Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

Hon. Edward Franz Mwalongo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Njombe Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

MHE. EDWARD F. MWALONGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ili na momi niweze kutoa mchango wangu kwenye Wizara hii ya Elimu, Sayansi na Teknolojia.

Awali ya yote, nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri na Naibu Waziri kwa kazi nzuri wanayoifanya, kwa kweli wanajitahidi, tunawaona wanakimbiakimbia, mara wako Njombe, Bukoba, Arusha kuangalia miundombinu mbalimbali ya shule na kuhakikisha kwamba watoto wa Kitanzania wanapata elimu nzuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi ni fundi na fundi niliyesoma kutoka shule ya sekondari ya ufundi na nikaenda chuo cha ufundi. Sasa hivi tunazungumza Tanzania ya viwanda lakini Tanzania hii ya viwanda tunayoizungumza kama vijana wetu wasipopata elimu ya ufundi ina maana kwamba vijana hawa wa Kitanzania watakuwa watumwa ndani ya nchi yao kwa sababu hawatakuwa na ujuzi wowote wa kufanya kazi katika viwanda hivyo ambapo wote tunasema tunaiendea Tanzania ya viwanda. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara ya Elimu ndiyo yenye jukumu la kutoa elimu na maarifa kwa Watanzania iache kufikiria kwamba ili kutoa elimu ya ufundi ni lazima tuwe na karakana kubwa sana, mashine kubwa sana, mitambo inayoendana na mitambo ya viwanda, hapana. Sisi wakati ule tunasoma ufundi tulisoma ufundi katika nyenzo ambazo zilituwezeshe kuwa mafundi mpaka leo tunafanya kazi hizo za ufundi na tunajivunia ufundi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa taarifa yako nikuambie humu ndani kuna mafundi sita ambao tumesoma na tunaujua ufundi vizuri na tunafanya kazi ya ufunzi vizuri kabisa. Uwekezaji kwenye ufundi kwa level ya sekondari ni kiasi kidogo sana, unaweza ukawa na shilingi 500,000 ukaanzisha fani ya ufundi sekondari. Kwa mfano, ufundi wa kujenga unahitaji kuwa na pimamaji, ndiyo kifaa cha gharama kuliko vifaa vyote, pimamaji moja ni shilingi ngapi? Chukulia shule ya sekondari inahitaji pimamaji kumi, unahitaji kamba ya kunyooshea ukuta, ubao, mwiko na konobao, hapo tayari fani ya ufundi kwa maana ya practical imekamilika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, unahitaji kitabu cha ufundi kwa maana ya theory na kitabu cha ufundi kwa maana ya michoro. Kwenye theory unahitaji ubadilishe masomo mawili tu, ubadilishe somo la physics liwe engineering science, lakini uondoe somo la biology uingize somo la somo la urasimu ama ufundi wenyewe. Kwa hiyo, ni rahisi sana kuweka ufundi sekondari kuliko kujenga Vyuo vya VETA. Leo hii kila mtu hapa analia ajengewe Chuo cha VETA, tutajenga Vyuo vya VETA mpaka lini ili tuweze kuendana na kasi ya ufundi? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu tuanzishe shule za sekondari za ufundi na si lazima kwenye shule ya sekondari ya ufundi tuanzishe fani sita au saba, tuanzishe shule moja, fani moja. Tunachukua shule moja tunaanzisha fani ya ujenzi, tunakwenda shule nyingine tunaanzisha fani ya umeme, shule nyingine tunaanzisha fani ya useremala, tunakwenda shule nyingine ya sekondari hivyo hivyo. Kwa hiyo, utakuja kuona jimbo zima ama nchi nzima sasa tunakuwa na shule nyingi za ufundi ambazo vijana wanapata maarifa na wakitoka pale wanakuwa tayari wanaanza kujitegemea. Tukisema tusubiri tuanze kujenga VETA, hela