Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maji na Umwagiliaji kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

Hon. Anthony Calist Komu

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Moshi Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maji na Umwagiliaji kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

MHE. ANTONY C. KOMU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nikushukuru sana kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia bajeti hii ya Wizara ya Maji ambayo ni bajeti muhimu. Kwa maoni yangu ni bajeti ambayo ingepaswa iwe labda namba mbili baada ya bajeti ya Wizara ya Elimu kwa umuhimu. Maji ni uhai si uhai wa binadamu tu isipokuwa uhai wa viumbe na hata uhai wa uchumi wenyewe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kuangalia hali ya maji nchini. Waziri amejaribu kujenga picha kwamba tuna hali nzuri sana katika Afrika Mashariki kwa sababu kiasi cha maji sasa hivi kwa maana ya mita za ujazo kilichopo kwa ajili ya matumizi ya kila mtu ni 1,800 kama alivyosema na akasema sisi ni wa kwanza Afrika Mashariki. Nataka Bunge lielewe, kwa mujibu wa taarifa za wataalam wa Wizara hali yetu ya maji si nzuri kwa sababu ifikapo mwaka 2025, tutakuwa tupo chini ya kiwango ambacho kinahitajika kwa binadamu mmoja, tutakuwa tumefikia mita za ujazo 1,500 na tutatangazwa kama nchi yenye uhaba. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia uwekezaji unaofanywa kwenye maji inaonekana wazi kabisa kwamba huko ndiko tunakokwenda. Kwa hiyo, kutulinganisha sasa hivi na walemavu wengine haitusaidii sana, ni lazima tuzungumze hali halisi na kwamba hali yetu ni mbaya na uwekezaji wetu hauashirii hata kidogo kwamba tutazuia kwenda kwenye nchi ambayo ina uhaba mkubwa wa maji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nasema hivyo kwa sababu leo tunavyozungumza katika vijiji vyetu vyote ni asilimia 46 tu ya watu wenye maji salama na maji safi. Sasa hili si jambo la kujisifia. Ukiangalia fedha ambazo zimetengwa kwa ajili ya bajeti ya maji hazioneshi kama tunaweza tukajiondoa hapa tuliko kwa sababu ni fedha kidogo, lakini vilevile pesa hizo zikishatengwa hazipelekwi na mahali pengine inakwenda sifuri kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nimejitahidi kusoma kidogo na hawa watu wa Wizara wamefanya kazi kubwa sana, wametengeneza miradi yote ya maji katika nchi hii kwenye hiki kitabu na zipo hapa. Wameonesha ili miradi yote ya maji iweze kukamilika tunahitaji shilingi trilioni 32.4 lakini leo pesa tuliyotenga, tumetenga shilingi bilioni 20 maana yake ni kwamba tunahitaji miaka 1,200 ili tuweze kukamilisha kilichoandikwa humu, tunatania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia mwaka jana pesa ambazo zilitengwa kwa ajili ya Tume ya Taifa ya Umwagiliaji shilingi bilioni sita, wamesema hapa kwamba hiyo bajeti imetekelezwa kwa asilimia 12 lakini waseme vilevile kwamba fedha za ndani hazikwenda hata shilingi moja, zimekwenda asilimia sifuri, fedha za nje ndizo zilizokwenda shilingi bilioni 2 ambazo ndizo zinazofanya asilimia 12. Katika hali ya namna hii tunatania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini maana ya kuwekeza kwenye maji ni nini? Maana ya kuwekeza kwenye maji ni kuwa na ajira ya uhakika, chakula cha kutosha na kuacha ku-import chakula kutoka nje. Leo kwa taarifa ya Benki Kuu ya Tanzania tunaagiza chakula kutoka nje cha shilingi bilioni 888.5 kila mwaka. Hizi fedha tungeweza tukazi-save, ndiyo maana sisi watu wa upinzani tunashangaa kweli kweli mnavyoshangilia hapa kuhusu kununua ndege cash. Hivi tuna-luxury gani ya kwenda kuwekeza shilingi trilioni moja kwenye ndege wakati kila mwaka tunapoteza shilingi bilioni 800 kwa ajili ya kununua chakula kwa sababu hatuwekezi kwenye maji? Tukiwekeza kwenye maji tukaokoa hizo fedha maana yake ni kwamba kila mwaka tungeweza kununua hizo ndege sita kwa mpigo, lakini kweli tumeanza na ndege ndiyo maana sisi tunawashangaa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hiyo ni hali ambayo kama hatutabadilika, tukaamua kuchagua vipaumbele ambavyo ni sahihi, vipaumbele vinavyowagusa watu wetu, vipaumbele ambavyo vinatufanya tuweze kupiga hatua kwa namna ya kuweza kuchochea uchumi wetu bado tutaendelea kuingia katika hatari na kama nilivyosema tunakwenda sasa ku-approach danger zone kwamba tutakuwa nchi ambayo wanaita kwa kiingereza water stress.

