Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

Hon. Margaret Simwanza Sitta

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Urambo

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

MHE. MARGARET S. SITTA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi lakini vile vile namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa nafasi ya kusimama humu Bungeni siku ya leo na wakati huo nawashukuru wapiga kura wa Urambo ambao wanaendelea kunipa ushirikiano. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nichukue nafasi hii kwanza kupongeza Rais Magufuli kwa kazi nzuri anayoifanya na hasa kwa hii elimu bure. Kwa kweli hata kwenye Wilaya yangu Urambo imesaidia sana kuongeza wanafunzi madarasani, namwombea kwa Mungu aendelee kufanya kazi nzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati huo huo nachukua nafasi kumpongeza Profesa Ndalichako, Naibu Waziri wake, Makatibu Wakuu na wasaidizi wake na watendaji wote wa Wizara ya Elimu kwa kazi nzuri wanayofanya. Jamani Wizara ya Elimu si mchezo mimi nimekaa pale kwa miaka miwili na nusu ni kazi kubwa, hongera Profesa Ndalichako, kazi ni kubwa na unaiweza, Mungu akusaidie usikilize tu yale tunayopendekeza ya kusaidia kuboresha yale unayoyafanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi naunga mkono Waheshimiwa Wabunge wote walioongea hapo awali waliopendekeza kuwe na Independent Education Regulatory Board. Kwa jinsi hali ya elimu inavyokwenda lazima tuwe na chombo ambacho kitaangalia na kuchambua Sera ya Elimu ikoje, itaangaia elimu ya msingi maana yake nini, kwa sababu mpaka sasa hivi watu wengi hawajui maana ya elimu ya msingi inatoka wapi inakwenda wapi. Kwa hiyo, Regulatory Board itatusaidia kuelewa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia itazungumzia suala la lugha za kufundishia, tuendeje wakati huu wa karne hii ya 21 wakati huo huo itaangalia mitihani inayotungwa iendelee kama ilivyo au iangalie aina ya shule, mazingira ya shule na kadhalika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo mimi naunga mkono kwamba kuwe na Independent Education Regulatory Board. Kwenye Sheria ya Elimu ilivyo sasa hivi kuna chombo kinaitwa Education Advisory Board hakifanyi kazi, kwa hiyo, mimi naomba kabisa Serikali itusikie wengi ambao tumeongea kwamba kuwe nan Independent Education Regulatory Board.

Mheshimiwa Mwenyekiti, humu ndani huwa tunaongea sana, tunapiga sana vita ndoa za utotoni, lakini niambie kwenye Jimbo langu kama Urambo, mtoto amemaliza darasa la saba hakuchaguliwa, wazazi wake hawana uwezo kumpeleka private, anafanya nini? Mimi huwa najiuliza sana, ili huyu mtoto afikie umri wa kuolewa anafanya nini?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, mimi napendekeza kwa Serikali itilie mkazo sana vyuo vya maendeleo ya wananchi, FDCs, lakini pia VETA. VETA zikitoa mafunzo ya aina mbalimbali ambayo wasichana hata na wavulana pia watakwenda yatawasaidia kukua kidogo, lakini niambie mahali ambako hakuna VETA kama Wilaya ya Urambo, FDC haina hela, huyu mtoto wa kike ili nimtunze mimi mpaka afikie umri wa kuolewa anafanya nini pale nyumbani?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, mimi natoa wito kwa Serikali itusaidie kuwa na Vocational Training Centres nyingi ili angalao ziwafanye wototo wapate ujuzi ambao utawasaidia kwenye hii sera ya viwanda, lakini pia na wenyewe kujiajiri, ili angalao kuwafanya wakue kidogo kuliko kuwaacha kama ilivyo.

Kwa hiyo, wakati huu naomba nitoe ombi kwa Mheshimiwa Waziri Urambo haina VETA, karibuni nitaleta barua ili watoto wangu wa kike wakuekue kidogo, wajifunze sayansi kimu, wajifunze ushonaji na mambo mengine, mapishi wawe ma-caterers na kadhalika, kwa hiyo, nitaleta ombo maalum Mheshimiwa Waziri kwenye ofisi yako. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia hili jambo ambalo naliongelea sasa hivi ni suala la TSC. Nimeshasema jambo hili mpaka wakati mwingine natamani sijui nilie hivi au nifanyeje? Maana ya TSC ni nini na functions zake ni nini? Mimi nakuomba Mheshimiwa Waziri, najua iko TAMISEMI, ilishtukia tu ikahamia TAMISEMI, lakini mimi kwa maoni yangu ungeniuliza ingekuwa kwako Mheshimiwa, kwa sababu wewe ndiye unayetaka Sera ya Elimu ifanye kazi, hawa watu wanavyohudumiwa ni sawa? Wanatekeleza sera yako kama ilivyo?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, mimi ningeomba msaidiane na Mheshimiwa Jafo, Waziri wa TAMISEMI, mupime hiki chombo TSC kinafanya kazi iliyokusudiwa au ni li jitu tu limekaa au unaweza kuita a white elephant? TSC inafanya nini? Imerahisisha vipi kutoa huduma kwa walimu?

