Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi

Hon. Edward Franz Mwalongo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Njombe Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi

MHE. EDWARD F. MWALONGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, asante kunipa nafasi nichangie katika hotuba iliyopo mbele yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ama kweli baniani mbaya kiatu chake dawa, Jeshi la Polisi wanalaumiwa lakini wanafanya kazi nzuri sana kwa sababu nasema kama polisi wasingekuwepo hali ingekuwaje? Usipomchokoza polisi hawezi kuhangaika na wewe, ukiona polisi wanashughulika na wewe ujue kwamba kuna kitu umekifanya kwamba umeenda kinyume na utaratibu na kinyume cha sheria. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nawapongeza sana Jeshi la Polisi kwa kazi nzuri wanayoifanya, wote tupo salama siku zote za maisha yetu kwa sababu ya Jeshi la Polisi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Jeshi la Polisi katika Mkoa wa Njombe bado Serikali haijalitendewa haki vizuri, Jeshi la Polisi hawajatendewa haki vizuri kwa sababu Njombe ni mkoa toka mwaka 2013 lakini mpaka leo hawajajengewa jengo la polisi la mkoa, hakuna Ofisi ya RPC, hakuna nyumba za polisi, polisi wale wa Njombe wanafanya kazi vizuri lakini hawana makazi. Polisi 400 vijana hawana makazi, hakuna nyumba hata moja ya polisi Njombe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kitendo hiki nakiona kwamba hatuwatendei haki askari wetu na wakati mwingine tunaweza tukawalaumu polisi kwamba hawatimizi wajibu wao vizuri, lakini wakati mwingine pengine wanapata na msongo kutokana na mazingira ya kazi wanayofanya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukienda Kituo cha Polisi Njombe nafikiri Mheshimiwa Waziri alifika alikiona, kile kituo nadhani ni cha mkoloni nimezaliwa nimekikuta. Kile kituo kwanza kipo ndani ya mita 30 za barabara halafu ni kichakavu sana. RPC wa Njombe kila siku anabomoa kaukuta angalau aongeze apate chumba cha kumtosha kufanya kazi. Kwa kweli hadhi ya polisi kwa Njombe bado haijawa sawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niombe sana Jeshi la Polisi Njombe waangalie kwa namna gani wanaweza wakasaidia kama Wizara na kama Serikali kuona kwamba Jeshi la Polisi linakuwa na jengo lake, linakuwa na ofisi nzuri na wanaweza kufanya kazi vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Jeshi la Magereza; kwanza kabisa katika Mkoa wa Njombe Magereza Mkoa haijafika. Maafisa wa Magereza Njombe wakihitaji mahitaji yao ya kiofisa ni lazima waende Iringa. Sasa je tukubaliane hapa kimsingi kwamba Magereza wamegoma kuja Njombe ama wanakuja? Nami kama wananiambia wamegoma nipo tayari kumwambiwa mwenye nchi kwamba magereza wamegoma kuja Njombe. Tunahitaji watu wa magereza waje Njombe ili kusudi shughuli zinazohusiana na Jeshi la Magereza ziweze kufanyika vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Askari Magereza Njombe wanafanya kazi nzuri sana, tarehe 2, nakumbuka ilikuwa Jumatatu ya Pasaka nilitembelea Magereza Njombe, niliongea na wafungwa, niliangalia makazi yao, lipo tatizo moja tu la msongamano lakini wafungwa wenyewe kwa maneno yao walitamka kwamba wanalelewa vizuri na wanatunzwa vizuri. Nilitembelea vyumba vyao vipo vizuri na wanasema kwamba maisha pale, ukiacha kwamba wao ni wafungwa na mahabusu lakini maisha ni mazuri na wanatendewa haki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilifika nikamweleza Mheshimiwa Waziri, lakini nilipata fursa ya kuuliza swali hapa na nikawa na mahabusu mmoja pale alikuwa anaumwa, namshukuru sana alichukua hatua haraka na mahabusu yule ametibiwa. Tatizo kubwa la Magereza Njombe ni uchakavu na msongamano, lakini msongamano huu unatoka wapi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa msongamano unasababishwa na kesi zisizokwisha mahakamani na upelelezi ambao haukamiliki. Kwa hiyo, ni kati ya Jeshi la Magereza na polisi kwa maana kwamba polisi hawapelelezi kesi kwa wakati na magereza wanashindwa kuwatunza wale mahabusu vizuri kwa sababu ya nafasi ni ndogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine linalojitokeza ni kwamba Magereza Njombe wana maeneo ya mashamba, maeneo yale hayatumiki, yamekuwa mapori kwa miaka mingi sana. Niombe sana Jeshi la Magereza hebu waone ni kwa namna gani wanaweza wakayatumia yale maeneo, vinginevyo sisi kama wananchi wa Njombe tutayavamia yale maeneo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikirudi katika matumizi ya ardhi ni kwamba sisi tukivamia ardhi ile tukiilima wasije wakatulaumu, lakini ni wajibu wao kuhakikisha kwamba Magereza Njombe wanalima mashamba yale na wanayafanyia kazi ili kusudi tuondokane na mapori hayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo nililiona pale Magereza Njombe pamoja na uzuri niliouona ndani ya gereza, usafi na mazingira ya ndani ni kwamba yule afisa magereza anakaimu. Mheshimiwa Waziri hebu angalieni kwa nini yule anaonekana msomi na anamudu kazi vizuri, kwa nini aendelee kukaimu siku zote hizo kwa sababu inamsababisha anashidwa kutoa maamuzi kwa sababu ya kukaimu. Niombe sana waliangalie hilo kiutumishi waone namna gani wafanye. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la uhamiaji haramu, nimeenda Gereza la Njombe nimekuta pale kuna watu wa Ethiopia 15 walikamatwa wakapelekwa mahakamani, wamehukumiwa wamemaliza kifungo lakini bado wapo gerezani, sababu wanasema hawajasafirishwa. Gereza lile ni dogo wanasababisha msongamano, halafu kesi imekwisha bado wanaendelea kuwepo gerezani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hebu niombe kama utaratibu wetu sisi ni kuwakamata hawa wanaoitwa wahamiaji haramu, basi tuangalie utaratibu mwingine wa kufanya, kwa sababu naamini kama tunaweza tukawakamata, kama tumewakuta kwenye lori tunamwambia dereva wa hilo lori, nyuma geuka, mbele tembea, rudi ulipotoka, kuliko anaenda kukamatwa Njombe anakaa Magereza ya Njombe anahukumiwa, matokeo yake anasabisha msongamano katika Gereza la Njombe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, matatizo haya naona yapo sehemu nyingi sana katika nchi yetu kwamba Jeshi la Magereza linapata tabu kutunza hawa wahamiaji haramu. Kama ni watu wanaopita njia tu tuangalie sheria zimekaaje; kama inawezekana kuwasindikiza wakamaliza msafara wao tuwasindikize wavuke waende wanapokwenda kuliko tunaendelea kubabaika nao hapa. Kwanza wanakula sembe yetu ya bure, hawatakiwi kwenda kazini tumewapeleka mahakamani, tunatumia nguvu zetu nyingi kuwatunza bila hata sababu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niliombe sana Jeshi la Uhamiaji waweze kuangalia hili jambo na Serikali iliangalie kwa umakini ili kusudi hawa watu waweze kurudi kwao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni suala la usalama barabarani, tunashukuru sana Askari wa Usalama Barabarani wanafanya kazi vizuri lakini wapo miongoni mwao hawafanyi kazi vizuri. Askari wa usalama barabarani wamegeuza kile kitengo kwamba ni sehemu ya kipato, wananyanyasa sana vijana wa bodaboda na maaskari wa usalama barabarani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, imeshatokea mahali pengine unakuta askari wa usalama barabarani amesimamisha gari katikati ya barabara halafu amefungua milango wa gari ili kusudi yule kijana asimame kwa ghafla au aingie porini ili amkamate, kuna sababu gani? Kwa sababu bodaboda zote zinajulikana ni za wapi, haiwezekani bodaboda ikawa inatoka Tabora kuja Dodoma haiwezekani. Kama ni bodaboda ya hapa Dodoma ni ya Dodoma na kama ni ya Njombe ni ya Njombe. Naomba vijana hawa waangaliwe, kama wana makosa basi wakamatwe kwa utaratibu wa ukamataji; wapo askari ambao kwa kweli ukamataji wao hauridhishi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwaombe sana tuwasaidie sana askari, tuwaelimishe vizuri ili kusudi ukamataji wao uweze kuwa ni ukamataji ambao unaweza ukamsaidia hata yule unayemkamata ajue ana kosa gani kuliko unapofungua milango ya gari halafu unataka mwenye bodaboda ajigonge kwenye milango ya gari au aingie porini ili umkamate, kwa hiyo ukamati huo sio ukamataji sahihi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, nashukuru sana kwa kunipa muda. Ahsante.