Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji

Hon. Mariamu Nassoro Kisangi

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji

MHE. MARIAM N. KISANGI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kunipa nafasi ya kuchangia katika Wizara hii ya Viwanda na Biashara. Kwanza nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuniwezesha siku hii ya leo kusimama hapa mbele na kuweza kuchangia katika Wizara hii. Pia niipongeze Serikali yangu ya Chama cha Mapinduzi kwa kazi kubwa wanayoifanya ya kuhakikisha kwamba tunapata Tanzania ya Viwanda. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimefurahia kuona hotuba ya Mheshimiwa Waziri inaeleza wazi kwamba nchi yetu imekuwa na jumla ya viwanda 53,876 lakini katika hivyo viwanda vikubwa ni 251, viwanda vya kati ni 173, viwanda vidogo 6,957 na vile viwanda vidogovidogo sana ni 46,495, sio kazi ndogo. Mara nyingi huwa tunatoa mfano kujenga nyumba ni kazi ngumu lakini kusema nyumba hii mbaya ni kazi rahisi sana, unatumia maneno sita tu. Leo hii Serikali hii ya Chama cha Mapinduzi imefanya kazi kubwa sana ya kuielekeza Tanzania yetu katika uchumi wa viwanda. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kusema peke yake hata kule kupiga debe ni kazi. Wananchi wa Tanzania sasa wameelekea katika kuileta Tanzania ya viwanda. Wawekezaji wote sasa wamebadilika na kutaka kuwekeza kwenye viwanda. Si jambo dogo lililofanywa na Serikali ya Chama cha Mapinduzi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda nimshukuru na nimpongeze Mheshimiwa Rais wetu, John Magufuli kwa kazi kubwa anayoifanya ya kuelezea na kutia nia yake ya dhati kabisa katika moyo wake kwamba anataka kuileta Tanzania katika uchumi wa viwanda. Lengo la viwanda si kwamba anavileta viwanda vile anataka kukuza ajira kwa vijana. Tumekuwa na vijana wetu wengi hawana ajira viwanda hivi vitakavyojengwa vijana wengi watapata ajira.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mambo mazuri yapo lakini changamoto kwa kila binadamu ipo na kwa jambo lolote utakalolifanya utakutana na vikwazo. Vikwazo hivyo vinaweza vikatatuliwa polepole lakini azma ya nchi yetu ni kuipata Tanzania ya viwanda. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kuipongeza Serikali yangu ya Chama cha Mapinduzi kwa kazi kubwa inayoifanya sasa naomba nirudi katika mchango wangu na nitachangia kuhusu leseni za biashara. Nimeona wazi kuna eneo wamesema wameweza kutoza faini za kukiuka sheria za biashara takribani shilingi bilioni 9.7. Kitendo hiki cha watu kukiuka kukata leseni na kuingiza pesa kiasi hiki tunaweza kuona ni kizuri lakini ndani yake kuna ubaya, lazima tujiulize kwa nini wananchi wanakiuka?

Mheshimiwa Mwenyekiti, masuala ya leseni na hasa katika Jiji langu la Dar es Salaam imekuwa mtihani. Mama lishe akikaa barabarani hana leseni, mama lishe akijiongeza akasema nikachukue tu kakibanda kadogo niweke hapa sufuria yangu ya wali, vikombe vyangu na meza yangu moja imekuwa shida katika Mkoa wa Dar es Salaam. Mama lishe huyo ataambiwa aende kwanza Manispaa kuomba leseni, ataambiwa nenda TRA ukapate clearance, ukifika TRA hakuachi hivihivi akakupa ile clearance tax clearance ya hivihivi kwamba unakwenda kwanza biashara lazima uanze kulipia si chini ya Sh.300,000. Unawenda halmashauri wanakwambia ulipe leseni hiyohiyo Sh.100,000, unarudi Sh.500,000 imeshaondoka mama lishe huyu biashara hajaanza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, akija kuanza biashara miezi mitatu anaambiwa ulipe kodi. Hivi huyu anayejitahidi kuboresha mazingira yake ndiyo sisi tunamuumiza kuliko yule aliyekaa pale anauza bila ya kitu chochote wala usafi. Nakuomba sana Mheshimiwa Waziri uliangalie hili akina mama wa Dar es Salaam kweli wanaendesha kwa kutumia biashara ndogondogo. Sisi katika Mkoa wetu wa Dar es Salaam hatuna mashamba ya kulima kwamba tunaweza kupitisha mazao yetu kwenye ki-carry kidogokidogo kukwepa kodi, sisi tunayo biashara. Biashara zetu ndiyo hizi akina mama kukaanga mihogo, kuuza ice cream lakini yule anayepata mtaji kidogo anahamisha mtaji wake, anauboresha, anaangalia ananunua viti vyake vya plastic sita, anaweka, anafanya biashara. Niiombe Serikali iangalie biashara za namna hii, waangalie jinsi gani watawaelekeza akina mama hawa waweze kulipa leseni vizuri si kwa uonevu, wala kukandamizwa na kodi lakini pia waweze na wao wenyewe kujiendesha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nije TBS. TBS si rafiki wa mfanyabiashara mdogo ni rafiki wa mfanyabiashara mkubwa. Nasema hivyo kwa sababu akina mama wa mkoa wangu wanatengeneza bidhaa mbalimbali zikiwemo sabuni, mafuta ya nazi, majani, mdalasini, wanajitahidi kwa kadri ya uwezo wao lakini wanavyokwenda TBS hawapati ushirikiano wa kuangalia ule ubora wa zile biashara zao hali ambayo inawafanya akina mama hao wakate tamaa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nimefuatwa na mabinti, nina deni la kulipa hapa Kinondoni, vijana wa filamu badala ya kuonyesha filamu wamejiongeza wakasema wao wawe wajasiriamali, wanatengeneza vitu vyao lakini TBS haiwapi ushirikiano kabisa. Nawaona wanatenga fedha za semina, semina hizo mnawapa akina nani wakati akina mama bado wanahangaika? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sasa nichangie eneo la TANTRADE ambayo sisi tunaita Sabasaba. Niwapongeze sana hawa TANTRADE wanawezesha kuonyesha maonesho mazuri, watu wanajaa, wanapata fedha, lakini sisi kama akina mama wa Dar es Salaam tunafaidika na nini wakati hatuna hata banda?

Mheshimiwa Mwenyekiti, sikatai kabisa na niwapongeze wanachukua akina mama Tanzania nzima. Sisi Dar es Salaam hatuna mgodi, ardhi ile ndiyo rasilimali iliyoko kwetu na uwanja ule ndiyo tunautegemea angalau na sisi Serikali ituwezeshe kupitia Uwanja ule wa Sabasaba. Leo hii akina mama wa Dar es Salaam wanahenyahenya tu mitaani inafika Sabasaba anaingia kwa tiketi anaenda kuangalia kazi za wenzie yeye kazi yake haipo. Niiombe Serikali, nikuombe Mheshimiwa Waziri utakaposimama unieleze kwamba Mkoa wa Dar es Salaam mwaka huu TANTRADE wako tayari kuwatengea banda angalau tent tu pembezoni na wao waweze kuonyesha bidhaa zao ili na sisi tuweze kufaidika? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kuna suala lingine kuhusu watoto. Watoto wa Temeke hawana sehemu ya kuchezea. Inapofika Sikukuu ya Iddi na Christmas wanazagaazagaa maeneo yale ya Uwanja wa Sabasaba, hawana pa kuchezea. Hivi Serikali inashindwa nini kuwafungulia watoto wale kucheza mle ndani ya uwanja siku ya Sikukuu ya Iddi na Christmas angalau na wao wafaidike na mradi ule wa Serikali yao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyeki, lakini pia katika kuingiza watoto wale wakiletwa wajasiriamali wakaleta bembea na michezo mbalimbali ya kitoto, itaisaidia Serikali pia kuingiza mapato. Kwa hiyo, niiombe Serikali yangu wafanye jitihada ili watoto wetu nao wakafurahie uwanja ule. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sasa nichangie kuhusu masoko. Ni ukweli kabisa kuna tatizo kubwa la masoko. Pamoja na kuhangaika kote na viwanda, bado bidhaa zetu zinakosa masoko. Mimi nashindwa kuelewa, bidhaa za Watanzania tunafika sehemu tunahamasisha lakini baada ya kutengeneza kile kitu unakuta gharama yake imekuwa kubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja kwa kumpongeza Waziri na Watendaji wote wa Wizara hii. Kazeni mwendo, mwendo huo huo, Mwenyezi Mungu atawasaidia.