zenyewe sijui tunaomba wapi, wanaotupatia hela wana masharti, mpige magoti, mfumbe na macho, muombe na kuomba ndiyo hela zije, lini, tunachelewa, tufundishe ufundi vijana tujikomboe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vijana hawa wakisoma ufundi itawasaidia sana. Nataka niwaambieni wanaosoma ufundi sekondari wanakuwa ni mafundi wazuri kuliko mfano wake. Ufundi wa umeme unahitaji chini ya shilingi 500,000 kuanzisha umeme shuleni. Unahitaji bisibisi, koleo, kipande cha waya na kipande cha ubao, biashara imekwisha, huyo ni fundi. Hata akienda university atatumia vifaa hivyo hivyo kujifunza umeme. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba sana Mheshimwa Profesa Ndalichako hebu toa maamuzi angalau kila Halmashauri ianzishe shule moja ya ufundi kwa fani moja kama jaribio ili tuone tunakwendaje. Baada ya hapo tutafanya maamuzi kila Halmashauri iwe na shule ngapi za ufundi kadri watakavyoona mazingira, lakini kwenye maeneo yale ya wafugaji anzisheni mafunzo ya mifugo huko sekondari, watu wajifunze ufundi lakini kupitia fani za mifugo, sehemu za wavuvi wajifunze uvuvi sekondari kitaalum ili kusudi vijana hawa wakitoka hapo sekondari wawe tayari wana elimu ya kutosha kuliko kusubiri hizo VETA ambazo tunajua kwamba ni ngumu sana kuzijenga. Karakana zinazojengwa ni gharama sana, tunahangaika kujenga mabweni na kachalika, shule za kata zipo tuanzishe ufundi kwenye shule za kata angalau kila halmashauri au kila jimbo shule moja ya ufundi kadri watakavyoona mazingira yanaruhusu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo napenda kulishauri Serikali uko mkanganyiko ambao nauona katika ya NECTA na NACTE. NACTE wanasimamia mitihani ya ufundi katika vyuo vya kati, lakini NECTA wanasimamia mitihani ya shule ya msingi, sekondari na mitihani ya ualimu. NACTE imeanzishwa kwa sheria ambayo imeipa nguvu ya kusimamia vyuo vyote vya kati; vyuo vya majeshi, vya afya, vya mifugo, vya madini, lakini jambo la kushangaza kozi ya ualimu wa elimu ya msingi imekwenda NECTA, lakini imerudishwa NACTE kwa hoja kwamba ule mfumo ambao NECTA wanautumia kudahili na kutoa mitihani si mfumo ambao unaweza ukamjenga mwalimu kuja kuwa mwalimu bora. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyeki, mimi nasema huu ni mkanganyiko, kama Wizara ya Elimu ndiyo iliyosimamia kuanzisha kwa NECTA na ikaagiza kwamba sheria ile iliyotungwa vyuo vyote vya kati viwe chini ya NECTA halafu yenyewe Wizara ya Elimu imeamua kujipendelea kuchomoa kozi moja tu ya ualimu wa primary na kubaki nayo kule kusema kwamba hii tunabaki nayo sisi. Wakati huo huo inaongezea masharti mengine kwamba chuo chochote kinachofundisha ualimu kisiwe na kozi nyingine hapo mahali yaani hawa watu wanaojifunza ualimu wakae wao tu kama walimu wasiwe na mtu mwingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jamani hii dunia ni pana, tunapowaweka wale walimu wakae hivyo tunamaanisha nini? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashauri kozi ile ya walimu irudishwe NACTE na waisimamie na walishaweka mifumo mizuri ya kuhakikisha kwamba hata mwalimu wa primary ambaye yupo kazini arudi apate elimu zaidi na aweze kuendelea kielimu. Kwa sababu kozi ile ya grade A ilikuwa ni kozi ambayo mwalimu akisoma si sifa ya kuendelea na masomo yoyote anabaki pale miaka yote, lakini ukiangalia kwenye Sera mpya ya Elimu inataka walimu waliojiendeleza na waweze kuendelea zaidi.

