Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maji na Umwagiliaji kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

Hon. Oran Manase Njeza

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbeya Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maji na Umwagiliaji kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kumpongeza Mheshimiwa Engineer Isack A. Kamwelwe (Mbunge), Waziri wa Maji na Umwagiliaji na Mheshimiwa Jumaa Aweso (Mbunge), Naibu Waziri wa Maji na Umwagiliaji, Profesa Kitila Mkumbo, Katibu Mkuu pamoja na wataalam wote wa Wizara ya Maji na Umwagiliaji kwa kazi nzuri waliofanya katika kipindi cha mwaka 2017/2018. Mpaka Machi, 2018 utekelezaji wa Wizara ni zaidi ya asilimia 56 ambayo ni zaidi ya mara mbili ukilinganisha na asilimia 25 ya mwaka 2016/2017.

Mheshimiwa Naibu Spika, kipekee naomba kumpongeza Mheshimiwa Waziri na Naibu Waziri kwa ziara wanazozifanya nchi nzima, zimeleta tija kubwa katika utekelezaji wa miradi. Katika ziara ya Naibu Waziri Mheshimiwa Aweso, alibaini mapungufu makubwa ya mradi ya maji katika Halmashauri ya Wilaya ya Mbeya. Mheshimiwa Aweso alipokagua mradi wa maji wa vijiji vya Horongo, Itimu na Mwampalala alijionea udanganyifu mkubwa wa mradi kutekelezwa chini ya kiwango na hata pale alipoambiwa mradi unatoa maji aligundua hata matenki hayakuwa na maji. Pia Mheshimiwa Kamwelwe alishuhudia utekelezaji wa asilimia mbili tu ya bajeti ya mwaka 2016/2017 huku taarifa zikipotosha kuwa miradi imekamilika na kulikuwepo madai ya wakandarasi wakati siyo kweli.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya ziara ya Waziri wa Maji aliagiza miradi yote iliyokuwa imekwama kwa zaidi ya miaka saba isimamiwe na Wizara ya Maji kupitia kwa Mkurugenzi wa Mamlaka ya Maji Mbeya, uamuzi huo umeleta matunda na miradi ifuatayo iko katika hatua nzuri sana za utekelezaji, mradi wa kijiji cha Ganjembe umekamilika asilimia
90. Mradi wa vijiji vya Swaya na Lupeta umekamilika kwa zaidi ya asilimia 80. Mradi wa Mbawi na Jojo umekamilika kwa asilimia zaidi ya 90.

Mheshimiwa Naibu Spika, mradi wa vijiji vya Idimi na Haporoto umekamilika kwa zaidi ya asilimia 60. Mradi wa vijiji vya Mshewe, Muvwa, Njelenje, Mapogoro na Njele bado upo kwenye hatua za mwanzo. Mradi wa kijiji cha Ilota upo kwenye hatua za mwanzo na napenda kuwashukuru Tulia Trust kuahidi kuchangia shilingi milioni 250. Mamlaka ya Maji ya Mji Mdogo wa Mbalizi imekubalika kuunganishwa na Mamlaka ya Maji Mbeya ili kuboresha huduma ya maji kwa Mji wa Mbalizi.

Mheshimiwa Naibu Spika, mradi wa maji wa Izumbwe, Iwindi na Mwashiwawala umekamilika kwa zaidi ya asilimia 50. Mradi wa skimu ya umwagiliaji kwa kijiji cha Mashewe umekamilka kwa zaidi ya asilimia 90.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na hatua nzuri ya miradi hapo juu bado kuna mahitaji makubwa ya maji kwa maeneo mengi ya Wilaya ya Mbeya hasa kwenye miji midogo ya Ilembo, Inyala, Isuto, Santilya, Iwigi, Ikhoho, Mjele. Kunahitajika maji kwenye vituo vya afya, zahanati na mashule karibu yote hayana maji. Nashukuru kuwepo kwa mradi wa maji kutoka Mto Kiwira na Truu ni mkombozi pia kwa Mbeya Vijijini na hata Mji Mdogo wa Mbalizi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kutokana na upungufu mkubwa wa maji kwenye mito kutokana na mabadiliko ya tabianchi na changamoto zingine napendekeza kujenga mabwawa makubwa kwenye maeneo ya vyanzo vya mito ambayo iwe pamoja na mabwawa makubwa kwenye vijiji vyenye uhaba wa mvua kama vile Mjele, Mshewe na Songwe. Rasilimali ya maji inaendelea kupungua kwa kasi kutokana na ongezeko la watu, uharibifu wa mazingira na pia mabadilko ya tabianchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, wastani wa maji umepungua kutoka mita za ujazo 7,862 kwa mtu katika mwaka 1962 na kupungua hadi wastani wa mita za ujazo 1,800 kwa mtu kwa mwaka 2017. Inaelekea mwaka 2025 upungufu utafika mita za ujazo 1,500 kwa mtu ambayo ni chini ya wastani wa mita za ujazo 1,700 kwa mtu. Kwa mwaka 2025 tutakuwa tumeingia kwenye kundi hatarishi (water stressed countries). Kutokana na hali hiyo napendekeza Wizara ichukue hatua kubwa za kukabiliana na changamoto hizi ikishirikiana na Wizara ya Mazingira. Jitihada za kukabiliana na changamoto za upungufu wa maji zionakane kwenye bajeti ikiwemo kuongeza bajeti ya mabwawa na utunzaji wa vyanzo vya maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, kutokana na mahitaji makubwa ya bajeti ya maji na pia changamoto za upatikanaji wa fedha za nje napendekeza kuongeza tozo za mafuta kwa kila lita ya petroli na dizeli kutoka shilingi 50 hadi shilingi 100. Imedhihirika kwa mwaka 2017/2018 Mfuko wa Maji ulikusanya shilingi bilioni 158 na Wizara imetumia ipasavyo na imeleta mafanikio makubwa katika utekelezaji wa kwenye miradi ya maji vijijini.

Mheshimiwa Naibu Spika, kutokana na changamoto za utekelezaji wa miradi ya maji katika Halmashauri zetu napendekeza uanzishwaji wa Wakala wa Maji Vijijini. Wakala wa Maji Vijijini atawezesha kupunguza uhaba wa wataalam wa maji na pia ataongeza uwajibikaji katika utekelezaji kwa wakala wa maji vijijini kutawezesha utekelezaji wa miradi ya maji kwa ubora na ufanisi zaidi.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja.