Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

Hon. Othman Omar Haji

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Gando

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

MHE. OTHMAN OMAR HAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kunipa nafasi hii kuchangia katika Wizara hii ya Elimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza naomba nimpe angalizo kwanza Mheshimiwa Waziri kwamba nchi yetu kitakwimu inakuwa na idadi kubwa ya watu. Idadi hii inakwenda kuathiri kwa njia moja au nyingine katika sekta yetu ya Wizara ya Elimu, sasa sijui Mheshimiwa Waziri ameliona hili na ikiwa ameliona amejipanga namna gani? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili nchi yetu imetangaza kwamba inakwenda kuwa Taifa la viwanda. Taifa la viwanda linahitaji rasilimali watu wenye ujuzi ambao wataweza kuzalisha kwa ufanisi na wenye tija. Kama ulivyozungumza katika hotuba yako page namba 42 kwamba vyuo vikuu ni nguzo moja muhimu sana katika kuhakikisha kwamba Serikali inakwenda kutekeleza malengo yake muhimu yaliyojipangia kwa kuzalisha rasilimali watu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vyuo vikuu kuna changamoto zake, nafikiri unafahamu Mheshimiwa Waziri kwamba vyuo vikuu kuna changamoto za wanafunzi wanaosoma elimu ya juu. Moja ya changamoto hizo Mheshimiwa Waziri ni kwamba wanafunzi wanaosoma masomo ya Uzamili, baadhi ya masomo wanachukua si chini ya miaka minne. Mafunzo hayo Mheshimiwa Waziri ikiwa utakwenda kusoma nchi za nje yanachukua si chini ya miaka miwili. Tatizo hili Mheshimiwa Waziri inakuwaje hapa nchini wanafunzi wetu wasome zaidi ya miaka minne ambapo nchi za wenzetu wanakuwa ni chini ya miaka miwili, nini kimeongezeka hapa kwetu?

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukienda katika mafunzo ya Uzamivu utakwenda kusoma ikiwa hujaoa utaoa, ikiwa hujazaa utazaa, utapata wajukuu na utaota mvi bado degree hujahitimu, nini tatizo? Matatizo haya Mheshimiwa Waziri yanakwenda kusababisha uhaba wa Wahadhiri katika vyuo vyetu. Napenda Mheshimiwa Waziri hili ulione kwamba tatizo la kuwaweka wanafunzi muda mrefu katika masomo yao linakwenda kusababisha kuwa na uhaba wa Wahadhiri ndani ya vyuo. Tatizo ambalo halitakwenda sambamba na ongezeko la watu na ndiyo ukaona kuna idara nyingine pale vyuo vikuu wanachukua chini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitakupa mfano mmoja, Idara ya Fizikia pale Chuo Kikuu ambayo katika vyuo vyote vinavyotoa Masters hapa nchini ni Chuo Kikuu cha Dar es Salaam peke yake, lakini wanafunzi wanaoingia kwa mwaka hawavuki wanafunzi 11. Wanafunzi 11 kweli Mheshimiwa Waziri wanatosheleza nchi nzima kwa mwaka? Hao miaka minne hujahitimu pale. Hii ni kwa sababu Wahadhiri wetu hawataki kurithiwa, hawataki wasaidiwe pale Chuo Kikuu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mhadhiri anabakia pale hawezi kutoka mpaka apelekwe kaburini pale. Namuomba Mheshimiwa Waziri suala hili la kuwatesa wanafunzi wa vyuo vikuu linawarudisha nyuma, ukitilia maanani kwamba wanafunzi wengi wanaosoma vyuo vyetu vya ndani ni watoto wa kimaskini. Hili linapelekea wengi wao warudi nyuma wasipende kusoma katika vyuo vyetu vya ndani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nawaomba sana Wahadhiri wetu wa vyuo vikuu walione hili na waone kwamba wao wapo pale ili kulisukuma Taifa hili na Taifa linawategemea wao ili lisonge mbele.