Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

Hon. Eng. Stella Martin Manyanya

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Nyasa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

NAIBU WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote napenda nianze kwa kumshukuru sana Mwenyezi Mungu, mwingi wa rehema kwa kutujalia afya na baraka tele zinazotuwezesha kutekeleza majukumu tuliyokasimiwa kwa maendeleo ya Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa namna ya pekee napenda kumshukuru sana Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa imani yake kwangu na kwa kuniteua kuwa Naibu Waziri wa Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji. Nathamini sana dhamana aliyonipa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, namshukuru pia Mheshimiwa Makamu wa Rais, Mama Samia Suluhu, Mheshimiwa Kassim Majaliwa Majaliwa, Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa mwongozo wao thabiti. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda pia kumshukuru Mheshimiwa Charles Mwijage, Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji kwa mwongozo na ushirikiano wake mkubwa unaoniwezesha kutekeleza vizuri majukumu niliyopewa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba uniruhusu pia kuishukuru sana familia yangu kwa sala na ushirikiano wao ambao ni Baraka na nguvu ya kipekee kwamba…

KUHUSU UTARATIBU . . .

NAIBU WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa hekima zako na ndiyo maana tulikuchagua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda pia kumshukuru tena, narudia, Mheshimiwa Charles Mwijage, Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji, kwa mwongozo na ushirikiano wake mkubwa unaoniwezesha kutekeleza vizuri majukumu niliyopewa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba uniruhusu kuishukuru sana familia yangu kwa sala na ushirikiano wao ambao ni baraka na nguvu ya kipekee kwangu katika kutekeleza majukumu haya mapya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nachukua pia fursa hii adhimu kuwashukuru sana wapiga kura wangu wote na wananchi wa Jimbo la Nyasa kwa kuendelea kuniamini na kunipa ushirikiano kama Mbunge wao.

KUHUSU UTARATIBU . . .

NAIBU WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi tumelelewa kwa nidhamu kwa upande wa kambi hii ndiyo maana Mwenyekiti akisema neno tunaheshimu. Kwa sababu maelekezo ya Kiti ndiyo ya mwisho. Naomba uheshimu Kiti. Wewe usiteseke, uendelee kuomba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, unapojenga hoja, kuna namna ya kuvuta pumzi. Mimi ni Yohana, ndiyo naanza utangulizi hapa, kwa hiyo, usiniletee vurugu. Ninachosema ni kwamba Tanzania sasa tunajenga viwanda, endelea kusikiliza hoja.

na kamanda wetu mkuu mnamfahamu, ni Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Kwa hiyo, namshukuru na tunashukuru kwa mwongozo anaoutoa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyosema, hoja zetu zitajibiwa zaidi kwa kadri tunavyoenda, lakini nikianzia na hoja ya tafsiri ya viwanda na suala hilo lilitolewa na Mheshimiwa Aida Joseph. Napenda niseme kwamba kiwanda ni eneo ambapo shughuli ya kiuchumi hufanyika ikihusisha uchakataji wa malighafi (value addition) kwa lengo la kuzalisha bidhaa ambazo hutumika moja kwa moja kwa mlaji au viwanda vingine. Hotuba ya bajeti ya mwaka 2018/2019 ukurasa wa tano, aya ya 15 mpaka 16 imeeleza hayo na imeainisha viwanda hivyo kwa kadiri ya ngazi zake na imefafanua kwa uwazi kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile nikiunganisha na suala ambalo lilijitokeza kwa upande wa hoja ya Mheshimiwa Cecil Mwambe, viwanda hivyo vinavyozungumzwa ni viwanda gani na ni vipi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, jana Mheshimiwa Waziri alipokuwa akitoa hotuba yake, alionesha kitabu ambacho tuliamua kwa makusudi kuorodhesha viwanda vyote. Hiyo ipo katika soft copy ambayo imekabidhiwa kwa ajili ya gharama, lakini pia muda, tumesema kitabu ni hiki. Kama kweli Mheshimiwa Cecil unatoka kwenu Ndanda na unawajua watu wako wote, njoo chukua kitabu hiki upitie, watu wa Ndanda utawaona wako humu, wale wote wenye viwanda vidogo sana, vidogo, vya kati na vikubwa kwa kadri ya utaratibu uliopo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuwafahamisha Waheshimiwa Wabunge kwamba viwanda ni sawa na binadamu, vinazaliwa, vinakua na vinakufa. Kwa hiyo, usishangae kuona kwa data hizi ambazo zilitengenezwa na kuhakikiwa na NBS toka mwaka 2014 na pia kuongezeka kwa idadi hii ambayo tunasema kufikia sasa, vingine vinaweza visiwe kwenye kazi kwa sababu hatufanyi uhakiki kila siku.

