Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maji na Umwagiliaji kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

Hon. Zuberi Mohamedi Kuchauka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Liwale

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maji na Umwagiliaji kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuanza mchango wangu kwenye Wizara hii kwa kuangalia Tume ya Umwagiliaji kwani ufanisi wa Tume hii ni wa kutiliwa mashaka. Miradi mingi ya umwagiliaji inayosimamiwa na Tume hii ukamilifu wake si wa kuridhisha na miradi mingi imehujumiwa sana kutokana na usanifu wa miradi hiyo kutokuwa wa kuridhisha.

Mheshimiwa Naibu Spika, mfano mradi wa Ngongowele, Wilayani Liwale uliosanifiwa na Tume hiyo Kanda ya Kusini, mradi huu umehujumiwa sana hadi leo mradi huu umekwama sana. Hata hivyo, watu wa Japan wameonesha nia ya kuleta fedha ili kufufua mradi huu lakini tayari watu hao wa Kanda wameanza kutia mikono yao ili kuendelea kuhujumu mradi huu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu maji mijini, pamoja na takwimu kuonesha hali ya upatikanaji wa maji mijini ni ya kuridhisha, je, Wizara ina uhakika maji haya yanawafikia wananchi kwani kiwango cha maji kinachopotea njiani ni kikubwa sana. Mfano katika Jiji la Dar es Salaam maji mengi hupotea barabarani kabla ya kuwafikia wananchi kutokana na ubovu wa miundombinu ya maji hasa kupasuka kwa mabomba kunakosababishwa na ukarabati wa barabara na ujenzi holela wa miundombinu ya maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu kumtua mama ndoo, pamoja na nia nzuri ya sera hii lakini utekelezwaji wake si mzuri kwani miradi mingi inashindwa kukamilika kutokana na ukosefu wa fedha na utendaji usioridhisha kutokana na watendaji wengi kwenye Halmashauri zetu kushindwa kuelewa miongozo ya Wizara hii. Mfano pale Waziri anaposema wahandisi watangaze kazi kabla ya kupewa fedha jambo ambalo halitekelezeki na linawachanganya wahandisi wengi wa Wilaya juu ya utekelezaji wake. Ni bora Serikali ikawa wazi juu ya jambo hili kwani miradi mingi vijijini imekwama.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kushindwa kupeleka fedha za miradi ya maji ni kwenda kinyume na sera hii ya kumtua mama ndoo kichwani. Vilevile gharama za maji vijijini ni ghali pengine kuzidi hata gharama za maji mijini, jambo hili limefanya miradi mingi iliyokamilika kushindwa kujiendesha kwa kukosa fedha za kununua dizeli za kuendeshea mitambo ya maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika Halmashauri ya Wilaya ya Liwale ilikuwa na miradi ya kutafuta chanzo cha maji kwa ajili ya Mji wa Liwale baada ya chanzo chake cha mwanzo cha Mto Liwale kushindwa kukidhi mahitaji. Sasa ni miaka minne mradi huu umesimama huku fedha za mradi huu zikiendelea kuliwa bila chanzo hicho kupatikana. Mji wa Liwale unakua kwa kasi na unakabiliwa na uhaba mkubwa wa maji. Vilevile maji yanayopatikana hayana ubora kwani hayawekwi dawa kwa kuwa hawana dawa wala matanki ya kufanyiwa treatment ya maji, hivyo hulazimika kuyaleta kama yalivyotoka mtoni.

Mheshimiwa Naibu Spika, hakuna uhusiano wa moja kwa moja kati ya takwimu tunazopewa na Mheshimiwa Waziri na uhalisia wake kwani hali ya upatikanaji wa maji nchini ni mbaya ukilinganisha na maelezo ya Mheshimiwa Waziri. Hakuna mji wala kijiji kilicho na utoshelevu wa maji. Hata pale yanapopatikana basi upatikanaji wake ni ghali sana hasa vijijini. Ushauri wangu, ni vyema sasa watendaji walete takwimu sahihi ili sisi Wabunge tuweze kushauri vizuri Serikali ili kutatua tatizo hili sugu la maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la kuongeza fedha kwenye Mfuko wa Maji ni bora sasa likatekelezwa ili kuiongezea fedha Wizara hii. Ongezeko kutoka shilingi 50 kufikia shilingi 100 kwani tatizo kubwa la Wizara ni fedha kwa ajili ya miradi yake