Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji

Hon. Jitu Vrajlal Soni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Babati Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji

MHE. JITU V. SONI: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kupata nafasi siku ya leo kuchangia. Awali ya yote, naomba kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa afya na kunijalia kufika hapa leo.

Mheshimiwa Spika, nichukue fursa hii kwanza kumshukuru Mheshimiwa John Pombe Magufuli, Rais wetu kwa kazi nzuri na kubwa anayoifanya pamoja na watendaji wake wote. Muhimu ni kuelewa dhana nzima na mahali ambapo wanataka nchi yetu ielekee. Mimi nashukuru kwa hii dhana nzima ya kuwa na Sera ya Viwanda ambapo naamini kabisa tukienda vizuri na wote tukachangia vizuri na kila mmoja akaweka mawazo yake pale na tukaangalia changamoto zilizopo na namna ya kukabiliana nazo, mafanikio yapo na uchumi wetu utaendelea kukua.

Mheshimiwa Spika, sasa hivi uchumi wetu ni mzuri na unaendelea kukua, kuna changamoto ndogo ndogo ambazo naamini Wizara ya Viwanda na Biashara chini ya Mheshimiwa Mwijage na Naibu Waziri pamoja na timu nzima ikiongozwa na Katibu Mkuu na wote wanafanya kazi nzuri na kubwa. Changamoto bado zipo na tunahitaji kuwapa msaada, kuwapa mawazo mbadala na maeneo ambayo wanafanya vizuri tuwapongeze lakini maeneo ambayo wanatakiwa kuyafanyia kazi wafanyie kazi.

Mheshimiwa Spika, jambo la muhimu ni kuangalia namna ya kuunganisha Serikali yaani coordination bado haipo. Waziri unafanya kazi peke yako na kila Wizara inajitegemea. Mngefanya kazi kwa kuunganisha Wizara zote ili tupate mafanikio makubwa. Tanzania bado easy of doing business haipo. Bado kuna ukiritimba mkubwa na ukiangalia kila mmoja anajitahidi kuhakikisha kwamba anafanikiwa.

Mheshimiwa Spika, muhimu ni kuangalia namna ya kulinda viwanda vya ndani. Namna ya kulinda viwanda vya ndani ni lazima muwekeze kufanya utafiti wa uhakika kuhakikisha kwamba bei ya uzalishaji wa viwanda vyetu vya ndani inakuwa ndogo ili isishindane na bidhaa zinazotoka nje, hilo ndilo jambo kubwa kuliko yote. Leo hii wote wanaowekeza kwenye viwanda gharama yao ikiwa ni kubwa kuliko zile bidhaa zinazotoka nje watashindwa kufanya kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sisi watu binafsi tukifanya utafiti tunakuta bado tuna changamoto kwenye regulatory bodies zetu. Tunaendelea kushauri mziunganishe, ziwe moja na watu wasiwe analipa kwenye hizi regulatory bodies, ingekuwa ukishalipa kwenye leseni ya biashara basi huko huko kila kitu kiwe kimelipiwa ili tusipate usumbufu. Wanapokuja kukagua wakague wakati wowote lakini wasisumbuliwe kwa maana kwamba kila mmoja anataka alipwe tozo yake.

Mheshimiwa Spika, jambo lingine muhimu ni kuwekeza kwenye utafiti. Kwa sababu bila kufanya utafiti wa uhakika, kwenye TIRDO, SIDO na COSTECH ipatiwe fedha bado suala hili la namna ya sisi kuendelea itakuwa ni ngumu. Kwa mfano, ukiangalia viwanda vya ndani bei ya kuzalisha sukari, mafuta lakini pia bidhaa zote zinazoweza kuzalishwa ndani ya nchi, leo tuangalie kwenye pamba (Cotton to Clothing) ni ngumu. Kamati yetu ilitembelea kule MWATEX na viwanda vingine, bado unakuta gharama zao ni kubwa sana ukilinganisha na bidhaa inayotoka nje. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa usiangalie tu pale kwenye kiwanda anaajiri watu wangapi na analipa nini, angalia spillover effect kwamba kuanzia mkulima mpaka hapo inapofika kwenye kiwanda na bado ile nguo itakayozalishwa wale washonaji na wengine ni kiasi gani itaweza kuzalisha. Bei ya bidhaa inayotoka nje Serikali ilituahidi kwamba nchi ambazo tunaagiza kutoka kwao kwa wingi mtaangalia bei zao, wengi wana-under declare. Wakisha-under declare kwa mfano kwenye hii Cotton to Clothing mtu wa ndani hawezi kushindana na huyu wa nje.

Mheshimiwa Spika, ni vizuri tukapata uhakika wa bei ya uzalishaji na ni vizuri mkakaa na wafanyabiashara wakawaeleza bei ya uzalishaji wa viwanda vya ndani. Sehemu nyingine, kwa mfano, kwenye pombe kali, ni mahali ambapo Serikali inapoteza pesa nyingi sana kwa sababu gharama yake ya uzalishaji haijulikani. Wengine wanauza kwa bei ya kodi tu, sasa ile pombe anauzaje? Ina maana kuna mahali ambapo tunapoteza mapato mengi ni vizuri kuangalia. Pia tukiangalia viwanda vyetu kwa mfano vya mbolea, yeye kwa upande wa kodi anatozwa kodi zote hawezi ku-claim kwa sababu end product yake bado haina VAT lakini ile inayotoka nje haitozwi, unakuta gharama yake ya uzalishaji inakuwa kubwa hawezi kushindana na ile mbolea ambayo imetoka nje.

