Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

Hon. Felister Aloyce Bura

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

MHE. FELISTER A. BURA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia asubuhi ya leo na nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa nafasi ya kusimama katika Bunge lako hili tukufu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama walivyosema Wabunge wengine na mimi niungane nao kumpongeza sana Mheshimiwa Profesa Ndalichako kwa kazi nzuri anayofanya na alianza kufanya hata kabla hajawa Waziri, alikuwa mtumishi mwema kule alikokuwa NACTE na naamini anaendeleza utumishi huo, mimi sina la kukwambia zaidi ya kukuombea kwa Mwenyezi Mungu na kuwaombea watumishi wengine wa Wizara hii kwa Mwenyezi Mungu ili kazi yao iendelee kuwa njema. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi hii pia kupongeza Serikali kwa progaramu ya lipa kulingana na matokeo (EP4R), kwa programu hii wamefanya kazi kubwa ya ukarabati wa shule kongwe nchini. Katika mkoa wangu wa Dodoma wamekarabati shule ya sekondari Mpwapwa, shule ya sekondari Dodoma, shule ya sekondari Bihawana na Shule ya sekondari ya Msalato pia. Wanafanya kazi nzuri, shule hizi zilikwishachakaa na siku moja tuliingia katika vyoo vinavyotumika katika shule hizi nilishangaa uwepo wa Mungu kwa wanafunzi, kwa sababu nilishangaa watoto hawapati fungus, shule ilikuwa yanatisha hasa vyoo na mabweni.

Kwa hiyo niombe sana Serikali waendelee na programu hii na Mheshimiwa Waziri nikuombe Dodoma sasa ni Makao Makuu na hatuna majengo shule ya mfano na hasa ya wasichana katika Mkoa wa Dodoma, kama kuna uwezekeno programu hii itusaidie kujenga shule kubwa ya kitaifa, shule ya wasichana ambapo wasichana watajengewa mabweni, walimu watakuwa wa kutosha na iwe shule ya sayansi, tunawataka wasichana ambao watasoma sayansi kusaidia Taifa hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru pia kwamba tumeona Waraka Na. 2 wa mwaka 2016 unayozungumzia kiwango cha ufaulu kwamba mwanafunzi wa form two akipata “D” mbili anaruhusiwa kuendelea na elimu, anaruhusiwa kusonga mbele darasa lingine, lakini hao wanafunzi wanaoruhusiwa kwa “D” mbili kwenda form three au kidato cha tatu ndiyo hao tunaowategemea kwenda vyuo vikuu, tunawaruhusu kwa ufaulu mdogo mno.

Mheshimiwa Waziri wewe ni Profesa, unajua ulivyo- fight kupata uprofesa wako, hukwenda na “D” mbili kidato cha tatu, kuna haja ya kubadilisha ufaulu kwa watoto wa sekondari tunawandaa wanafunzi kuwa maprofesa, tunataka watoto wetu wawe maprofesa kama wewe, tunataka wawe madaktari ufaulu wa chini wa “D” mbili haufai na umepitwa na wakati Mheshimiwa Waziri, niombe Serikali sasa na ukimwambia mtoto “D” mbili anakwenda kidato cha tatu hajishughulishi na kusoma na hata walimu hawaongezi bidiii katika kufundisha kwa sababu anajua mtoto akipata “D” mbili anaingia kidato kingine. Kwa hiyo, niombe sasa kuwepo na ushindani ili wanafunzi wajishughulishe na walimu wajishughulishe kuwaandaa watoto. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie pia wanafunzi wanaomaliza kidato cha nne hawapati nafasi ya kuingia kidato cha tano na wale wanaomaliza kidato cha sita wanashindwa kupata nafasi ya kuendelea na vyuo vikuu. Wanafunzi hawa wanarudi mitaani, lakini wanaporudi mitaani hawana kazi za kufanya, tunasema Serikali iwape asilimia tano ya mapato ya Halmashauri zetu ili wajiandae kuwa wajasiriamali, hawana elimu ya ujasiriamali pamoja na elimu wanayopata kwa muda mfupi kwa Maafisa Maendeleo ya Jamii lakini haiwasaidii sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali ikiimarisha VETA, ikaimarisha JKT na ikapeleka vifaa kwa ajili ya kujifunzia, watoto wetu wanaomaliza kidato cha nne wakaenda VETA wale wanaomaliza kidato cha sita wakashindwa kuendelea na masomo wakaenda VETA wakitoka kule watakuwa na stadi ya kuwatosha kujitegemea na hata Serikali unapotoa mkopo kwa ajili ya ujasiliamali wanapopewa mikopo ya kutoka Halmashauri zetu watakuwa na uwezo wa kujitegemea. Tunapowapa mikopo na elimu hiyo wanayotoka nayo ya nadharia sidhani kama elimu hiyo inawasaidia na matokeo yake asilimia 40 tu ya mikopo ya vijana inarudishwa asilimia 60 wanashindwa kurudisha kwa sababu hawana elimu ujasiliamali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie tafiti zinazofanywa na vyuo vikuu na hasa Chuo Kikuu cha Kilimo (SUA). Tunategemea SUA iwasaidie wakulima wetu tafiti wanazozifanya za mazao, tabianchi, itusaidie katika kukuza kilimo, lakini tafiti hizi haziwafikii wakulima. Tafiti hizi zinaishia kwenye makaratasi na sana wanafaidi aidha wanaokaa Morogoro na wale ambao wanajuhudi za kufuatilia tafiti hizi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, SUA imeanzishwa kutusaidia ninaomba sasa tafiti za mazao zinazofanywa na SUA ziwafikie wakulima na ziwasaidie wakulima, mbegu wanazozifanyia tafiti zifike kwa wakulima wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna shida sana na walimu, nyumba za walimu, upungufu wa walimu wa sayansi, hili limezungumzwa na litaendelea kuzungumzwa na Wabunge, Serikali ione namna sasa, elimu bure wanafunzi wengi wanasoma, lakini madarasa ni yale yale, madawati ni yale, walimu wameongezeka kidogo, lakini wa sayansi hatuna hilo Serikali ione namna ya kutusaidia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri amezungumzia pia ubunifu kwamba wanawajenga wanafunzi, wanawajenga watu katika ubunifu, lakini tusipoanza katika elimu ya sekondari hatutapata wabunifu wazuri hata katika mambo ya uchoraji, engineering na michezo kama hatutawajenga wanafunzi vizuri hatutawapata.

Pia kuhusu elimu ya TEHAMA, katika shule za sekondari hakuna elimu ya TEHAMA kama ipo ni shule za private, lakini shule za Serikali kama wanafundishwa ni nadharia, basi tuone namna wanapotoka sekondari wanaokwenda vyuo vikuu wanatamani kuwa wasomee masomo ya TEHAMA lakini anapoanzia kule kwanza lugha yenyewe ya kubabaisha ya kiingereza, lakini la pili hajawahi kuiona hiyo computer alipokuwa shule ya msingi wanayoiona computer ni wale ambao wanasoma shule za private. Serikali ijenge uwezo kwa Walimu na kujenga miundombinu katika shule zetu za sekondari za Serikali kwamba TEHAMA wanaianzia sekondari na anaanza akiwa na vifaa vya kutosha kusomea, miundombinu ianzie sekondari.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.