Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maji na Umwagiliaji kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

Hon. Joseph Leonard Haule

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Mikumi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maji na Umwagiliaji kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

MHE. JOSEPH L. HAULE: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kwa nafasi hii. Awali ya yote nashukuru sana kwa ziara za Mheshimiwa Rais, Waziri wa Maji, Naibu Waziri wa Maji na Katibu Mkuu wa Wizara ya Maji katika Jimbo letu la Mikumi. Natumaini mmezisikia changamoto za watu wa Mikumi kuhusu maji na ninashukuru sana baadhi ya changamoto hizo zimepata ufumbuzi. Baada ya kutoa shukrani hizo, naomba nichangie changamoto kadhaa za muhimu Jimboni Mikumi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu Mradi wa Maji wa Madibira, huu ni mradi wa muda mrefu sana tangu mwaka 1974 hadi 1975 na miundombinu yake imechakaa sana. Nashukuru Serikali imetenga shilingi 300,000,000 ili kukarabati na kutanua intake pamoja na upanuzi wa mitandao ya kuunganisha wateja. Ila nasikitika kuwa karibu mwaka mmoja sasa mzabuni amepatikana ila bado hajapewa kibali cha kuanza kazi kutoka Wizarani. Tunaomba sana apatiwe kibali ili aanze kazi hiyo ya kukarabati miundombinu mara moja.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mradi wa Maji wa Sigaleti (Kata ya Ruaha); chanzo hiki cha maji kilifanyiwa usanifu na wataalam wa maji wa Wilaya ya Kilosa baada ya kuagizwa na Mheshimiwa Waziri ambaye alifanya ziara Jimboni Mikumi mwaka 2017. Wataalam walijiridhisha kuwa chanzo hiki kina maji mengi na salama na uhakika na pia yanaweza kusaidia sana wananchi wa kata kubwa ya Ruaha yenye wakazi 35,000 pamoja na kata za jirani za Kidodi, Vidunda na Ruhembe. Pia wataalam walifanya tathmini kuwa kiasi cha shilingi bilioni mbili kinatakiwa ili kufanya mradi huu uweze kuhudumia wananchi hawa wanaoteseka na tayari tathmini hiyo nilishaikabidhi kwa Waziri husika. Tunaomba sana mradi huu uweze kuingizwa katika bajeti ya mwaka huu ili kumtua mama wa Ruaha ndoo kichwani.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu Bwawa la Dachi (Kata ya Malolo); bwawa hili ni muhimu sana kwa umwagiliaji katika Kata ya Malolo, mradi huu ulifadhiliwa na JICA ya Japani kwa fedha shilingi 600,000,000 ili kujenga makingio ya mchanga unaotishia kuupoteza kabisa Mto Mwega unaotumiwa sana na kutegemewa sana na wananchi wa Kata ya Malolo kwa kilimo. Kumetokea ubadhirifu mkubwa sana wa fedha hizo na makingio yaliyojengwa yamejengwa chini ya kiwango na kusababisha mchanga kuendelea kumwagika kutoka milimani na kwenda kujaza Mto Mwega. Nilishawahi kuomba Serikali iingilie kati na Mheshimiwa Waziri aliahidi kulifuatilia jambo hili, lakini naona hakuna majibu mpaka sasa.

Mheshimiwa Naibu Spika, namuomba sana Mheshimiwa Waziri atakapokuja kujumuisha atuambie amefikia wapi na tunaomba sana Wizara iweze kuingilia kati na kusikia kilio hiki cha muda mrefu sana cha wananchi wa Kata ya Malolo kwani tegemeo lao la kilimo linategemea sana Mto huu wa Mwega.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunaomba sana tusaidiwe visima virefu katika Jimbo la Mikumi kwani tumekuwa tukisahauliwa sana katika uchimbaji wa visima virefu hasa katika kata za Ruhembe, Vidunda, Mhenda, Tindiga, Zombo, Malolo, Uleling’ombe, Kisanga, Mabwerebwere, Kilangali, Mikumi, Ruaha, Kidodi, Masanze na Ulaya. Tunaomba sana kata hizi za Jimbo la Mikumi zifikiriwe kwa jicho la huruma maana wananchi wetu inafika mahali wana-share kunywa maji kwenye mito na wanyama kitu ambacho kinahatarisha sana afya zao na magonjwa ya maambukizi.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mikumi tumebarikiwa kuwa na vyanzo vingi sana vya maji. Mwisho kabisa niiombe sana Wizara itume wataalam wake kwenye Jimbo la Mikumi kwa kuwa pamoja na taabu na changamoto kubwa sana ya maji tunayokabiliana nayo lakini Jimbo la Mikumi limebarikiwa vyanzo vingi sana vya maji ambavyo vingeweza kumaliza kabisa kero ya maji.

Mhshimiwa Naibu Spika, kwenye Jimbo langu la Mikumi tunaomba sana wataalam waje kuviangalia vyanzo vifuatavyo; Mto Iyovi, Mto Simbalambende na Kisanga. Natumaini tukifanikiwa kuvitumia vyanzo hivi tutakuwa kwa kiasi kikubwa tumefanikiwa kumtua mama ndoo kichwani. Ahsante.