Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

Hon. Tunza Issa Malapo

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

MHE. TUNZA I. MALAPO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Awali ya yote nataka kusema kwamba elimu ni uwezo si idadi tu ya watu ambao wanaingia shuleni. Tunatarajia watoto wanaoingia wafundishike, wawe na uwezo wa kutatua changamoto zilizopo katika mazingira yao; hapo tutapata maendeleo katika elimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Mheshimiwa Waziri akija atujibu kwa ufasaha kuhusu hivyo vitabu vya darasa la nne ambavyo mpaka sasa hivi bado havijafika shuleni, watoto wetu wanajifunza kwa kutumia kitu gani? Ukifungua katika hotuba yako ukurasa wa 69 yaani tunaanza mbele kabla ya nyuma. Ukurasa wa 69.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukurasa wa 69 pale namba 62 roman (ii) inasema; “Mradi wa kuendeleza elimu ya ualimu imeandaa mapitio ya mitaala wa elimu ya ualimu ili kuwa na mtaala unaokidhi mahitaji ya sasa na unaoendana na mtaala wa elimu msingi ulioboreshwa.”

Mheshimiwa Mwenyekiti, muone mambo ya ajabu ya Serikali ya CCM, kumbe mpaka wanapeleke mtaala shule za msingi, huku kwenye ualimu hawajawafundisha. Tunategemea walimu wale wakawafundishe wale watoto ambao mtaala ule hawaujui sasa wanaenda kufundisha kitu gani. Mheshimiwa Waziri naomba unapokuja hapa uje na majibu, haya ni maneno yako siyo ya kwangu nimekwambia ukurasa wa 69 roman (ii). (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nazungumzia vyuo vya ualimu; hawa watu wamesahaulika sana. Wakufunzi wa vyuo vya ualimu wamesahaulika, mimi nimetoka kule, takriban wazungumzaji wote waliozungumza hapa hawajataja vyuo vya ualimu. Wakufunzi wanadai, morale imeshuka, wana matatizo mengi katika kazi yao ya ualimu. (Makofi)

Mheshimiwa Waziri una vyuo 35 tu vya ualimu nchi hii, mwenzako Mheshimiwa Jafo ana shule za msingi ngapi, ana shule za sekondari ngapi lakini wewe una vyuo vya ualimu 35, naomba uende ukawasikilize, utatue matatizo yao. Shida ya ualimu inatokea huko kwa sababu watu wamechoka, mpaka leo unamwambia amfundishe mwalimu, mtaala wenyewe maskini haujui anamfundisha kitu gani?

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakwenda kwenye fedha za ruzuku. Hizi fedha zimekadiriwa tangu mwaka 2001; mwaka 2001, shilingi 10,000 kwa mtoto wa shule ya msingi, shilingi 25,000 kwa mtoto wa sekondari. Katika hiyo shilingi 10,000 shilingi 4,000 inabakia Serikali haiendi shuleni kwa ajili ya ununuzi wa vitabu. Sasa nakuuliza Mheshimiwa Waziri shilingi 6,000 inayoenda shule kumgharamia mwanafunzi kwa karne hii inatosha? Na kama haitoshi utuambie mkakati wa makusudi ambao umeuweka wa kuhakikisha kwamba hiyo fedha inaongezwa. Pendekezo langu ifike shilingi 20,000 kwa mtoto wa shule ya msingi na ifike shilingi 50,000 kwa mtoto wa shule ya sekondari. Pia uniambie katika hiyo 4,000 inayobakia Serikali Kuu imenunua vitabu kiasi gani na kwa takwimu zipi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, fedha za maendeleo; katika Wizara ya Elimu fedha zinazotengwa ni chache karibu zote asilimia 100 ya fedha za maendeleo mnategemea wahisani, ninyi mapato yenu ya ndani hayatengi fedha za maendeleo. Sasa nataka kukuuliza Mheshimiwa Waziri tunajua kuna miradi mingi, kwa mfano mradi wa KKK, ni mradi mzuri ambao implementation yake ingekuwa nzuri tunaamini ingesaidia, lakini mnategemea wahisani. Mtuambie nyinyi kwenye mradi huu mmeweka kiasi gani na mmefuatilia kwa kiasi gani mradi huu unaweza kufanya kazi vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la walimu wa sayansi tumekuwa tukiliongea na tutaendelea kulio... (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)