliyepewa kuijenga ni TBA na Nyakato ni SUMAJKT. Wanafanya vizuri sana chini ya Kanali Ngata. Kwa hiyo, hiki kitengo kiimarishwe, kinaweza kikatusaidia mambo mengi sana hapa nchini kuliko hata TBA. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana.