Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

Hon. Dr. Stephen Lemomo Kiruswa Mamasita

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Longido

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

MHE. DKT. STEVEN L. KIRUSWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, pongezi kwa Rais wetu Dkt. John Joseph Pombe Magufuli kwa kazi kubwa na nzuri anayofanya kwa maendeleo ya nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pongezi kwa Waziri Profesa Ndalichako na Naibu wako Ole Nasha kwa hotuba yako nzuri iliyosheheni mambo mengi mazuri kuhusu elimu nchini mwetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nachangia hoja katika masuala matatu; kwanza, elimu ya awali (tazama hotuba ukurasa 78), pili; elimu maalum (tazama hotuba ukurasa 81) na tatu; Programu ya Lipa kwa Matokeo (EP4R) ukurasa wa123 – 124.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza elimu ya awali, Serikali iweke kipaumbele katika uanzishwaji wa shule za chekechea, shule za awali kabla ya darasa la kwanza (pre- schools). Kwa kuwa msingi mzuri wa elimu huanzia katika shule za awali, nashauri ijihusishe rasmi katika uanzishwaji wake na kuajiri walimu waliofuzu kutoa elimu kwa ngazi hiyo (early childhood development).

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali iandae mitaala ya elimu ya awali. Nashauri Serikali ianzishe taasisi mahsusi ya elimu ya awali kama ilivyo Taasisi ya Elimu ya Watu Wazima.

Mheshimiwa Mwenyekiti, siri ya mafanikio katika shule za binafsi ni kwa sababu wamezingatia kumuendeleza mtoto kuanzia umri mdogo kabisa (3 -5 years) kabla ya kuanza elimu ya msingi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kuelekeza juhudi za kuboresha elimu nchini kuanzia ngazi ya elimu ya awali, naomba Serikali izingatie kuwa shule za awali zilizoko ndani ya shule za msingi nchini haziwasaidii watoto wadogo walio chini ya umri wanaotoka au kukaa mbali na shule, hususan kwa jamii za wafugaji wanaoishi mbali na shule. Hivyo Serikali izingatie haja ya kusogeza huduma za elimu bora ya awali hadi kwenye vitongoji. Elimu hii itolewe na walimu waliosomea tofauti na sasa ambapo elimu hii ndani ya vituo vya ngazi ya vitongoji hutolewa na walimu wasio na ujuzi (failures wa darasa la saba au kidato cha nne) wanaoajiriwa na wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, elimu maalum; ukienda ukurasa wa 81 wa kitabu cha hotuba ya Waziri kifungu cha 80(i) na (ii) utapata maelezo yasiyojitosheleza kuhusu usimamizi wa elimu maalum. Natoa rai kwa Serikali/Wizara ijipambanue kwa ufasaha zaidi kuhusu elimu maalum. Naunga mkono suala la elimu jumuishi lakini nashauri kuwepo kwa vitengo mahsusi ndani ya shule zetu kuanzia chekechea hadi vyuo kwa ajili ya nyanja mbalimbali za elimu maalum. Mbadala wake zianzishwe shule mahsusi kwa ajili ya ulemavu wa aina tofauti. Shule za viziwi (chekechea – vyuo), vipofu (chekechea – vyuo), wenye mtindio wa ubongo (chekechea – vyuo).

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu programu ya lipa kulingana na matokeo katika elimu (EP4R), huu mpango ni mzuri sana. Naomba uongezewe bajeti na wigo wa miradi ya kutekelezwa upanuliwe kulingana na mahitaji ya shule husika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba katika Wilaya yangu ya Longido fedha hizi pamoja na mambo yameshaelekezwa, lakini pia zielekezwe katika kununulia gari la shule. Sekondari zetu saba zilizo katika remote areas ambapo huduma muhimu na dharura ikitokea ziko mbali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, shule za sekondari za bweni Wilayani Longido ambazo zinastahili kuwa na gari la shule ni pamoja na shule ya wasichana Lekule iliyoko Gelai Lumbwa umbali wa kilometa 90 kutoka barabara ya lami na makao makuu ya Wilaya, Flamingo sekondari Kata ya Meirugoi ambayo ipo zaidi ya kilometa 90 kutoka barabara ya lami, shule ya sekondari Ketumbeine iliyoko umbali wa kilometa 60 kutoka lami, shule ya Enduimet sekondari kilometa 110 kutoka Longido Mjini na barabara ya lami, sekondari ya Tingatinga kilometa 50, sekondari ya Engeremibor kilometa 40, sekondari mpya tarajiwa ya Matale kilometa 60.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.