Mheshimiwa Mwenyekiti, namuomba nikimaliza, njoo uchukue, kama unawafahamu watu wako utawaona humu, mimi wa kwangu nimewaona. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, ni kuhusu kuwezesha taasisi za tafiti na teknolojia kuchochea maendeleo ya viwanda. Niseme tu kwamba ni kweli kuna umuhimu mkubwa sana wa kuziwezesha taasisi hizi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inatambua umuhimu wa taasisi hizi, hasa katika kufanya tafiti zinazolenga uongezaji thamani, ubora na kupunguza upotevu wa mazao na malighafi mbalimbali kwa kutumia teknolojia sahihi. Vilevile kupitia tafiti hizi, taasisi hizi zinaainisha maeneo ya uanzishwaji wa viwanda (industrial mapping) ili kuweza kutoa ushauri kwa Serikali na sekta binafsi, kuanzisha viwanda shindani na endelevu. Tafiti hizi zitawezesha kuwa na matumizi bora na yenye tija ya rasilimali zetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imekuwa ikitenga fedha kuziwezesha taasisi hizi. Kwa mfano tu, kumekuwepo na ongezeko la fedha za maendeleo zilizotolewa kutoka shilingi milioni 678.95 mwaka 2016/2017 hadi shilingi bilioni 7.511 mwaka 2017/2018 likiwa ni ongezeko la asilimia 1,006 ya fedha zilizotolewa na Serikali kwa taasisi hizi. Jitihada za Serikali za kuwezesha zaidi kifedha zitaendelea kutokana na umuhimu wa taasisi hizi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kuna suala lilikuwa limezungumzwa kuhusiana na Kiwanda cha Viuadudu. Kiwanda cha Viuadudu cha Kibaha kilianza uzalishaji wa kibiashara kuanzia tarehe 3 Februari, 2017. Kiwanda hiki kina uwezo wa kuzalisha lita milioni sita za viuadudu kwa mwaka. Hadi sasa kiwanda kimezalisha jumla ya lita 449,503 ambazo zimeuzwa ndani na nje ya nchi kama vile Niger na Angola. Ni kweli kabisa jumla ya Halmashauri 84 zilikuwa zimechukua dawa, yaani viuadudu katika kiwanda hiki na Halmashauri tisa ziliweza kulipa nyingine tunaendelea kuzihamasisha. Kiwanda hiki ni muhimu sana katika vita yakutokomeza ugonjwa wa malaria nchini na hasa katika hili eneo la malaria, tunamshukuru sana Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli ambaye alitoa fedha kwa ajili ya kupeleka kwenye Halmashauri ambazo zilikuwa zina maambukizi makubwa ya Malaria na fedha hizo zililipwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala kuhusiana na utekelezaji wa Mkataba wa C2C. Katika hotuba ya mwaka 2017/2018 tulieleza kwa kirefu mikakati tuliyoandaa kwa ajili ya uendelezaji viwanda ikiwepo ya sekta ya pamba hadi mavazi. Hotuba hii imejielekeza katika utekelezaji wa kipindi cha mwaka mmoja, mfano katika aya ya 50 inaeleza uanzishaji Kiwanda cha Vifaatiba vinavyotumia Pamba Simiyu, aya ya 52 inaeleza juu ya ufufuaji wa Morogoro Canvas Mill na vinu kumi vya kuchambua pamba. Aidha, aya ya 51, tumeeleza jinsi tunavyoshughulikia changamoto zinazokabili sekta ya pamba hadi mavazi, jambo ambalo limebainishwa kwenye Mkakati ya C2C. Mambo hayo yaliyotekelezwa ni sehemu ya utekelezaji wa Mkakati wa C2C.