Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maji na Umwagiliaji kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

Hon. Janet Zebedayo Mbene

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Ileje

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maji na Umwagiliaji kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

MHE. JANET Z. MBENE: Mheshimiwa Naibu Spika, ninashukuru kwa fursa ya kuchangia hoja ya Wizara hii muhimu na ya kipaumbele kwa mustakabali wa maendeleo, afya na ufanisi wa Taifa letu. Mengi yaliyochangiwa na Wabunge kuhusu utaratibu mzima na usimamizi wa Wabunge kuhusu utaratibu mzima na usimamizi wa miradi ya maji ni ya maana na ni lazima sasa hivi ufanywe uchunguzi wa kina kuhusu matumizi ya fedha nyingi sana za miradi ya maji ncjhi nzima.

Mheshimiwa Naibu Spika, ningependa kuungana na Wabunge wenzangu waliopendekeza kuwa miradi ya maendeleo ya maji isimamiwe moja kwa moja na Wizara ya Maji yenyewe badala ya huu utaratibu wa sasa wa kuachiwa Halmashauri. Hii tunaiomba kwa sababu tumeona kule ambako Wizara imesimamia miradi imekuwa na ufanisi zaidi.

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kuishauri Serikali kwa mara nyingine tena kuwa Tanzania ina mikoa mingi inayopata mvua nyingi sana na inaishia ardhini au baharini. Serikali ituoneshe mpango mkakati iliojiwekea wa kuvuna maji nchi nzima kutumia njia mbalimbali, kuchimba mabwawa makubwa ili yatumike kumwagilia mazao, kufuga samaki na kutumiwa majumbani na taasisi, kuwekwa matanki ya kukinga maji kwenye taasisi za kijamii na kaya za watu maeneo yote. Tunaitaka Serikali ije na mpango madhubuti ulioainisha maeneo ya kujenga mabwawa na kuweka matenki (mapipa).

Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara ya Maji ishirikiane kwa karibu sana na Wizara ya Mazingira na Wizara ya Ardhi na ya Kilimo kwa ajili ya kuweka mipango ya pamoja ya uvunaji maji, ulinzi wa vyanzo vya maji na umwagiliaji na kilimo na ufugaji. Hili ni muhimu, tunaomba tamko na mkakati wa Wizara katika hili.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna miradi mingi mipya ya maji imeshapata kibali cha kuingiwa mikataba kutoka Wizara ya Maji, lakini haipelekewi fedha, je, utaratibu ukoje? Vilevile Halmashauri nyingi zimewasilisha hati za madai Wizarani, lakini fedha hazijatolewa na tunajua kuchelewa kulipa husababisha penalty ambazo zinatuletea gharama nyingine, je, kuna utaratibu gani katika ulipaji wa certificates?

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna haja sana ya bajeti ya kuhamasisha na kutoa mafunzo ya umuhimu wa kutunza vyanzo vya maji na kuweka adhabu kali kwa wote wanaovamia vyanzo vya maji kama ambavyo Maliasili wamesimamia maeneo yote ya hifadhi. Ninaomba Wizara ya Maji ijifunze kutoka nchi kama Israel, Afrika Kusini au Australia na hata nchi za Marekani Kusini juu ya jinsi ya kutunza maji yote yanayopatikana Tanzania.

Mheshimiwa Naibu Spika, usimamizi wa fedha inayotolewa kwenye miradi ya maendeleo ya maji si ndogo kwa kiwango chochote kile. Kitu kinachohitajika sasa ni jinsi ya kufanya ufuatiliaji na tathmini ya karibu ya matumizi ya fedha hii ili kila senti ilete thamani stahili.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo unda kamati ya kufuatilia matumizi ya fedha yote iliyoingizwa kweye maji kwa miaka mitano iliyopita. Naunga mkono hoja na naomba kuwasilisha.