Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maji na Umwagiliaji kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

Hon. Innocent Sebba Bilakwate

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kyerwa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maji na Umwagiliaji kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

MHE. INNOCENT S. BILAKWATE: Mheshimiwa Naibu Spika, nimshukuru Mungu kwa kuniwezesha kuendelea kuwatumikia wananchi wangu wa Jimbo la Kyerwa. Pia nikushukuru wewe binafsi kunipa nafasi ya kuchangia Wizara hii muhimu ya Maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, nichukue fursa hii kumpongeza Mheshimiwa Rais wangu, Waziri, Naibu Waziri na watendaji wake wote kwa kazi nzuri zinazofanyika kuboresha huduma ya upatikanaji wa maji kwa Watanzania, yaani kumtua mama ndoo kichwani.

Mheshimiwa Naibu Spika, maji ni muhimu sana na ni ukweli usiopingika Serikali inafanya kazi kubwa sana ingawa ziko changamoto nyingi ikiwemo upungufu wa pesa pamoja na wataalam wa kutosha.

Mheshimiwa Naibu Spika, nichukue fursa hii pia kuishukuru Wizara ya Maji kwa pesa ambayo tumetengewa mwaka 2017/2018 shilingi bilioni 2.1 ambazo zimetusaidia kuboresha miradi mbalimbali kama mradi wa Mabila, Kaisho, Isiringiro, Rutunguru, Kagenyi na mengineyo midogo midogo. Lakini pia tumeweza kuanza mradi mpya wa vijiji 57 ambavyo utakuwa mkombozi kwa Wanakyerwa ambao utaweza kuhudumia zaidi watu 200,000 utakapokuwa umekamilika.

Mheshimiwa Naibu Spika, mradi huo mkubwa tumefikia hatua ya kutangaza tender, namuomba sana Mheshimiwa Waziri na watendaji wake wa Wizara kutufuta machozi ya kilio cha muda mrefu cha kukosa maji kwa wana Kyerwa ambao hali yao ya upatikanaji ni mbaya sana. Kwa kweli naomba sana Serikali imetuweka kwenye bajeti tumetengewa shilingi bilioni moja tu ambapo mradi unahitaji zaidi ya shilingi bilioni 140. Natambua sana hatua hii tuliyofikia ya usanifu na design Wizara imefanya kazi kubwa. Waziri, Mkurugenzi wa Maji Vijijini kuhakikisha tunafikia hapa, bado imani yangu ni kubwa sana kwao mpaka mradi huo unakamlilika na Wanakyerwa wanapata maji safi na salama.

Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara ya Maji inafanya kazi nzuri na kubwa sana lakini miradi inayosimamiwa na Halmashauri ni kampuni za mifukoni na za kupeana kiurafiki, na hatimaye miradi ni ya hovyo. Mfano miradi ya Itera, Mradi wa Rutunguru, Kaisho na Isingiro mpaka sasa hakuna kinachoendelea. Kuna mradi kata ya Rukuraijo vifaa vimeibiwa kama solar na vingine, lakini hakuna hatua zilizochukuliwa na maradi wa Kigorogoro ambao una zaidi ya miaka kumi lakini hakuna kinachoendelea. Niiombe Wizara kufuatilia miradi kujua kinachoendelea, lakini pia kukagua kazi iliyofanyika, kwamba ni sawa na pesa iliyotolewa?

Mheshimiwa Naibu Spika, kama Wabunge wengi walivyoshauri kuongezwa shilingi 50 kwenye mafuta ili mradi kama wetu ambao ni mkubwa uongezewe pesa na hii itasaidia Wizara kuendelea angalu kuongeza bajeti yao.

Mheshimiwa Naibu Spika, kutokana na usimamizi usioridhisha wa baadhi ya Halmashauri kwenye sekta ya maji kama ilivyokuwa kwenye upande wa barabara zilizokuwa zinasimamiwa na Halmashauri na ikaundwa TARURA, tuombe sana Serikali kuunda chombo ambacho kitasimamia maji vijijini yaani Wakala wa Maji Vijijini hii itasaidia sana Wizara kuongeza ufanisi.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo niendelee kumshukuru Waziri, Katibu Mkuu na watendaji wake wote wa Wizara kutusaidia kufika hapo tulipofika kuanzisha mradi wa vijiji 57 ushirikiano umekuwa mkubwa sana. Naunga mkono hoja.