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kulijitokeza suala la ulipaji wa fidia kuhusiana na maeneo tunayotegemea ya uwekezaji, EPZA. Na mimi nikiwa natoka Mkoa wa Ruvuma, niseme tu kwamba ukienda katika kitabu cha randama kama unacho kaka yangu Mheshimiwa Dkt. Damas Ndumbaro, utakuta pale tayari kuna fedha zilizotengwa kwa ajili ya kulipa fidia. Kwa upande wa Ruvuma, Songea, nafahamu Mheshimiwa Waziri Mkuu tarehe 23 Desemba alikuwa pale na wananchi walilalamika sana juu ya suala hilo. Jumla ya shilingi 2,624,990,000 zimetengwa kwa ajili ya shughuli hiyo. Pia kuna maeneo ya mikoa mingine ambayo wanaweza wakapata taarifa hizo kupitia ukurasa huu wa 210.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie kuhusu Serikali kuiwezesha Tanrade, kuhakikisha kwamba bidhaa za Tanzania zinaingia katika masoko ya Kimataifa na kwamba Serikali iwezeshe TanTrade kuwekeza katika miundombinu ya masoko, maghala na viwanja vya maonesho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mwaka 2017/2018, Serikali ilitenga shilingi milioni 500 kwa ajili ya uendelezaji wa miundombinu ya Uwanja wa Maonesho ya Mwalimu Nyerere na kwa mwaka 2018/2019 TanTrade imetenga shilingi 2,376,400,000 katika bajeti ya maendeleo ikiwa ni ongezeko la shilingi 1,876,400,000. Ongezeko hili linatarajia kuongeza ufanisi katika utafutaji wa maeneo ya uwekezaji kwa ajili ya kujenga ofisi za kanda, viwanja vya maonesho, miundombinu ya masoko katika kanda mbalimbali nchini, kuongeza huduma karibu na wananchi na kuongeza tija katika biashara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kulijitokeza pia suala la Sheria ya FCC na hali halisi ya mazingira ya biashara. Sheria ya FCC inaonekana inakinzana na mazingira halisi ya kufanya biashara. Tulishauriwa kuhusu Serikali kuwa na teknolojia bora ya kutofautisha kati ya bidhaa bandia na bidhaa halisi na Sheria ya FCC ifanyiwe marekebisho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia FCC imekuwa ikifanya utambuzi wa baadhi ya bidhaa bandia kwa kutumia teknolojia miongoni mwa bidhaa ambazo utambuzi wake unatumia teknolojia.Ni bidhaa za kielektroniki na wino wa kurudia (catridge).Serikali inaendelea kushirikiana na wazalishaji wa bidhaa mbalimbali ili kupata teknolojia za utambuzi katika bidhaa wanazozalisha. Utambuzi wa bidhaa bandia hufanyika kwa kuzingatia Sheria ya Alama za Bidhaa ya mwaka 1963 kama ambavyo ilirekebishwa mwaka 2007 na 2012 na Kanuni zake za mwaka 2008.

Vilevile kwa kutumia TEHAMA pamoja na kushirikiana na taasisi za utafiti wa elimu ya juu kuimarisha usimamizi vitumike kuhawilisha (commercialization) matokeo ya tafiti kutoka vituo hivyo ili matokeo ya tafiti hizo yaweze kutumika kutengeneza mifumo, huduma na bidhaa hiyo kusaidia kukuza uchumi. Hiyo ipo katika hotuba ya mwaka 2018/2019 ukurasa wa 161 aya ya 327.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la kuuza ufuta kwa kutumia mfumo wa stakabadhi ghalani, maandalizi yameshafanyika ambapo kikao cha wataalam kimefanyika Mkoani Dar es Salaam tarehe 30 Aprili, 2018. Maandalizi ya kikao cha wadau yamekamilika ambapo kinatarajiwa kufanyika Mkoani Dodoma pia tarehe 15 hadi 16 Mei, ili kupata maoni ya mwisho kabla ya utekelezaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika suala la kulinda viwanda vya ndani, eneo hilo limechangiwa na Waheshimiwa Wabunge wengi na naomba radhi, sitaweza kuwataja wote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kimsingi Serikali inafanya juhudi kubwa katika kulinda viwanda vya ndani. Juhudi hizo ni pamoja na kuhakikisha kunakuwepo mazingira bora ya uzalishaji viwandani ikiwa ni pamoja na kupunguza gharama za uzalishaji, yaani andiko la blueprint limebainisha masuala yote ya kushughulikia, kuimarisha udhibiti wa bidhaa kutoka nje ya nchi na kuhakikisha kodi stahiki inalipwa na hivyo kutoa suluhisho la under-invoicing, under-declaration, tax evasion na pia masuala ya njia ya panya, kuongeza kodi kwa bidhaa kutoka nje ambazo viwanda vyetu vina uwezo wa kuzizalisha hapa nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na haya ambayo nimeyaeleza, niseme tu kwamba kuna mambo mengine ambayo yalijitokeza. Mfano, suala la lumbesa. Katika suala hili kumekuwa na manung’uniko mengi kutoka kwa baadhi ya Waheshimiwa Wabunge kukamatwa magunia yakiwa yamebeba viazi na bidhaa za aina hiyo. Tunachosema ni kwamba gunia linaweza likawa limewekwa lumbesa, liwe gunia dogo au kubwa, lakini tunachosisitiza ni umuhimu wa kuwa na mizani itakayopima kwa kilo. Ukishapima kwa kilo, ina maana kilo 50 itajulikana ni kilo 50. Kama utakuwa hauna mzani, kwa vyovyote vile itakuwa ni vigumu mtu kutambua kwamba hizi ni kilo 50 na hivyo kupelekea kuwaibia wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nitoe rai kwa Watanzania wote kuhakikisha kwamba wanapofanya shughuli zao zote za kibiashara za kuuza bidhaa zao, wahakikishe bidhaa zile ambazo zinahusika katika upimaji wa kilo, basi watumie kilo na siyo kutumia magunia pekee.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile kwa upande wa Wizara tunaangalia namna ya kufanya marekebisho ya sheria, hasa kuhusiana na suala la ujazo wa magunia yenyewe. Kama unavyofahamu, ni kwamba gunia la kilo 100 hata kulibeba bado linaweza lisilete afya kwa mbebaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa misingi hiyo, kwa kuzingatia kwamba tunaenda na viwango, tunasema kwamba tuwe na ujazo tofauti tofauti utakaowezesha hata wale ambao wanahusika katika shughuli za ubebaji mizigo, wafanye hivyo katika vipimo ambavyo ni sahihi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo, kulijitokeza pia suala la Mheshimiwa Mariam Kisangi kuomba juu ya watoto au akina mama kuweza kufanyia shughuli zao za kibiashara katika uwanja wa pale Sabasaba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kimsingi suala hilo baada ya kujadiliana, Mheshimiwa Waziri wangu kwa ridhaa yake, lakini pia taasisi ya TanTrade, tumeona ni jambo jema sana kwa sababu litawezesha akina mama hao katika hizo siku watakazoweza kwenda kufanya shughuli zao pale kwanza kupata mapumziko, lakini pia kuwa jirani na familia zao na kufanya biashara ndogo ndogo zitakazowawezesha wao kupata kipato zaidi. Kwa hiyo, utaratibu rasmi utawekwa ili kuwezesha namna bora zaidi ya kushughulikia jambo hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ni kuhusu ujenzi wa uchumi wa viwanda kwamba liendane na kutengeneza ujuzi. Ni kweli kabisa kwamba hilo ni suala muhimu sana. Serikali imekuwa ikifanya jitihada hizo katika kuhakikisha kwamba kupitia Wizara nyingine, kama ambavyo inaeleweka kwamba ujenzi wa uchumi wa viwanda siyo wa Wizara moja, ni wa Wizara mbalimbali; kupitia Wizara mbalimbali ikiwemo Wizara ya Elimu lakini pia TAMISEMI, kuhakikisha kwamba mafunzo ya aina mbalimbali yanatolewa, lakini hata Vyuo vyetu Vikuu vimekuwa pia vikitoa mafunzo ya ujasiriamali.