Nashauri tuangalie upya na hili ni Bunge tusimame kama Bunge tuisimamie na kuishauri Serikali iache haya mambo ambayo ni ya kujenga impression wakati hali yetu ni mbaya.

Mheshimiwa Mwenyekiti nikienda kwenye miradi hii ambayo imetangazwa humu, iko miradi ya umwagilaji ya toka mwaka 2004 haijaisha. Katika miradi 312 ni miradi 55 tu ambayo imeweza kukamilika maana yake ni asilimia 17. This is very serious. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti kama Wabunge wengine walivyosema unavyokwenda kumpa mkandarasi pesa kidogokidogo, unakuta kuna mradi ambao unapaswa ujengwe kwa shilingi bilioni sita unapeleka shilingi bilioni 900, hauko serious. Tabia hii ni lazima tuibadilishe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niende kwenye jimbo langu. Kule kwenye la Moshi Vijijini tuna mradi mmoja wa Kata ya Old Moshi Magharibi na niliwahi kuuliza kwenye swali la msingi hapa ulitangazwa toka mwaka 2012, tukaambiwa mkandarasi atakwenda site, kila tukiuliza tunaambiwa utaanza mwaka unaofuata mpaka leo huo mradi wa vijiji vya Telamande haujaanza. Naomba Waziri akija hapa atuambie huo mradi utaanza lini? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii asilimia 46 wanayosema kwamba kuna maji, wanahesabu mpaka yale mabomba ya Moshi Vijijini yaliyojengwa na Lucy Lameck mwaka 1975 ambapo miundombinu yake imeshachakaa na vyanzo vingi vya maji hayo vimeshakauka, kwa hiyo na vyenyewe wanahesabu kwamba kuna maji. Ndiyo maana kuna watu wengine watu wa Kaskazini wasubiri kwa sababu wanafikiri kule kuna maji, sisi kule tuna shida. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna kata yangu moja inaitwa Mabogini ina vijiji kumi ni vijiji vinnetu vina maji. Kule Mtakuja kwa Wamasai, Mserikia, Mawala kwa Mheshimiwa Mbatia, Mikocheni TPC hakuna maji, watu wanatafuta maji kama wanavyotafuta mafuta ya taa au petroli. Kwa hiyo, tunaomba muangalie mambo haya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna mradi mkubwa ambao ulijengwa na Wajapani unaitwa Moshi Lower Irrigation Scheme. Mradi ule ni wa kisasa sana lakini na wenyewe kwa sababu hakuna maintenance fund, hakuna watumishi wenye weledi wa kuweza kusimamia machines ambazo zimeachwa kule, hakuna mashine hata moja inafanya kazi na sasa hivi unaanza kubomoka na huko kwenye hatari vilevile ya kwisha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho, huu utaratibu wa kutokupeleka fedha kwenye Wizara mbalimbali na hasa hii ya Maji maana yake ni kwamba there is no value for money kwa zile pesa za matumizi tunazotoa, unalipa mtu ambaye humtumii. Maana yake ni kama unatoa sadaka au ruzuku tu na hii ni matumizi mabaya ya fedha za walipa kodi wa nchi hii. Ni lazima tusimamishe hayo mambo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ningeomba sana Bunge lako liielekeze Serikali ichukue vipaumbele vichache vyenye matokeo makubwa kwenye uchumi wetu, iweke nguvu hapo na imalize miradi hiyo. Leo tunaenda kushika Stigler’s Gorge, hatujaangalia uchumi wa gesi kule umeendaje, tunaenda kuangalia Stigler’s Gorge kuna Mchuchuma na Liganga ambao unaweza kutupa umeme hatuendi, sasa tukifanya hayo mambo kwa mtindo huo hatutaweza kufika.