Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

Hon. Zuberi Mohamedi Kuchauka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Liwale

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nianze mchango wangu kwenye hoja hii na mazingira ya uwekezaji. Mazingira ya uwekezaji nchini bado siyo mazuri sana hasa kwa wawekezaji wadogo wadogo

au wazawa. Mazingira haya yanafanya gharama za uzalishaji wa bidhaa nchini kuwa juu kiasi cha kufanya bidhaa zinazozalishwa nchini kushindwa kumudu ushindani wa bidhaa zinazozalishwa nje ya nchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, utitiri wa mamlaka za usimamizi ni kikwazo kingine kwa wawekezaji wazawa, mfano bidhaa moja husimamiwa na mamlaka zaidi ya tano kama vile kiwanda kidogo cha kusindika nafaka husimamiwa na TBS, TFDA, OSHA, NEMC na kadhalika. Taasisi hizi zote zinatoza ada au ushuru.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kukosekana kwa kiwango maalum cha bidhaa (standard) kunafanya wazalishaji kukosa ushindani ulio sawa kwenye soko. Bidhaa ya aina moja huzalishwa katika ubora au standard tofauti, mfano hapa nchini hatuna kiwango au standard ya bidhaa za nafaka kama sembe na unga wa ngano hivyo washindani hushindania rangi ya sembe bila kujali ubora wake ambao unapaswa upimwe kwa extraction rate toka kwenye maghali ghafiki. Taasisi kama TBS na TFDA wana standard ambayo ndiyo ingekuwa mwongozo kwa wasindikaji wote wa nafaka hivyo kulinda upotevu wa nafaka unaotokana na wasindikaji kukosa standard badala yake wanashindania weupe wa sembe, mchele au ngano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, upatikanaji wa malighafi kwa viwanda vidogo ni tatizo lingine hasa kwa yale mazao yanayouzwa kwa njia ya mnada. Wawekezaji wadogo hushindwa kuingia mnadani kushindana na wafanyabiashara wakubwa, hivyo viwanda vidogo vidogo hukosa malighafi baada ya kushindwa kuingia mnadani. Mfano, vikundi vya ubanguaji wa korosho hukosa korosho baada ya akina mama hao kushindwa kuingia mnadani, hawaruhusiwi kununua korosho nje ya mnada.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivyo naishauri Serikali ione namna nzuri ya kuwawezesha wawekezaji hawa wadogo namna ya kupata malighafi ikiwezekana waruhusiwe kununua nje ya mnada.

Mheshimiwa Mwenyekiti, uwekezaji katika viwanda kwa kiasi kikubwa hutegemea mazao ya mashambani kilimo, wako wawekezaji wanaotaka kuwekeza kwenye kilimo kwanza ili kupata malighafi za viwandani na hatimaye waje kwenye viwanda vya kusindika mazao ya kilimo lakini upatikanaji wa ardhi ni mgumu sana, hasa kwenye vijiji ambavyo havijaingia kwenye mpango wa matumizi bora ya ardhi. Jambo hili limekuwa kikwazo kikubwa kwa wawekezaji wa upande wa kilimo hasa kwa mashamba makubwa, urasimu wa upatikanaji wa ardhi ni lazima ukaangaliwa upya ili uwekezaji katika kilimo uwe na tija.

Mheshimiwa Mwenyekiti, uwepo wa viwanda nchini kulitegemea kufungua ajira kwa wazawa, lakini kinyume chake ajira nyingi nchini huchukuliwa na wageni hasa kwenye viwanda vya watu binafsi. Wazawa wameendelea kuwa vibarua viwandani. Hakuna namba maalum ya ajira kwa wageni wakati katika nchi za wenzetu mwekezaji anaposaini mkataba wa uwekezaji hupewa idadi maalum ya wafanyakazi wa kigeni lakini hapa kwetu hakuna ufuatiliaji wa sheria hii. Mfano, Uganda mwekezaji wa kigeni huruhusiwa kuajiri wafanyakazi watano tu nje ya nchi yao ili kuwapa ajira wazawa na hao wachache waliopata ajira mishahara yao ni midogo sana na mazingira ya kazi (job security) ni ndogo sana, wazawa wananyanyaswa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika sekta ambazo zimesahauliwa katika uwekezaji nchini ni sekta ya kilimo. Pamoja na kuwa na ardhi kubwa yenye rutuba kwa mazao mengi, lakini sekta hii haijatangazwa kama ilivyo sekta nyingine. Wawekezaji wa kilimo cha biashara hapa nchini kinafanywa kwa kiwango kidogo sana. Mfano, hapa nchini viwanda vyote vya ngano vinaagiza ngano kutoka nje kwa asilimia mia moja, hakuna mashamba ya ngano nchini tangu kufa kwa mashamba ya NAFCO.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili tuende na kauli mbiu ya nchi ya viwanda basi ni vema tukaamua kuwekeza kwenye kilimo.