Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji

Hon. Shamsia Aziz Mtamba

Sex

Female

Party

CUF

Constituent

Mtwara Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji

MHE. SHAMSIA A. MTAMBA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipatia nafasi ili na mimi niweze kuchangia katika Wizara hii ya Viwanda na Biashara. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, awali ya yote, napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunijaalia afya nzuri na leo hii kuweza kusimama katika Bunge hili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, napenda kutoa pongezi za dhati kabisa kwa Mwenyekiti wangu wa Chama-Taifa, full bright, Profesa Ibrahim Lipumba kwa kazi kubwa ambayo anaifanya ya ujenzi wa Chama changu. Pia napenda kutoa pongezi za dhati kabisa kwa Naibu Katibu Mkuu, Mheshimiwa Magdalena Sakaya kwa kazi kubwa ambayo anaifanya ya ujenzi wa Chama changu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba niingie katika mada. Wakati Tanzania tunaelekea katika uchumi wa viwanda, ni lazima tuwe na umeme wa uhakika na hakuna mwekezaji atakayekubali kujenga kiwanda ili apate hasara kwa sababu umeme unapokosekana kwa saa nne tu ni hasara kubwa kwa mwekezaji. Kwa mfano, itabidi apunguze wafanyakazi lakini pia wafanyakazi wataliobaki wanahitaji mishahara. Pia uzalishaji utakuwa chini ya kiwango, kwa mfano, kiwanda kilichopo kule kwetu Mtwara, Kiwanda cha Saruji cha Dangote kama kilikuwa kinazalisha kwa siku tani 100, umeme unapokatika uzalishaji utapungua, kiwanda kitazalisha tani 60 badala ya tani 100. Hii ni hasara kubwa kwa Taifa na mwekezaji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nije katika masuala ya ajira. Umeme unapokuwa wa mgao au unapokatika mwekezaji itabidi apunguze wafanyakazi. Akifanya hivyo atakuwa amepunguza ajira na familia nyingi zitaishi maisha ya dhiki kwa kuwa kipato cha familia kitakuwa kimepungua.

Mheshimiwa Spika, vijana wengi sasa wameamua kujiajiri kwenye viwanda vidogo vidogo kama viwanda vya kuchomelea (welding), viwanda vya kuwekea samaki, viwanda vya kutengeneza barafu, viwanda vya salon za kike na za kiume, vyote vitakuwa hazifanyikazi kwa kukosa umeme wa uhakika. Hii ni hasara kubwa kwa Taifa.(Makofi)

Mheshimiwa Spika, nije upande wa kodi za Serikali. Uzalishaji wa viwandani ukipungua hata kodi za Serikali nazo zitapungua. Serikali itashindwa kutimiza majukumu yake ya kupeleka miradi ya maendeleo kwa wananchi wake. Ushauri wangu kwa Serikali iwekeze nguvu kubwa katika uzalishaji wa gesi iliyoko kule Msimbati, gesi ya Mnazi Bay ili iweze kutimiza majukumu yake ya kusambaza umeme wa majumbani na viwandani.

Mheshimiwa Spika, niongelee masuala ya kibiashara. Akina mama wengi tumepata mwamko wa kufanya biashara lakini kikwazo kikubwa tunachokumbana nacho ni kodi kubwa tunazotozwa na Maafisa wa TRA, tunafanyiwa makadirio makubwa mno. Naiomba Serikali yetu Tukufu ya Mheshimiwa Rais John Pombe Magufuli itupunguzie kodi hizi kwa sisi wajasiriamali, kama maduka ya nguo, vifaa vya ujenzi, mahoteli, biashara ya magari ya abiria yaendayo mikoani na daladala. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipatia nafasi.