Mheshimiwa Spika, kwa sababu ni viwanda na biashara mngeangalia pia kwa nini informal sector inazidi kukua? Leo hii asilimia 80 ya watu wako kwenye informal sector (sekta isiyokuwa rasmi), ni kutokana na hizi tozo, kodi na ushuru mbalimbali ambapo mtu anaona ni kero anaona ni bora aendelee kuwa informal na maisha yanaenda. Kama tuki-formalize na tukiangalia namna ya kwenda haraka Serikali itapata mapato mengi zaidi kwa sababu tax base yetu tukiitanua nina uhakika kabisa kwamba unaweza ukapunguza hizo kodi nyingine ili wengi walipe kodi ziteremke na compliance itakuwa ni kubwa. Kwa hiyo, hilo ni jambo muhimu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kama mngekuwa mnafanya kazi na viwanda vingine, niwape mfano, Manyara tuna Kiwanda cha Kuchambua Pamba, ambapo kwenye sekta nzima ya kilimo wanatumia umeme kwa muda mdogo, ni viwanda kabisa vikubwa vinatumia kwa muda wa mwezi au miezi miwili halafu wanafunga mpaka msimu ujao. Unakuta wanalipishwa capacity charges ya miezi mitatu asilimia 70 ya ile gharama, cost of production lazima iwe juu. Kwa mwendo huo viwanda vingi vitaendelea kufungwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini tukija kwenye maziwa na viwanda karibu vyote msipoangalia, msipokaa na Wizara nyingine ambazo zote ziko kwenye sekta hiyo ya viwanda, kuanzia production mpaka wakati wa kuuza, bado hamtakuwa mmevilinda viwanda vya ndani. Ni muhimu kuangalia namna ya kupata cost of production, faida na kodi. Ni muhimu Serikali iendelee kupata kodi yake sahihi maana isipopata kodi yake sahihi hizi ndoto zetu za kuwekeza kwenye huduma nyingine hatutafanikiwa.

Mheshimiwa Spika, pia tuangalie viwanda ambavyo vitalenga wakulima, wafugaji, wavuvi, vitu wanavyozalisha vinawezekana kupatikana ndani ya nchi. Kwa nini tunaendelea kuagiza vitu vyote kutoka nje? Bahati nzuri Mheshimiwa Rais pia amelizungumzia mara nyingi, tunaomba sasa muendelee kushirikiana kama Serikali moja, kuwe na uratibu baina ya Wizara zote ili ndoto yetu iweze kutimia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia kuna jambo lingine ambalo ni muhimu tujue kwamba viwanda haviwezi kujitegemea bila kujua raw material yatakuwa yanatoka wapi. Kwa nchi yetu raw material kwa sehemu kubwa ni sekta ya kilimo, mifugo na uvuvi. Tukiwekeza kwenye hizo sehemu tatu na mkaweka mkakati kwamba mwaka huu tunafanya kwenye product mbili au tatu, tukawekeza value chain nzima, yaani mnyororo wa thamani kutokea kwenye uzalishaji, viwandani mpaka kwenye kuuza, nina uhakika kabisa kwamba ndani ya miaka miwili, mitatu, tutaona mabadiliko makubwa.

Mheshimiwa Spika, ni aibu kwa nchi yetu kuagiza bidhaa ambazo tungeweza kuzalisha ndani ya nchi hii. Mifano ipo mingi, kwanza tuangalie kwenye matunda na mbogamboga, samaki, vitu vyote hivi tunaweza kuzalisha ndani ya nchi. Ni vizuri kama Serikali kwa pamoja tuwekeze kwa ajili ya upatikanaji wa bidhaa hizo. Juice zote tunazokunywa hakuna hata tone moja linalozalishwa hapa nchini zote ni concentrates kutoka nje.

Mheshimiwa Spika, hata kwenye biashara, kwa mfano kwenye pombe kali, bei ya kodi baina ya pombe inayozalishwa ndani ya nchi na nje ya nchi ni ndogo, hivyo hivyo kwenye juice. Sasa tuangalie, inayozalishwa ndani ya nchi ama tufute kabisa au ipungue kabisa lakini ile inayotoka nje tuipandishe ili watu wawe na incentive ya kuwekeza hapa nchini, waone kwamba ni bora kuwekeza hapa nchini kuliko kuagiza kutoka nje.

Mheshimiwa Spika, nchi nyingine bado zina mamlaka ya kusamehe kodi kwenye bidhaa zao za export lakini sisi hatuna. Kama Kenya au Zambia wanazalisha wao wanapewa kuingiza nchini bila kodi unakuta bidhaa zao ndio ziko kwenye soko letu badala ya sisi bidhaa zetu kuingia sokoni, kwa sababu sisi hatuna msahama wa aina yoyote. Nchi za SADC tayari tuna ile SADC Protocol ambapo bidhaa zao zinapouzwa kwenye nchi hizi kodi yake ni ndogo, kwa hiyo, ushindani unakuwa mdogo.

Mheshimiwa Spika, ni vizuri kama Serikali muangalie mambo haya na Wizara hii ya Viwanda na Biashara ndiyo mnatakiwa kufanya utafiti wa uhakika, mshauri Wizara nyingine zote kwa pamoja mfanye nini. Pia tuhakikishe kuna miundombinu muhimu kama barabara na umeme kwa wale wanaohitaji kuwekeza kwenye viwanda. Vilevile tuwaondolee changamoto nyingine, kwa mfano, watu wanaanzisha viwanda halafu unasema barabara hii mwisho tani kumi hatuwezi kufika. Ni muhimu Wizara hii iendelee kushauriana na wengine.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja.