Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi kwa mwaka wa fedha 2016/2017.

Hon. Janet Zebedayo Mbene

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Ileje

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi kwa mwaka wa fedha 2016/2017.

MHE. JANET Z. MBENE: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kukushukuru kwa fursa hii ya kuchangia hotuba hii. Nampongeza Mheshimiwa Mwigulu Nchemba, Waziri wa Kilimo, Mifugo na Uvuvi na Naibu Waziri wake, Watendaji Wakuu wa Wizara pamoja na Katibu Mkuu na Naibu Makatibu Wakuu na Watendaji wote kwa kazi nzuri na iliyotukuka inayofanywa na Wizara yao. Napongeza hotuba nzuri iliyosheheni mipango na utekelezwaji wake wenye uhalisia, inayotekelezeka na itakayoleta maendeleo ya uhakika katika sekta hii muhimu. Wizara iwatumie sana vijana wasomi katika sekta hii.
Mheshimiwa Naibu Spika, ili Taifa letu liendelee kwa kasi ni lazima tuboreshe kilimo na viwanda kwa kuzingatia kuendesha kilimo cha kisasa kwa maana yake pana. Napendekeza kuundwa kwa vikosi kazi vya vijana wawazalishaji wa kilimo, ufugaji na uvuvi wa kisasa na hawa watengewe maeneo, waandikishwe kama vikundi rasmi na wajengwe uwezo wa kielimu, kimitaji, nyenzo, mbegu, mitamba na vifaranga vya samaki. Waunganishwe na masoko na wajengewe maghala.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imekuwa ikitumia fedha nyingi kuagiza mbegu nje ya nchi ilhali Tanzania ina ardhi kubwa na ya kutosha, vile vile tuna mashamba yaliyotengwa kwa ajili ya uzalishaji wa mbegu ambayo yamekuwa na matumizi hafifu. Tunayo maeneo mengi yaliyotengwa na yanayofaa kufuga mitamba yatumiwe kikamilifu ili wananchi waweze kufuga mifugo bora kwa kipato, ajira, lishe hata biashara ya nje.
Mheshimiwa Naibu Spika, maeneo yanayozalisha mazao ya aina mbalimbali kwa wingi hasa Nyanda za Juu Kusini, Kaskazini, Kusini na Magharibi yana changamoto kubwa ya maghala ya uhifadhi wa chakula kwa usalama, biashara na hata kuunganishwa na mfumo wa leseni za stakabadhi ghalani. Naomba kufahamu ni vigezo vipi vinavyotumika kugawa maghala haya? Ileje haijatengewa fedha za ujenzi wa maghala pamoja na kuwa ni wilaya mojawapo inayoongoza kwenye kuzalisha chakula. Naomba Serikali ipitie upya mgao huu na kuitendea haki mikoa yenye uzalishaji mkubwa na yenye fursa kubwa kwa maendeleo ya kilimo, mifugo na uvuvi.
Mheshimiwa Naibu Spika, kutokana na lengo la kuboresha sekta hizi kuna haja sasa ya kutumia teknolojia ambayo imesambaa maeneo yote kuanzisha rural telecentres ambazo zitatumika kutoa taarifa za uzalishaji bora, masoko na taarifa za hali ya hewa kwa wazalishaji. Maafisa Ugani wapangwe upya kwenye vijiji na wapewe vigezo vya kazi zao na wapimwe kutokana na utendaji wao yaani tija itakayotokana na huduma kwa wazalishaji. Kila Afisa Ugani awe na mashamba ya mfano ya mkulima, mfugaji, mvuvi au yeye mwenyewe aoneshe mfano huo. Vijana wasomi watumiwe kwa kiasi kikubwa kwenye maeneo haya.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuna haja kubwa ya kuiboresha sekta ya ufugaji kwa kuboresha elimu ya ufugaji, kuboresha huduma za biashara ya mifugo kwa kuzingatia ubora wa mifugo inayokubaliwa Kimataifa ili tuweze kuuza nje mifugo na bidhaa za mifugo yetu na kuwaongezea wafugaji kipato. Vile vile kuna haja ya kuhamasisha matumizi zaidi ya bidhaa za ufugaji hapa nchini yaani nyama, maziwa, mayai na kadhalika. Hili likizingatiwa siyo tu litaboresha afya ya wananchi hasa watoto bali itakuza soko la ndani na kukuza kipato cha ufugaji.
Mheshimiwa Naibu Spika, suala la masoko ya mifugo ni changamoto kubwa yanahitaji kufanywa ya kisasa zaidi kwa kuwa na huduma muhimu. Vile vile kutenga maeneo siyo tu ya kufunga bali ya kunenepesha mifugo kabla ya kupeleka sokoni. Serikali iainishe malengo yanayotegemewa kwenye maeneo kwa ufugaji, mapato tunayotegemea na mifugo mingapi inategemea kuhudumiwa katika mfumo huu.
Mheshimiwa Naibu Spika, kutokana na matatizo ya tabia nchi na umuhimu wa mazao ya uvuvi kwa lishe, ajira na mapato imefikia wakati sasa wa kuainisha kwa kasi na nguvu kubwa uvuvi wa mabwawa nchi nzima ili kutoa ajira nyingi hasa kwa vijana na lishe na biashara. Hii ni shughuli ambayo ni umuhimu na inatoa fursa kubwa sana kwa ajira na biashara. Tungependa kupata taarifa kamili ya mpango mkakati wa maendeleo ya uvuvi huu Tanzania mapema iwezekanavyo ikiainisha wapi Serikali inalenga kuwekeza mabwawa ya kuzalisha vifaranga, vyakula vya samaki na mabwawa yenyewe kila Wilaya yatakuwa mangapi, wapi na vijana wangapi wanalengwa na tunategemea kuongeza pato la Taifa kwa kiasi gani?
Mheshimiwa Naibu Spika, uhusiano kati ya Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi na Wizara ya Viwanda. Ili Sera ya Viwanda ifane, kuna haja ya Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi wakae pamoja na Wizara ya Viwanda ili kuhakikisha kuwa viwanda vya usindikaji vinajengwa sehemu zenye uzalishaji mkubwa wa mazao ya kilimo, ufugaji na uvuvi. Hii itahakikisha mavuno yote ya kuchakatwa yako tayari wakati viwanda vinapojengwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, Wilaya ya Ileje imepata bajeti ndogo sana ya kilimo chini ya TAMISEMI, hii ni fedha ndogo sana kwa uzalishaji mkubwa unaotakiwa Ileje. Vilevile Ileje pamoja na uzalishaji wa mazao mengi haijapangiwa maghala ambayo ni muhimu sana kwa uchumi wa soko. Naomba Wizara ipitie upya uamuzi wake wa kujenga maghala kwa kuzingatia uzalishaji uliopo. Serikali ipitie upya mgao wa fedha kimkoa kwenye kilimo. Mikoa inayozalisha kwa wingi iwezeshwe zaidi.
Mheshimiwa Naibu Spika, wakati tunazungumzia kuboresha kilimo cha kisasa na kwenda kwenye uchumi wa viwanda ni lazima tuwe na mpango wa haraka wa upimaji ardhi. Kwa kufanya hivyo itakuwa rahisi hata kwa wawekezaji wanaotaka kuja kuwekeza kwenye kilimo, ufugaji na uvuvi kufanya hivyo.
Mheshimiwa Naibu Spika, ushirika bado hatujaupatia vizuri jinsi ya kutunufaisha. Tusimamie vizuri suala hili la ushirika na usimamizi wake na wazalishaji wenyewe wasimamie.
Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante na naunga mkono hoja.