Kwa hiyo, naomba sana Wizara muangalie muwape nafasi hiyo NACTE waendelee na mafunzo ya ualimu. Najua mlisema kwamba mnamashaka na ile mitaala na kadhalika lakini naomba basi hayo mashaka muwe mnayaondoa haraka, kama mnaona mashaka hayaondoki haraka basi tuwatafute na waombezi wawaombee ili kusudi mashaka yenu haya yaondoke haraka ili kazi iende. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo naliona nalo ni muhimu sana nilichangie hapa ni kuanzishwa kwa chombo huru cha kusimamia elimu. Tunasema kwamba chombo hiki kitasaidia sana kupata elimu vizuri katika nchi yetu, kitasimamia kwa haki na kitahakikisha kwamba kila mmoja anayehusika na elimu anafuata utarabu. Unaona kabisa kwamba kwenye taasisi au Wizara nyingine kuna vyombo kama OSHA, EWURA, hizi ni regulatory bodies. Kwa hiyo, sisi elimu tuwe nayo basi kusudi elimu yetu sasa isiguswe na mtu, asitoke mtu alikotoka akasema hiki kiwe hivi, hiki kiwe hivi, ikae hivyo na isimamiwe hivyo naomba sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ni suala Sera ya Elimu ya mwaka 2014, suala hili leo hii ndiyo linaleta mkanganyiko. Sera mpya ya Elimu imeanza kutumika na watoto walioanza kutumia sera hii mpya leo wako darasa la nne. Niungane na Mheshimiwa Bulembo aliyesema kwamba hivi itakuwaje, tunaomba Mheshimiwa Waziri utakapokuja hapa utuambie kwamba watoto hawa waliopo darasa la nne leo watafika darasa la sita ama wataishia darasa la saba ili kusudi hata wazazi huko mitaani tuwajenge kisaikolojia wawe wanajua nini kitafanyika. Sera hii ya Elimu pamoja na kuizindua wakati ilipozinduliwa maandalizi yalikuwa bado, ndiyo maana leo unaweza ukakuta sera ipo haina sheria, sera ipo haina kanuni, matokeo yake linaweza likatokea kundi lisilojulikana likaja likaipeleka Serikali Mahakamani kupinga sera hii na mkashindwa hata kujitetea kwa nini mnatoa elimu kwa kutumia sera hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niwaombe sana tufuate utaratibu wa sera, leteni sheria Bungeni, sheria ipitishwe wekeni na kanuni zake kusudi sera hii ikae vizuri. Vilevile andaeni vitabu na mviweke katika msingi kwamba zinafuata sera hiyo kuliko sasa tunaambia vitabu vya darasa la nne havipona wakati mwingine mnaambiwa mtaala upo lakini vitabu hakuna, mafunzo kwa walimu hakuna kwa sababu sera hii tumeiendea haraka mno. Kama tumeiendea haraka tujitahidi kwa sababu watoto sasa wako darasa la nne. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni suala la ufaulu. Ni kweli ufaulu unasikitisha, ni-declare interest kwamba mimi ni mmiliki wa shule, lakini ufaulu katika shule za umma unasikitisha. Kinachosikitisha si kingine si kwamba hakuna walimu, bali mazingira siyo mazuri Serikali ijitahidi kuweka mazingira mazuri. Hata kama unapata majibu rahisi, ukikutana na watendaji wa Serikali wanakwambia nyie private si mnachuja, huwezi kuchuja darasa zima lakini Serikali una uwezo wa kuchuja, una shule za vipaji Ilboro, Mzumbe, zipo zile shule na mmekuwa mkipeleka hao mnaowachuja vilevile. Kwa hiyo, mimi nafikiri Serikali iandae mazingira mazuri ili kusudi...

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana, naunga mkono hoja na nawatakia kila la kheri Wizara ya Elimu wafanye kazi vizuri.