Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi kwa mwaka wa fedha 2016/2017.

Hon. Shabani Omari Shekilindi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Lushoto

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi kwa mwaka wa fedha 2016/2017.

MHE. SHAABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri wa Kilimo, Mifugo na Uvuvi, toka mwaka 2014/2015, 2015/2016 pesa za maendeleo hazijafika katika Halmashauri ya Wilaya ya Lushoto. Kwa hiyo, naishauri Serikali yangu ipeleke pesa hizi kwa wakati. Pesa hizi kwa kutofika imedumaza kabisa Sekta ya Kilimo pamoja na wakulima kutopata huduma hii muhimu ukizingatia 70% ya wananchi wa Tanzania ni wakulima.
Mheshimiwa Naibu Spika, upungufu wa wataalam; katika Halmashauri ya Wilaya ya Lushoto kuna wataalam 35 tu ambao wanahudumia vijiji 125. Hii inapelekea kila mtaalam kuhudumia wakulima 3,000 kitu ambacho ni vigumu kumfikia kila mkulima. Kwa hiyo, kuna upungufu wa wataalam 55 – 60. Niombe Serikali ipeleke wataalam hawa ili kuwanusuru wakulima wetu hawa. Kwa kuwa Serikali hii ni sikivu na ina mpango mzuri wa kumuinua mkulima wa Tanzania, ni imani yangu wataalam hao watafika kwa wakati.
Mheshimiwa Naibu Spika, suala la ruzuku na pembejeo katika nchi hii bado ni tatizo kwani hazifiki kwa wakati pia mara kwa mara hazimlengi mkulima aliyekusudiwa kwani kuna udanganyifu mkubwa unafanyika. Katika Halmashauri ya Wilaya ya Lushoto pembejeo hizi zinatolewa kwenye mazao ya nafaka tu yaani mahindi na mpunga. Niombe wakulima wa mbogamboga na matunda nao wafikiriwe. Kama inavyojulikana Lushoto ni ya wakulima wa mbogamboga na matunda, Serikali isiposaidia wakulima hawa itakuwa haijasaidia wakulima wa Lushoto.
Mheshimiwa Naibu Spika, miche bora ya kahawa. Kahawa iliyopo Wilaya ya Lushoto ni ya zamani mpaka imepelekea zao hilo kupotea. Hivyo, niombe Serikali ipeleke miche bora na ya kisasa ili kufufua zao hili ambalo ndiyo tegemeo kubwa la wana Lushoto.
Mheshimiwa Naibu Spika, naiomba Serikali yako iwatafutie masoko wakulima wa Lushoto hapa nchini na nje ya nchi. Pia Serikali itoe ushuru kwenye mazao haya ya mbogamboga na matunda kwani unawakatisha tamaa wakulima wetu hao. Pamoja na hayo, nimshukuru Waziri wa Kilimo katika hotuba yake iliyoelezea kutoa ushuru kwenye vizuizi na hatimaye ushuru ukachukuliwe sokoni.
Mheshimiwa Naibu Spika, zao la nyanya limepungua sana katika Halmashauri ya Lushoto kwa kuwa kumezuka ugonjwa unaitwa Kantangaze. Ugonjwa huu umeathiri zao zima la nyanya na ugonjwa huu dawa yake inauzwa ghali mno. Kipimo cha dawa hii miligramu nne inauzwa sh. 4,500 ambayo ni bomba la nyanya lenye kuingia lita 15 wakati huo shamba la nyanya linaingia bomba 20 hadi 25. Kwa hiyo, mkulima wa kawaida hawezi kumudu gharama hizo. Niombe Serikali iwaangalie wakulima hawa kwa jicho la huruma ili mkulima yule wa hali ya chini aweze kumudu kununua dawa hiyo.
Mheshimiwa Naibu Spika, unaposema kilimo ni uti wa mgongo kinaenda sambamba na miundombinu ya barabara hasa za vijijini. Naomba Serikali yangu iangalie hilo nalo.