Mheshimiwa Mwenyekiti, na mimi ninaamini kabisa ukimtaka mwalimu afanye kazi vizuri, wanasema wajibu na haki. Je, hii TSC inafanya kazi iliyokusudiwa? Ukiangalia majukumu yake mengi tu kuajiri, kuhamisha, sijui kufanya nini, inafanya kazi hiyo? Ili kurahisisha kweli wanaotekeleza Sera ya Elimu wafanye kazi vizuri?

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ningeomba kuishauri Serikali kuhusu mtoto wa kike. Kuna wakati mimi nilifanya kazi Wizara ya Elimu kwenye miaka ya themanini na kitu palikuwa na kitengo kilichokuwa kinaangalia elimu ya mtoto wa kike. Mimi ningeshauri kwa hali ilivyo ya watoto wa kike na mambo tunayoyaona, napendekeza kwa Serikali kwamba iwe na kitengo kinachoangalia mtoto wa kike na elimu. Kwa sababu ukichukua pale wanapoanza elimu ya msingi wote wako karibu idadi sawa tu, inaweza kuwa 50/50, lakini ukiangalia inaenda kwa msonge mpaka unafika chuo kikuu wote wameshaisha hapa njiani. Sasa kulikuwa na haja ya kuwa na chombo ambacho kitamshughulikia mtoto wa kike.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi naomba niwaambie Serikali kwamba, haijafikia hatua ambayo tukaridhika, kwamba watoto wa kike na wa kiume wanaenda sawa kwa upande wa elimu. Kwa hiyo, natoa wito kwa Serikali kuwa na kakitengo kadogo ambako zamani kalikuwepo, sijui Serikali iliridhika ikakaondoa. Mimi nilikuwa naomba bado kitengo cha kumuangalia mtoto wa kike na elimu kirudishwe, ili watoto wa kikenao wafike kama wenzao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini lingine ni in-service training. Naishauri Serikali in-service training, yaani mafunzo kazini yanavyotolewa mpaka sasa kwangu mimi naona bado. Nimesoma kitabu nimeona idadi ya walimu waliopata mafunzo ni wachache sana. Naomba Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi bado ibebe jukumu la mafunzo kazini kwa ajili ya walimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, walimu wanapotoka chuoni wengine wameshafundisha miaka 30 wanahitaji kupigwa msasa ili waende na wakati. Kwa hiyo, mimi naomba kabisa kwamba, in-service training bado inahitaji kufanyiwa kazi na kusimamiwa na Wizara ya Elimu yenyewe, lakini ukiwapa TAMISEMI kwa jinsi ambavyo Wilaya zilivyo, Wilaya nyingine zitakwenda juu nyingine zitabaki chini. Kwa hiyo, mimi nilikuwa nafikiria kwa upande wa mafunzo kazini Mheshimiwa Waziri tusaidie ili in service training iendelee kutolewa na Wizara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia, nilitaka niipongeze Serikali kwa hii performance based (P4R). Mimi nimeipenda sana kwa sababu, utaratibu ulioko sasa hivi unakwenda kwenye shule, shule yenyewe inaangalia utaratibu gani wa kutafuta fedha, kwa hiyo, inapunguza gharama kuliko ile ambayo fedha inachukuliwa anapewa mtu contractor na nini. Kwa hiyo, mimi nilikuwa nafikiri hii P4R ni nzuri, naomba tu iendelee. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia nadhani la mwisho ambalo ningependa kulizungumzia ni suala la ukaguzi. Bado mimi kwa mtazamo wangu na understanding yangu, tunahitaji chombo cha ukaguzi kinachojitegemea. Wakaguzi walivyo bado wako chini ya idara, hawapewi fedha za kutosha, lakini kule Wilayani kwenye Halmashauri wanapokosa mafuta kwenda kukagua wanamuomba Mkurugenzi. Huyu uliyekwenda kumpigia magoti asubuhi, ukamuomba mafuta ya dizeli au petroli, huyo huyo akakusimanga ukaenda ukamkagulia shule zake halafu jioni unamletea taarifa, ataisoma?

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kama kukiwa na independent kabisa chombo ambacho kinaangalia quality assurance na jinsi idadi ya taasisi zinazotoa elimu zilivyoongezeka kwa kweli, nakusihi kabisa Mheshimiwa Waziri anayehusika muangalie umuhimu wa kuwa na chombo cha ukaguzi kinachojitegemea ili kikague shule za Serikali na shule za binafsi bila kujali kwamba haya mafuta yametolewa. Kwa sababu, watakuwa wanajitegemea wanapata mafuta yao wao wenyewe kuliko kwa hali ilivyo bado ni idara tu ndani ya Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo mimi naomba nimpongeze Mheshimiwa Dkt. Ndalichako na wote wanaofanya kazi katika Wizara ya Elimu nikiamini kwamba wametusikiliza mengi na hasa hili la Independent Education Regulatory Board. Kwa kweli, Mungu awasaidie abariki kazi yenu ni ngumu, lakini mnajitahidi kadiri muwezavyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.