Vilevile kwa upande wa Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji tunacho Chuo cha Biashara (CBE) ambacho kinatoa mafunzo ya ujasiriamali, lakini pia mafunzo ya vipimo, hayo yote yanawezesha wananchi kufanya shughuli zao kiukamilifu lakini pia kufanya shughuli zao kwa tija. Kwa hiyo, mchango huo ni mzuri na tutaendelea kuufanyia kazi ili kuhakikisha kwamba wananchi wengi zaidi wanaelimika na kuweza kufanya shughuli zao inavyostahili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala la kwamba biashara nyingi kushindwa kufanya vizuri, ilizungumzwa kwamba kutolewe elimu siyo tu katika miji ni mpaka vijijini zitolewe elimu. Nakubaliana kabisa na suala hili, ni kwamba biashara ni sawa na binadamu, biashara zinaumwa kama binadamu, mtu anapokuwa hajui namna ya kufanya biashara inamfanya hata hiyo biashara ikianzishwa isiweze kuendelea. Kwa hiyo, Wizara yetu tumeona kwamba kuna kila sababu

ya kuanzisha vituo ambavyo vitasaidia katika kuwezesha kutoa tiba (business clinics) kwa ajili kusaidia viwanda hivyo vidogo vidogo, pia na biashara ndogo ndogo kusaidia katika kuleta uongozi wa masuala ya kiuwekezaji. Tupo katika mkakati huo na tutapokuwa tumekamilisha taratibu zetu basi tunaamini kwamba masuala hayo yatakuwa yamekaa vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya maneno hayo, kuna ambao walizungumzia ili tuweze kuwa na biashara vizuri au uwekezaji vizuri suala la amani ni suala muhimu sana, naunga mkono hoja hii ambayo ililetwa na Mheshimiwa Lwakatare, amani itaanzia humu Bungeni, mwenzako akiongea lazima umsikilize, uwe na uhimilivu, lakini kama hatutakuwa na amani ya kusikilizana hata kama kuna jambo la msingi mtu unakuwa kama tunafanya mchezo wakati watu tunakuwa tumefikiria tunafanya mambo ya msingi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo niwaombe sana Waheshimiwa Wabunge, kwa kuwa wote tuna dhamira moja ya kumuunga mkono Rais wetu kuhakikisha kwamba uchumi wa ujenzi huu wa viwanda unakua, basi tumuunge mkono kwa dhati na tuhakikishe kwamba tupitie vizuri vitabu hivi vilivyoandikwa na Wizara yetu ukurasa kwa ukurasa mtapata mambo mengi sana ambayo kwa hakika yatajenga na kuhakikisha kwamba tunajenga vizuri uchumi wetu, tusaidiane.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, naunga mkono hoja.